Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Laiti Ningalifanya Hivyo Mapema Zaidi’

‘Laiti Ningalifanya Hivyo Mapema Zaidi’

‘Laiti Ningalifanya Hivyo Mapema Zaidi’

Kuna sababu nzuri za kuita zoea hili uraibu. Uchunguzi uliofanywa nchini Marekani ulionyesha kwamba wavulana wa darasa la nane (wenye umri wa miaka 13 hivi) walikuwa wakitumia wastani wa saa 23 hivi kwa juma kucheza michezo ya video. Pia watu wengi wazima ni waraibu wa michezo hiyo. Fikiria Mkristo anayeitwa Charles. * Anasema, “Mimi niliona michezo ya video kuwa njia ya kuepuka matatizo na madaraka na kujistarehesha. Lakini nilikuwa mraibu. Nilikuwa mraibu wa michezo ya video kama vile watu wanavyokuwa waraibu wa dawa za kulevya au kileo.”

Charles anasema kwamba alianza kucheza “kwa ukawaida” alipokuwa na umri wa miaka 11 hivi. Anasema, “Sikuwa nikicheza michezo inayohusisha roho waovu au yenye jeuri, lakini niliicheza kwa muda mrefu kupita kiasi. Kuna nyakati ambapo ningetumia majuma kadhaa kufikiria tu jinsi nitakavyotatua tatizo fulani la mchezo iwe nilikuwa shuleni au katika utendaji fulani wa Kikristo.”

Charles aliguswa moyo na kichwa cha makala ya gazeti Amkeni! la Desemba 22, 2002, “Je, Michezo ya Kompyuta Ina Ubaya Wowote?” Anasema: “Baada ya kusoma gazeti hilo, nilijaribu kupunguza muda niliotumia kucheza. Hata hivyo, baada ya muda, nilianza tena kutumia wakati mwingi kucheza.”

Wakati wa uchumba na muda mfupi baada ya ndoa, Charles alifaulu kupunguza muda aliotumia kucheza. “Lakini,” anasema, “mchezo mpya ulitokea ambao nilikuwa nimeutarajia kwa muda mrefu. Nilikopa pesa za kununua kompyuta ambayo ingeweza kucheza mchezo huo. Mchezo huo ndio uliochukua muda wangu mwingi zaidi. Ulininyima wakati wa kumtumikia Yehova. Pia nilikuwa nikimpuuza mke wangu.” Punde si punde, Charles alitambua kwamba alipaswa kuchukua hatua madhubuti. Anasema: “Niliamua kuharibu michezo yangu yote ya video. Niliifuta kwenye kompyuta yangu na kuitupa yote kwenye pipa.”

Je, Charles anajuta kuhusu uamuzi wake? La hasha. Anasema, “Siwezi kueleza jinsi nilivyojihisi mtulivu baada ya kufanya hivyo. Ninahisi kwamba mzigo mzito umeondolewa mabegani mwangu. Ninahisi kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, na nimekuwa nikisali kwake kwa ukawaida. Pia ninamjali mke wangu zaidi. Ninashukuru sana kwa kushinda uraibu wangu. Ninajuta kwamba sikufanya hivyo mapema zaidi.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Jina limebadilishwa.