Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulipata Kitu Bora Zaidi

Tulipata Kitu Bora Zaidi

Tulipata Kitu Bora Zaidi

SIMULIZI LA FRANCIS DEL ROSARIO DE PÁEZ

Mnamo 1988, mimi, ndugu zangu pamoja na wanamuziki wengine tulitumbuiza maelfu ya watazamaji huko Madison Square Garden, New York City. Nilicheza dansi katika bendi yetu ambayo ilikaribishwa kwa vifijo. Tulipokuwa wadogo, Baba alitusaidia kupata mafanikio.

BABA, ambaye pia alikuwa mwanamuziki, aliona kwamba kaka zangu saba walikuwa na kipawa cha muziki. Kwa hiyo aliuza nyumba yetu na kununua ala za muziki na vifaa muhimu ili kuwasaidia waanzishe bendi. Wakati huo nilikuwa mtoto tu, kwani nilizaliwa miaka michache mapema mwaka wa 1966. Familia yetu ilikuwa ikiishi katika mji wa Higüey katika Jamhuri ya Dominika.

Ndugu zangu walifanya tamasha yao ya kwanza ya muziki mnamo 1978 kwenye ukumbi wa mji wa Higüey. Baadaye walihama na kuanza kufanya tamasha zao kwenye mji mkuu, Santo Domingo. Walianza kuimba na kucheza mtindo wa merengue, na hivyo wakawa maarufu sana. * Bendi hiyo iliitwa Los Hermanos Rosario (Ndugu za Rosario).

Kwa kuwa kwa muda mrefu nilitamani sana kuwa mchezaji dansi maarufu, nilitaka kujiunga na ndugu zangu. Kwenye sherehe fulani ndugu yangu Pepe, aliyekuwa kiongozi wa bendi hiyo, alinialika nicheze dansi, huku akisema: “Francis ndiye dada yangu mdogo zaidi, naye anajua kucheza dansi.” Wote waliokuwako walifurahishwa na dansi yangu. Nilipotambua jambo hilo, nilimwambia Pepe kwamba ningetaka kucheza dansi mbele ya bendi hiyo. Hivyo, nikiwa na umri wa miaka 16 nilianza kucheza dansi kwenye tamasha zote za Los Hermanos Rosario.

Mafanikio ya Kazi

Kabla ya hapo, kulikuwa na waimbaji wa kike katika bendi za merengue lakini hakukuwa na mwanamke aliyecheza dansi mbele ya kikundi cha wanaume. Nilipanga miondoko yangu nikitumia mbinu mpya ya kucheza dansi ili kufuatana na midundo ya merengue. Baada ya mtindo wangu wa kucheza dansi kujulikana na wengi, uliitwa a lo Francis Rosario.

Tuliimba wimbo fulani wa merengue ulioitwa “Cumandé,” ambao baadhi ya maneno yake yalisema: “Y ahora todo el mundo como Francis Rosario” (Sasa kila mtu acheze kama Francis Rosario). Kisha watu wangeiga mtindo wangu wa kucheza dansi. Nyakati nyingine waliketi sakafuni ili kunitazama badala ya kucheza dansi. Hatimaye, picha yangu ndiyo iliyotumiwa kutangaza maonyesho ya bendi yetu. Kila aliyeona tangazo hilo alijua kwamba kutakuwa na tamasha ya Los Hermanos Rosario.

Baada ya kuanza kufanya tamasha na ndugu zangu, wanamuziki wengine waliongezwa kwenye bendi hiyo, kutia ndani ndugu watatu ambao jina lao la mwisho ni Páez. Mmoja wao, aliyeitwa Roberto na ambaye alicheza tarumbeta, akawa mume wangu. Ndugu hao walianza kuchangia kufanikiwa kwa bendi yetu. Bendi ya Los Hermanos Rosario ilianza kupokea mialiko mingi ya kufanya tamasha kwenye televisheni huko Santo Domingo, na vilevile katika nchi nyingine.

Mnamo 1988, tulisafiri hadi Marekani na Kanada. Mojawapo ya tamasha tulizofanya ni ile ya Madison Square Garden ambayo imetajwa mapema. Vikundi vingi maarufu vya merengue vilifanya tamasha huko, lakini bendi yetu ndiyo iliyopokelewa vizuri zaidi. Baada ya tamasha hiyo, sikuzote wadhamini walipanga bendi yetu iwe ya mwisho kucheza. Kuliko wakati mwingine wowote, watu walikuwa wakivutiwa na mtindo wangu wa kucheza dansi, na mashabiki wa Los Hermanos Rosario wakaanza kuongezeka. Pia mauzo ya nyimbo zetu zilizorekodiwa yalianza kuongezeka.

Tulisafiri nchi nyingi kama vile Kolombia, Ekuado, Panama, Puerto Riko, Kurasao, Hispania, Ujerumani, na nchi nyingine. Baada ya muda mfupi tukawa wanamuziki mashuhuri zaidi Amerika Kusini. Mambo muhimu zaidi maishani mwangu yakawa kucheza dansi, jukwaa, mavazi, na vipodozi.

Nilipokuwa mseja, nilikuwa nikisema kwamba ikiwa mwanamume angevutiwa nami lakini awe hapendi kucheza dansi, ningemwacha kabla ya kuacha kucheza dansi. Hata hivyo, mtazamo wangu kuelekea mambo niliyopaswa kutanguliza maishani ulikuwa karibu kubadilika.

Kutambua Umuhimu wa Mambo ya Kiroho

Badiliko hilo lilianza tulipokuwa tumezuru Visiwa vya Canary mwaka wa 1991. Mimi na Roberto tulikuwa tumeoana muda mfupi kabla ya hapo. Ndugu yake Freddy, ambaye pia alishirikiana na bendi hiyo, alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na sikuzote alikuwa na vichapo vyao.

Siku moja niliona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika chumba cha Freddy na nikaanza kukisoma. Nilivutiwa na sura yenye kichwa, “Je, Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?” Nilivutiwa na sura hiyo kwa sababu Mama alikuwa amesema kwamba mtu aliyefanya mambo mabaya atachomwa kwenye moto wa mateso. Kwa hiyo niliogopa kwenda motoni.

Majuma machache baadaye, tulipokuwa bado kwenye Visiwa vya Canary, mimba yangu iliharibika. Waliponipeleka hospitalini, nilimwambia Roberto amwombe Freddy kitabu nilichoona chumbani mwake. Nilitaka kukisoma nikiendelea kupata nafuu. Nilikipenda kitabu hicho. Kati ya mambo niliyojifunza ni kwamba Biblia haifundishi kuwa kuna mahali penye moto wa mateso na kwamba Mungu hajakusudia kamwe kumtesa mtu yeyote. (Yeremia 7:31) Nilifurahi kujua kwamba Biblia inafundisha kuwa wafu hawajui jambo lolote.—Mhubiri 9:5, 10.

Tuliporudi katika Jamhuri ya Dominika, Freddy alimtuma mmoja wa Mashahidi wa Yehova atutembelee. Alitueleza tumaini la Biblia la kuishi milele katika paradiso duniani, na jambo hilo lilichochea upendezi wa mume wangu. (Zaburi 37:29; Luka 23:43) Tuliamua kujifunza Biblia.

Nabadili Maadili na Mambo ya Kutangulizwa

Nilipoendelea kujifunza Biblia, nilianza kubadili maoni yangu kuhusu kazi niliyoipenda sana. Kanuni za Biblia zilianza kubadili fikira zangu. (Waroma 12:2) Nilikuwa nikijiuliza: ‘Je, kweli ninapaswa kucheza dansi hii mbele ya watu hawa wote? Sifurahii jambo hilo.’ Nilisali hivi kwa Mungu, “Tafadhali nitoe katika hali hii.” Nilimweleza mume wangu jinsi nilivyohisi, naye alihisi kama mimi. Aliniambia: “Uwe mwenye subira mpenzi. Acha kushirikiana na bendi hii, nami nitaacha baadaye.”

Nilipata mimba tena, na kwa kuwa singeweza kucheza dansi sana, nilipata wakati wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme mara nyingi zaidi. Mikutano hiyo iliniimarisha sana mimi na Roberto, ambaye alihudhuria pia, na ikafanya tutambue umuhimu wa kukutanika pamoja na watu wa Yehova. Tulifahamu kwamba ili tufanye maendeleo katika kweli ya Biblia, tulihitaji mafundisho na kitia moyo kinachopatikana kwenye mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Hata tulipofanya kazi nje ya Jamhuri ya Dominika, mimi na Roberto tulitafuta Jumba la Ufalme na kuhudhuria mikutano.

Baada ya kujifungua, nilirudi kazini, lakini sikufurahia kazi hiyo. Badiliko hilo lilionekana waziwazi, na nikaanza kushutumiwa na waandishi wa habari. Mara nyingi niliulizwa hivi, “Mbona huchezi dansi kama zamani?” Niliendelea kusali kwa Yehova anitoe katika hali hiyo ili nisiwe na matatizo yoyote na ndugu zangu. Nilikuwa mmoja wa wamiliki wa bendi hiyo, na sikutaka kuzozana na ndugu zangu.

Nilipopata mimba tena, nilimwambia Rafa, aliyekuwa akisimamia bendi hiyo baada ya ndugu yangu Pepe kufa, kwamba ningependa kutumia wakati zaidi pamoja na watoto wangu na hivyo singerudi kazini. Aliniambia nifanye lile nililoona kuwa linafaa. Hakuna ndugu yangu hata mmoja aliyenipinga nisijifunze Biblia. Ninawashukuru sana kwa kutonipinga.

Maisha Mapya ya Kumtumikia Yehova

Mnamo 1993, baada ya kushirikiana na bendi hiyo kwa miaka kumi, niliacha kazi yangu na kujiweka wakfu kwa Yehova bila masharti. Nikawa mtangazaji wa habari njema ya Ufalme wa Mungu na baada ya Roberto kuacha kushirikiana na bendi hiyo, tulibatizwa mwaka wa 1994. (Mathayo 24:14) Freddy pamoja na ndugu mwingine wa Roberto, anayeitwa Julio, wakawa Mashahidi, na pia Manuel Pérez, mshiriki mwingine wa bendi hiyo. Wangali wanamtumikia Yehova kwa uaminifu hadi leo hii.

Watu wengi hawakuelewa kile kilichofanya niache kazi yangu kwani niliipenda sana. Wengine walihisi kama mtangazaji fulani mashuhuri wa televisheni nchini mwetu, kwamba hali hiyo ilikuwa ya muda tu. Alitabiri hivi: “Kama wanamuziki wote, hali hiyo itapita naye atajiunga tena na bendi hiyo.” Lakini sikufanya hivyo kamwe. Nilikuwa nimeazimia kujitoa kikamili kumtumikia Yehova.

Sasa tuna watoto watatu: Katty, Roberto, na Obed. Tunajaribu kuwafundisha kwamba mambo ya kiroho ndiyo ya maana zaidi maishani kuliko ya kimwili. Kwa sababu ya mambo tuliyojionea maishani, tunaweza kuwaonya kuhusu uvutano wenye kupotosha wa ulimwengu na kuwapa mwongozo unaofaa maishani. Tumenufaishwa sana na funzo letu la familia la Biblia tunalofanya kila juma, nalo hutusaidia tuwe na umoja katika ulimwengu ambao familia zinazidi kugawanyika.

Tumejaribu kuwafundisha watoto wetu wamwone Yehova kuwa mtu halisi ambaye wanaweza kumtumaini. (Methali 3:5, 6; Waebrania 11:27) Pia tumewaonyesha umuhimu wa kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya Kikristo. Kuona watoto wetu wakiishi kupatana na kweli ya Biblia ni zawadi isiyo na kifani. Kwa miaka miwili, nimekuwa nikitumikia nikiwa painia-msaidizi, neno ambalo Mashahidi wa Yehova hutumia kuhusu wale wanaotumia muda wa saa 50 au zaidi kila mwezi wakiwaeleza wengine imani yao inayotegemea Biblia. Na kwa miaka kadhaa sasa, mume wangu amekuwa mzee wa kutaniko la Kikristo.

Bado mimi huona merengue kuwa dansi nzuri. Lakini inasikitisha kwamba mitindo mingi ya merengue inayopendwa sasa ni tofauti sana na ile ya zamani. Kwa ujumla, mitindo ya zamani ilikuwa mizuri. Siku hizi ili kupata muziki mzuri wa merengue, tunapaswa kuwa wateuzi sana.

Manufaa ya Kumtumikia Yehova

Ulimwengu una mambo mengi, lakini lazima mtu afikirie hali zinazozunguka mambo hayo. Ndivyo ilivyo na muziki, ambao kijuujuu tu unaweza kuonekana kuwa wenye kuvutia sana na usiodhuru. Lakini sivyo ulivyo. Wengi ambao hujihusisha na muziki hutumia dawa za kulevya na hawafuati maadili. Kushiriki kwenye tamasha humfanya mtu ashirikiane na watu ambao dhamiri zao hazifanyi kazi hata kidogo na ambao hufurahia tu raha za sasa bila kujali matokeo.—1 Wakorintho 15:33.

Tumetambua kwamba jambo bora zaidi unaloweza kufanya ni kumtumikia Yehova. Ninakumbuka nikirudi kwenye hoteli baada ya mojawapo ya tamasha zetu kubwa zaidi na kuhisi kuwa maisha hayana kusudi. Sasa ninatambua kwamba ni kwa sababu hatukuwa tukitosheleza uhitaji wetu muhimu zaidi, yaani, uhitaji wetu wa kiroho.—Mathayo 5:3.

Sasa tunakazia fikira kumpendeza Muumba wetu hasa kwa kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wake. (Mathayo 24:14; Matendo 20:35) Familia yetu hupata furaha na uradhi kwa kufanya hivyo. Tunashukuru sana kuwa miongoni mwa watu wa Mungu na kuwa na marafiki wa kweli, yaani, ndugu na dada katika imani, ambao wana tumaini zuri kama sisi la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.—Marko 10:29, 30; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Tulipata pesa nyingi tulipokuwa tukiwatumbuiza watu. Lakini kwa kumjua Mungu wetu, Yehova, tumepata utajiri wa kiroho ambao ni wenye thamani zaidi kuliko mali zozote za kimwili. Tunafurahi sana kwamba tunaweza kumtumikia Mungu mwenye kusudi na mwenye furaha anayetutia moyo tumtumaini! (Zaburi 37:3) Tunasadiki kabisa kwamba tumepata kitu fulani kizuri zaidi kuliko umashuhuri na mali za kimwili, nasi tunasali kwa Yehova atusaidie tukiwa familia kufanya mapenzi yake milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Merengue ni aina fulani ya muziki wa dansi. Zamani, kikundi kidogo cha wanamuziki kilicheza merengue kwa kutumia kodiani, guiro (kikwanguzi cha chuma), na tambora (ngoma mbili ndogo zilizounganishwa). Baada ya muda, bendi kubwa zaidi (ambazo pia ziliitwa okestra katika Jamhuri ya Dominika) zilianzishwa. Kwa sasa, vikundi vingi vya merengue hutumia piano, saksafoni, tarumbeta, na ngoma za conga, na pia ala nyingine.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa pamoja na washiriki wengine wa bendi nilipoanza kazi yangu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kwenye tamasha huko New York City, yapata mwaka wa 1990

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tukiwa mbele ya Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 23]

Picha ndogo: Tukifanya funzo la Biblia la familia