Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuepuka Kupendezwa na Watu Wasiofaa?

Ninawezaje Kuepuka Kupendezwa na Watu Wasiofaa?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kuepuka Kupendezwa na Watu Wasiofaa?

“Nilianza kushirikiana na msichana fulani shuleni. . . . Hakutumia dawa za kulevya, wala kwenda kwenye karamu zisizofaa, naye hakuwa na wapenzi wengi. Hata hakutumia maneno machafu, naye alipata maksi za juu. Lakini kwa kweli hakuwa rafiki anayefaa.”—Beverly. *

KWA nini Beverly alifikia mkataa huo? Sasa anatambua kwamba msichana huyo alimfanya ajihusishe na mazoea yenye kudhuru. Beverly anaeleza: “Nilipoendelea kushirikiana naye, nilianza kusoma vitabu vinavyohusiana na pepo, na hata nikaandika hadithi kuhusu mambo hayo.”

Msichana anayeitwa Melanie pia alishawishiwa ajihusishe na mwenendo usiofaa, lakini mtu aliyemwongoza afanye hivyo alidai kuwa Mkristo mwenzake! Unawezaje kujua ikiwa mtu atakuwa rafiki mzuri? Je, nyakati zote ni hatari kushirikiana kwa ukaribu na watu wasioamini? Je, urafiki kati ya Wakristo huwa mzuri nyakati zote?

Lakini vipi kuhusu urafiki na mtu wa jinsia tofauti? Ikiwa ungependa kufunga ndoa na mtu fulani, unawezaje kujua ikiwa atakuwa na uvutano mzuri kiroho? Na tuone jinsi kanuni za Biblia zinavyoweza kutusaidia kujibu maswali hayo.

Ni Marafiki Gani Wanaofaa?

Kwa kuwa mwanashule wa Beverly hakumwabudu Mungu wa kweli, je, Beverly alipaswa kujihadhari kuhusu kufanya urafiki naye? Kwa kweli, Wakristo wa kweli hawasemi kwamba mtu ana mwenendo usiofaa au ni mwenye maadili mabaya kwa sababu tu yeye si mwamini mwenzao. Lakini mtu anapotaka kuwa na rafiki wa karibu, ni vizuri kuwa mwangalifu. Mtume Paulo aliwaonya hivi watu katika kutaniko la Korintho la karne ya kwanza: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Alimaanisha nini?

Huenda baadhi ya Wakristo hao Wakorintho walikuwa wakishirikiana na Waepikurea waliokuwa wafuasi wa mwanafalsafa Mgiriki Epikurasi. Ni kweli kwamba Epikurasi aliwafundisha wafuasi wake waishi kwa utimamu wa akili, ujasiri, kujizuia, na haki. Hata aliwaonya dhidi ya kufanya makosa ya siri. Kwa hiyo, kwa nini Paulo aliwaona Waepikurea, na wengine katika kutaniko waliokuwa na maoni kama hayo kuwa “mashirika mabaya”?

Waepikurea hawakumwabudu Mungu wa kweli. Kwa kuwa hawakuamini kwamba kuna ufufuo wa wafu, walihangaikia hasa maisha ya sasa na jinsi ambavyo wangepata faida. (Matendo 17:18, 19, 32) Haishangazi kwamba kwa kushirikiana na watu kama hao, wengine katika kutaniko la Korintho walianza kupoteza imani katika ufufuo. Ndiyo sababu katika 1 Wakorintho sura ya 15, ambapo tunapata onyo la Paulo kuhusu mashirika mabaya, kuna maelezo mengi yaliyoandikwa ili kuwasadikisha Wakristo hao wa mapema kuhusu uhalisi wa tumaini la ufufuo.

Tunajifunza nini? Hata watu wasiomwogopa Mungu wanaweza kuwa na sifa nzuri. Lakini ukiwafanya wawe marafiki wa karibu, wataathiri fikira, imani, na mwenendo wako. Kwa hiyo, katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, Paulo alisema: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.”—2 Wakorintho 6:14-18.

Fred, mwenye umri wa miaka 16, alijifunza hekima ya maneno hayo ya Paulo. Mwanzoni alijiunga na kikundi cha utendaji fulani wa baada ya shule ambao ungewafanya wasafiri kwenda nchi fulani inayositawi ili kuwafundisha watoto. Hata hivyo, yeye na wanafunzi wenzake walipokuwa wakijiandaa, Fred alibadili maoni. Alisema hivi: “Niliona kwamba kutumia wakati mwingi pamoja nao kungedhuru hali yangu ya kiroho.” Kwa sababu hiyo Fred aliamua kuacha utendaji huo na kuwasaidia watu wenye uhitaji katika njia nyingine.

Urafiki Kati ya Wakristo

Lakini vipi urafiki ndani ya kutaniko? Akimwandikia kijana Timotheo, Paulo alionya: “Ndani ya nyumba kubwa mna vyombo vya dhahabu na fedha, na pia mna vyombo vya miti na vya udongo, na vingine ni kwa ajili ya kusudi lenye kuheshimika lakini vingine ni kwa ajili ya kusudi lenye kukosa heshima. Kwa hiyo, kama yeyote akijiepusha kabisa na hawa wa mwisho, atakuwa chombo kwa ajili ya kusudi lenye kuheshimika, kilichotakaswa, chenye faida kwa bwana wake, kilichotayarishwa kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 2:20, 21) Kwa hiyo Paulo hakusahau kutaja ukweli wa kwamba hata kati ya Wakristo, kunaweza kuwa na wale wasiojiendesha kwa heshima. Naye hakusita kumwambia Timotheo ajiepushe nao.

Je, hilo linamaanisha kwamba unapaswa kuwashuku Wakristo wenzako? La. Wala haimaanishi kwamba unapaswa kutazamia rafiki zako wawe wakamilifu. (Mhubiri 7:16-18) Hata hivyo, kwa kuwa tu kijana huhudhuria mikutano ya Kikristo au wazazi wake ni wenye bidii katika kutaniko haimaanishi kwamba ni vizuri kuwa na urafiki wa karibu pamoja naye.

“Kwa matendo yake, mvulana [au msichana] hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu,” inasema Methali 20:11. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kujiuliza: Je, uhusiano wake na Yehova ndilo jambo kuu maishani mwa mtu huyu? Au, badala ya hivyo, je, kuna mambo yoyote yanayoonyesha kwamba “roho ya ulimwengu” ndiyo inayoongoza kufikiri na mtazamo wake? (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2) Je, unaposhirikiana naye unatiwa moyo zaidi umtumikie Yehova?

Ukichagua marafiki wanaompenda sana Yehova na mambo ya kiroho, utaepuka matatizo na vilevile utapata nguvu zaidi za kumtumikia Mungu. Paulo alimwambia Timotheo: “Fuatilia uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wanaomwitia Bwana kutokana na moyo safi.”2 Timotheo 2:22.

Urafiki na Watu wa Jinsia Tofauti

Ikiwa una umri wa kutosha na unataka kufunga ndoa, je, umefikiri kuhusu jinsi unavyoweza kutumia kanuni hizo unapochagua mwenzi? Kuna sababu nyingi zinazoweza kufanya uvutiwe na mtu fulani, lakini hali yake ya kiroho ndiyo inayopaswa kuwa jambo muhimu.

Kwa hiyo Biblia inaonya mara nyingi dhidi ya kufunga ndoa na mtu asiye “katika Bwana.” (1 Wakorintho 7:39; Kumbukumbu la Torati 7:3, 4; Nehemia 13:25) Ni kweli kwamba watu ambao si waamini wanaweza kutumainika, kuheshimika, na kuonyesha fadhili. Hata hivyo, hawana kichocheo ulicho nacho cha kuboresha sifa hizo na cha kudumisha ndoa kadiri miaka inavyosonga.

Kwa upande mwingine, mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova na aliye mshikamanifu kwake hujitahidi kusitawisha sifa za Kikristo na kuzidumisha, hata iweje. Anatambua kwamba Biblia inahusianisha kumpenda mwenzi wako na kuwa na uhusiano mzuri na Yehova. (Waefeso 5:28, 33; 1 Petro 3:7) Kwa hiyo, wote wanapompenda Yehova, wanakuwa na kichocheo chenye nguvu zaidi cha kudumu wakiwa waaminifu kwa wenzi wao.

Je, hilo linamaanisha kwamba ni lazima ndoa ya watu wanaomwabudu Yehova ifanikiwe? La. Kwa mfano, itakuwaje ukimwoa mtu ambaye hapendezwi sana na mambo ya kiroho? Kwa kuwa hajui jinsi ya kupinga uvutano uliopo katika mfumo huu, ni rahisi mtu aliye dhaifu kiroho kupeperuka kutoka katika kutaniko la Kikristo. (Wafilipi 3:18; 1 Yohana 2:19) Hebu wazia jinsi ungeumia na matatizo ambayo mngekabili katika ndoa yenu ikiwa mwenzi wako angejihusisha na “mambo ya unajisi ya ulimwengu.”—2 Petro 2:20.

Kabla ya kuanzisha uhusiano unaoweza kuongoza kwenye ndoa, fikiria: Je, mtu huyu anaonekana kuwa mtu wa kiroho? Je, yeye huweka mfano mzuri kwa kuishi kama Mkristo? Je, yeye ni imara katika kweli ya Biblia, au anahitaji wakati zaidi wa kukua kiroho? Je, unasadiki kwamba upendo kwa Yehova ndio hasa unaoongoza maisha yake? Ni jambo la maana kujua ikiwa mtu huyo ni mfano mzuri. Hata hivyo, mwishowe, lazima uwe na hakika kwamba yule unayependezwa naye amejitoa kabisa kwa Yehova naye atakuwa mwenzi mzuri wa ndoa.

Pia, kumbuka kwamba wengine ambao hupendezwa na “watu wasiofaa” huvutiwa kwanza na mambo yasiyofaa, kama vile aina fulani ya vitumbuizo au utendaji usiofaa. Vijana wenye mfano mzuri katika kutaniko la Kikristo hawawezi kushirikiana nawe katika mambo kama hayo. Kwa hiyo, chunguza moyo wako.

Ukiona kuwa moyo wako unahitaji kutiwa nidhamu, usikate tamaa. Moyo unaweza kutiwa nidhamu. (Methali 23:12) Jambo muhimu zaidi ni hili: Wewe unataka nini hasa? Je, unataka kuvutiwa na mema na wale ambao huyatenda? Kwa msaada wa Yehova unaweza kusitawisha moyo kama huo. (Zaburi 97:10) Na kwa kuzoeza nguvu zako za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa, itakuwa rahisi kwako kuamua ni nani wanaoweza kuwa marafiki wazuri na wenye kujenga.—Waebrania 5:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Marafiki wazuri huwa na uvutano mzuri wa kiroho