Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatimaye Kila Mtu Atakuwa na Nyumba Nzuri!

Hatimaye Kila Mtu Atakuwa na Nyumba Nzuri!

Hatimaye Kila Mtu Atakuwa na Nyumba Nzuri!

NJE tu ya jiji la Nairobi, Kenya, kuna makao maridadi ya Umoja wa Mataifa ya Gigiri, yenye ukubwa wa ekari 140, yanayotia ndani makao makuu ya mradi wa Umoja wa Mataifa unaoshughulikia makao (UN-HABITAT). Shirika hilo lilibuniwa ili kuonyesha azimio la kimataifa la kutatua tatizo la nyumba ulimwenguni. Katika uwanja wa makao hayo huko Gigiri, kuna sehemu yenye kupendeza iliyotengwa ili kutazama mazingira, ambayo ni mfano bora wa kile kinachoweza kutimizwa kunapokuwa na jitihada madhubuti na pesa za kutosha. Eneo ambalo wakati mmoja lilijaa takataka, sasa limegeuzwa kuwa mahali maridadi pa tafrija panapoweza kutumiwa na wafanyakazi na wageni.

Hata hivyo, kilometa chache tu kutoka hapo kuna mtaa mpya wa mabanda ambao unapanuka haraka. Mtaa huo ni kikumbusha chenye kusikitisha kuhusu jinsi ilivyo vigumu kusuluhisha tatizo la nyumba. Nyumba hizo zilizojengwa kwa udongo, vijiti, na mikebe, zina ukubwa wa meta 16 hivi za mraba. Vijia vyake vimejaa maji machafu yenye uvundo. Bei ya maji ni mara tano zaidi ya ile ambayo mkaaji wa Marekani hulipa kwa ajili ya maji. Wengi kati ya wakazi 40,000 hivi wanaoishi hapo wana umri wa kati ya miaka 20 na 30 na kitu. Si wavivu au wazembe. Walienda katika eneo hilo ili watafute kazi katika jiji la Nairobi lililo karibu.

Tofauti na eneo hilo, viongozi wa ulimwengu hukutana katika mazingira safi, mazuri, na yenye kuvutia ili kuzungumzia wakati ujao wa wanaume, wanawake, na watoto wanaoishi katika eneo lililo katika ujirani wao. Kulingana na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, jambo la kusikitisha ni kwamba “ulimwengu una mali, ujuzi, na uwezo” wa kuboresha sana maisha ya wakazi wa mitaa ya mabanda. Basi ni jambo gani linalohitaji kufanywa? Bw. Annan anasema: “Ni tumaini langu kwamba . . . wote wanaohusika [wataweza] kushinda hali ya kutojali na kutojishughulisha ambayo imezuia maendeleo.”

Hata hivyo, tumaini hilo ni halisi kadiri gani? Ni nini kitakachohitajiwa ili wanasiasa wote, wa kimataifa na wenyeji, waache kufikiria tu masilahi yao yenyewe na kushirikiana ili kupata suluhisho la tatizo hilo? Kuna Mtu fulani aliye na mali, ujuzi, na uwezo wa kukomesha tatizo lililopo. Jambo muhimu zaidi ni kwamba yeye pia ana huruma na nia ya kuchukua hatua hivi karibuni. Kwa kweli, tayari serikali yake imefanya mipango madhubuti ya kumaliza kabisa tatizo la nyumba ulimwenguni.

Mradi Mpya wa Kujenga Nyumba

Katika Biblia, Muumba wetu, Yehova Mungu, anataja yale anayokusudia kufanya. Anaahidi hivi: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya.” (Isaya 65:17) Jambo hilo litaleta badiliko kubwa. “Mbingu” hizo mpya za kiserikali zitatimiza mambo ambayo serikali za kisasa za wanadamu zimeshindwa kutimiza. Ufalme, au serikali ya Mungu, itahakikisha kwamba kila mtu atakayekuwa sehemu ya jamii mpya ya kibinadamu duniani atakuwa na afya nzuri, usalama, na atajiheshimu. Mapema, Isaya aliambiwa kwamba watu watakaokuwa sehemu ya jamii mpya ya kidunia wangekusanywa katika “siku za mwisho.” (Isaya 2:1-4) Hilo linamaanisha kwamba mabadiliko hayo yatatukia hivi karibuni.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.

Jambo muhimu ni kwamba katika maneno yaliyoandikwa katika mistari mingine ya Isaya sura ya 65, Mungu anataja kihususa kwamba wakati huo atamwandalia kila mtu makao ya kudumu. Anasema: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake. . . . Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake.” (Isaya 65:21, 22) Wazia ukiishi katika nyumba yako na katika mazingira safi yenye usalama katika paradiso nzuri! Ni nani asiyetamani hali kama hizo? Lakini unawezaje kuwa na hakika kuhusu kile ambacho Mungu ameahidi?

Ahadi Unayoweza Kutumaini

Mungu alipowaumba Adamu na Hawa, hakuwaweka katika mazingira makame. Badala yake, aliwaweka katika bustani maridadi huko Edeni iliyokuwa na hewa safi, maji na chakula tele. (Mwanzo 2:8-15) Adamu aliambiwa ‘ajaze dunia,’ lakini si kupita kiasi. (Mwanzo 1:28) Tangu mwanzo, Mungu alikusudia kila mtu afurahie utaratibu, upatano, na mambo mengi mazuri.

Baadaye, katika siku za Noa, jamii ya kibinadamu ilikuwa na jeuri na ukosefu mwingi sana wa adili, hivi kwamba “dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:11, 12) Je, Mungu alifumbia macho tu hali hiyo? La. Alichukua hatua mara moja. Alisafisha dunia kwa kuleta Gharika ulimwenguni pote kwa ajili ya jina lake na kwa ajili ya Noa mwadilifu na wazao wake. Kwa hiyo Noa na familia yake walipotoka kwenye safina na kuingia katika makao yao mapya, waliambiwa kwa mara nyingine wasambae, ‘wawe wengi, na kuijaza dunia.’—Mwanzo 9:1.

Hata baadaye, Mungu aliwapa Waisraeli urithi aliokuwa amemwahidi babu yao Abrahamu. Nchi hiyo ya Ahadi ilitajwa kuwa “nchi nzuri na kubwa . . . inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:8) Kwa sababu ya kutotii, Waisraeli walirandaranda nyikani bila makao ya kudumu kwa miaka 40. Hata hivyo, ili kutimiza ahadi yake, mwishowe Mungu aliwapa nchi ambayo wangeishi. Simulizi lililopuliziwa linasema hivi: “Yehova akawapa pumziko kuwazunguka pande zote . . . Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa ameipa nyumba ya Israeli; mambo yote yalitimia.”—Yoshua 21:43-45.

Hatimaye Kila Mtu Atakuwa na Nyumba!

Kwa hiyo, ni wazi kwamba maneno ya Yehova katika Isaya sura ya 65 si ahadi za bure. Kwa kuwa yeye ndiye Muumba wa vitu vyote, bila shaka ana uwezo wa kufanya lolote linalohitajika ili kuisafisha dunia na kutimiza kusudi lake la awali kuielekea. (Isaya 40:26, 28; 55:10, 11) Isitoshe, Biblia inatuhakikishia kwamba anataka kufanya hivyo. (Zaburi 72:12, 13) Alichukua hatua hapo zamani ili kuwaandalia wanadamu waadilifu nyumba zinazofaa, naye atafanya hivyo tena hivi karibuni.

Kwa kweli, Mwana wake, Yesu Kristo, alipokuja duniani aliwafundisha wafuasi wake wasali hasa kwamba ‘mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’ (Mathayo 6:10) Alionyesha kwamba dunia itakuwa paradiso. (Luka 23:43) Hebu wazia hilo litamaanisha nini. Hakutakuwa tena na mitaa ya mabanda, maeneo ya maskwota, watu wanaolala barabarani, au watu kufukuzwa mahali wanapoishi. Huo utakuwa wakati wenye furaha iliyoje! Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, mwishowe kila mtu atapata makao ya kudumu!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Nyumba za Waisraeli wa Kale

Ni wazi kwamba, kama tu Wakanaani waliowatangulia, Waisraeli walipendelea nyumba za mawe kwani zilikuwa imara zaidi kuliko nyumba nyingine nazo ziliwalinda dhidi ya wavamizi. (Isaya 9:10; Amosi 5:11) Hata hivyo, katika maeneo tambarare, matofali yaliyokaushwa kwa jua au yaliyochomwa yalitumiwa kujenga kuta za nyumba. Paa nyingi zilikuwa tambarare na nyakati nyingine chumba kingine kilijengwa juu yake. Mara nyingi kulikuwa na kiokeo katika ua na nyakati nyingine pia kulikuwa na kisima au tangi la maji.—2 Samweli 17:18.

Sheria ya Musa ilitia ndani sheria fulani kuhusu ujenzi. Bila shaka, usalama ulikuwa jambo muhimu zaidi. Ukuta mfupi ulipaswa kujengwa kuzunguka paa tambarare ili kuzuia misiba. Amri ya kumi iliwaonya Waisraeli dhidi ya kutamani nyumba ya mwenzao. Mtu aliyelazimika kuuza nyumba yake alikuwa na haki ya kuikomboa tena, angalau kwa muda fulani.—Kutoka 20:17; Mambo ya Walawi 25:29-33; Kumbukumbu la Torati 22:8.

Nyumba katika Israeli ilikuwa pia mahali muhimu pa kutoa maagizo ya kiroho. Akina baba waliagizwa kihususa kwamba walipaswa kuwafundisha wana wao matakwa ya Mungu walipokuwa wameketi nyumbani, na makao yao hayakupaswa kuwa na kitu chochote kilichohusiana na ibada ya sanamu.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; 7:26.

[Picha]

Katika Israeli la kale, nyumba zilitumiwa kwa utendaji wa kiroho kama vile kuadhimisha Sherehe ya Vibanda

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Nyumba za Zamani Zaidi

Biblia haisemi kwamba mwanadamu wa kwanza, Adamu, aliishi ndani ya nyumba. Hata hivyo, andiko la Mwanzo 4:17 linasema kwamba Kaini ‘alijishughulisha na ujenzi wa jiji, akaliita hilo jiji kwa jina la mwana wake Enoko.’ Huenda ikawa jiji hilo lilikuwa tu kijiji chenye ngome kwa kulinganisha na viwango vya sasa. Simulizi hilo halitaji majengo yaliyojengwa wakati huo. Huenda jiji lote lilikuwa tu na washiriki wa karibu wa familia ya Kaini.

Mahema yalitumiwa sana kama nyumba katika nyakati za mapema. Mzao mwingine wa Kaini, Yabali, anasemwa kuwa “mwanzilishi wa wale wanaokaa katika mahema na walio na mifugo.” (Mwanzo 4:20) Ni wazi kwamba ingekuwa rahisi kupiga mahema na kuyang’oa wanapohama.

Kadiri wakati ulivyopita, jamii nyingi zilijenga majiji yaliyokuwa na nyumba za hali ya juu zaidi. Kwa mfano, katika jiji la Uru, ambako wakati mmoja mzee wa ukoo Abramu (Abrahamu) aliishi, magofu yanaonyesha kwamba wakazi fulani waliishi katika nyumba zilizopigwa plasta na kupakwa chokaa, zilizokuwa na vyumba 13 au 14. Huenda ikawa watu wengi sana wakati huo walitamani kuwa na nyumba kama hizo.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mungu anawaahidi waadilifu makao mazuri