Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanaotoa Ushahidi Wenye Nguvu

Vijana Wanaotoa Ushahidi Wenye Nguvu

Vijana Wanaotoa Ushahidi Wenye Nguvu

Vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova huzungumza kwa ujasiri kuhusu imani yao wakiwa shuleni na katika huduma ya Kikristo, na wamepata mafanikio mengi kwa kufanya hivyo. Fikiria mifano ifuatayo. *

Kristina anasema: “Nilipokuwa katika darasa la tatu, mwalimu alimpa kila mmoja wetu kitabu cha kuandika utendaji wetu wa kila siku. Mwalimu alisema kwamba angesoma vitabu vyetu kisha atuandikie maelezo fulani. Niliamua kuandika katika kitabu changu hotuba ambayo ningetoa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mwalimu alionekana kuwa amevutiwa na jambo hilo, kwa hiyo nilimwalika aje kwenye Jumba la Ufalme ili kusikiliza hotuba yangu. Mwalimu huyo alikuja pamoja na mwalimu aliyenifunza nikiwa darasa la kwanza. Baadaye shuleni, mwalimu alieleza darasa lote jinsi alivyofurahia hotuba yangu. Nilifurahi sana. Lakini mambo hayakuishia hapo. Mwaka mmoja hivi baadaye, nilisimulia jambo hilo kwenye kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova, na mwalimu wangu alihudhuria kusanyiko hilo pia. Baadaye, mimi na rafiki yangu ambaye ni painia tulimtembelea mwalimu aliyenifundisha nilipokuwa katika darasa la tatu na kumwachia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Hata amewahi kuhudhuria kusanyiko letu la wilaya!”

Sydnee, alipokuwa na umri wa miaka sita, alikuwa stadi katika kuzungumza kwa ujasiri na wanafunzi wenzake kuhusu kweli za Neno la Mungu, kutia ndani hali ya wafu na cheo cha Yesu anapolinganishwa na Mungu. Mama yake anasema: “Yeye amekuwa mhudumu mdogo mwenye bidii na asiyeogopa.” Alipokuwa akimaliza mwaka wake wa kwanza shuleni, Sydnee alikuwa na huzuni. Alisema, “Nina wasiwasi kuhusu wanafunzi wenzangu. Watajifunzaje juu ya Yehova?” Sydnee alikuwa akifikiria jambo fulani. Siku ya mwisho shuleni, alimpa kila mwanafunzi zawadi iliyokuwa imefungwa. Zawadi hiyo ilikuwa kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Sydnee aligawanya vitabu 26, huku akiwaambia wanafunzi kwamba wanaweza kufungua zawadi zao nyumbani wakiwa pamoja na wazazi wao. Sydnee huona wanafunzi wenzake kuwa eneo lake la kuhubiri. Hata aliwapigia simu ili kujua maoni yao kuhusu kitabu hicho. Msichana mmoja alisema kwamba yeye husoma kitabu chake kila jioni pamoja na mama yake.

Alipokuwa na umri wa miaka 15, Ellen alimpa mwalimu wake wa historia nakala kadhaa za Amkeni! Ellen anasema: “Alipendezwa nazo, na amekuwa akisoma Amkeni! kwa miaka miwili sasa.” Ellen anaendelea kusema: “Hivi karibuni nilimpa Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, naye akaniambia kwamba binti zake wawili wanakifurahia sana. Kwa hiyo nilimpa kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Baadaye, alinipa kadi. Ilisema hivi: ‘Asante sana kwa vitabu hivyo. Mimi na binti zangu tunavisoma kwa bidii. Inapendeza sana kuona kijana aliyejitoa na aliye thabiti kama wewe. Umepewa zawadi bora zaidi, imani ya kipekee. Umenifundisha mengi zaidi ya yale ambayo ningekufundisha!’ Jambo hilo lilinionyesha kadiri ambavyo watu huthamini kweli ya Biblia tunapojitahidi kuwahubiria.”

Daniel alikuwa na umri wa miaka sita alipopata funzo lake la kwanza la Biblia. Anasema: “Nilikuwa nikienda kwenye mafunzo pamoja na mama, lakini nilitaka kupata mtu nitakayemfundisha mwenyewe.” Daniel alichagua Bi. Ratcliff, mwanamke mzee aliyekuwa amemwachia vichapo vya Biblia. “Ningependa kukuonyesha kitabu ninachokipenda zaidi, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia,” akamwambia, huku akiongeza hivi: “Ningependa kujua kama ninaweza kuja kila juma na kukusomea kitabu hicho.” Bi. Ratcliff alikubali pendekezo la Daniel. “Tulianza kujifunza na Bi. Ratcliff baadaye siku hiyo,” asema Laura, mama ya Daniel. “Daniel na Bi. Ratcliff walisoma mafungu kwa zamu, kisha Daniel akamwambia asome baadhi ya maandiko yaliyoonyeshwa mwishoni mwa hadithi. Niliambatana na Daniel, lakini Bi. Ratcliff alipendelea kuzungumzia mambo hayo na Daniel tu!” Baada ya muda, Daniel na Bi. Ratcliff walianza kujifunza kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Wakati huo, dada mdogo wa Daniel, Natalie alikuwa mkubwa vya kutosha kusoma, kwa hiyo alijiunga nao. Bi. Ratcliff alikuwa na maswali mengi na mengine yalikuwa magumu sana. Lakini Daniel na Natalie walitumia kijitabu Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia na fahirisi iliyo upande wa nyuma wa Biblia kuwasaidia kupata majibu yanayotegemea Biblia. Bi. Ratcliff, ambaye amekuwa Mkatoliki maisha yake yote alisisimuliwa na mambo aliyokuwa akijifunza. Alisema hivi pindi moja baada ya funzo: “Laiti ningalianza kujifunza Biblia miaka mingi iliyopita!” Kwa kusikitisha, Bi. Ratcliff alikufa hivi karibuni akiwa na umri wa miaka 91. Lakini kwa sababu ya kujifunza Biblia aliweza kufahamu kweli nzuri, kutia ndani tumaini la Biblia la watu kufufuliwa katika dunia paradiso. Sasa Daniel ana umri wa miaka kumi na anaongoza mafunzo mawili ya Biblia. Natalie, ambaye sasa ana umri wa miaka minane, anajifunza Biblia na msichana mdogo wa rika lake.

Vijana kama Kristina, Sydnee, Ellen, Daniel na Natalie huwafurahisha wazazi wao Wakristo. Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba wanaufurahisha moyo wa Yehova, naye hatasahau upendo ambao vijana hao wanaonyesha kwa ajili ya jina lake.—Methali 27:11; Waebrania 6:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Vichapo vyote vilivyotajwa katika makala hii vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kristina (juu), na Sydnee

[Picha katika ukurasa wa 19]

Daniel na Natalie

[Picha katika ukurasa wa 19]

Ellen