Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Napaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

Napaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

Vijana Huuliza . . .

Napaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

“Ingawa mimi ni mwenye haya, ninaweza kufungua kituo cha Intaneti na kuzungumza na watu ambao kwa kawaida singezungumza nao. Hawanijui.”—Peter. *

“Mtu hujihisi huru kusema chochote anachotaka katika kituo cha maongezi.”—Abigail.

VITUO VYA MAONGEZI ni njia ya kutumia Intaneti kuwasiliana moja kwa moja na mtu kwa kuandikiana ujumbe. Vituo hivyo vinaweza kutumiwa na watu wengi ambao wanaweza kuandikiana na kujibu ujumbe.

Vijana ambao hutumia Intaneti huvutiwa hasa na vituo fulani vya maongezi. Mamilioni ya vijana kutoka tamaduni mbalimbali hutumia vituo hivyo kila siku kujadiliana kuhusu mambo ya kila aina. Sasa shule fulani zinatumia njia hiyo ya mawasiliano ulimwenguni. Kwa mfano, chini ya usimamizi wa walimu wao, huenda wanafunzi huko Marekani wakajadiliana kuhusu masuala ya kijamii na wanafunzi wenzao huko Hispania, Uingereza, au kwingineko. Wanafunzi wanaweza hata kujadiliana kuhusu kazi za shuleni pamoja na injinia, mwanakemia, au mtaalamu mwingine mwenye ustadi.

Hata hivyo, wengi hawatumii vituo hivyo ili kujadiliana tu kuhusu mambo ya shule. Ikiwa wewe hutumia Intaneti, ni hatari zipi unazopaswa kujua?

Mahali pa Kuvizia Watu Kingono

Abigail anasema hivi: “Nilikuwa nikizungumza na watu fulani kwenye kituo cha maongezi kisha mwanamume fulani akaniuliza kama ninajua vijana wowote wenye umri wa miaka 14. Alitaka kufanya ngono nao. Alisema kwamba alikuwa tayari kuwalipa ili wafanye ngono naye.”

Kuna visa vingi sana kama hivyo. Tatizo la watu kuvizia wengine kingono kwenye Intaneti limeenea sana hivi kwamba serikali fulani zimetoa miongozo ya jinsi ya kuwalinda vijana. Kwa mfano, kichapo fulani cha Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) huonya kuhusu watu ambao huanza kuzungumza waziwazi kuhusu ngono mara tu wanapoanza maongezi kwenye vituo hivyo. Kinaonya pia kuhusu watu ambao “huwashawishi watu hatua kwa hatua kwa kuwaonyesha upendo, fadhili, na hata kuwapa zawadi.”

Kikionyesha njia hususa ambazo baadhi ya watu hao hutumia, kichapo hicho cha FBI kinasema: “Wao husikiliza matatizo ya watoto na kuwahurumia. Wao hujua muziki wa hivi karibuni na mapendezi ya watoto. Hatua kwa hatua watu hao hujaribu kufanya watoto wasiwe na haya kwa kutaja maneno fulani kuhusu ngono na kuzungumzia mambo mengine kuhusu ngono.”

Hatari haitokani tu na watu wazima waliopotoka. Unapaswa pia kujihadhari na vijana ambao hawajui au hupuuza viwango vya maadili vya Biblia. Fikiria kisa cha mwanamume kijana anayeitwa Cody. Alikuwa akizungumza na vijana wengine kwenye Intaneti wakati msichana mmoja alipomwalika kwenye kituo cha maongezi cha faragha. Kisha akamuuliza swali la kumshawishi kingono. Cody alijizuia na kukatiza mazungumzo hayo mara moja.

Kwa sababu ni jambo la kawaida kupendezwa na ngono, huenda ikawa vigumu sana kwako kutenda kama alivyofanya Cody. Peter, aliyetajwa awali anakiri hivi: “Nilidhani kwamba ningeweza kujizuia na kukatiza mazungumzo ikiwa yangebadilika na kuwa mazungumzo kuhusu ngono. Lakini mara nyingi sikuyakatiza na nilijikuta nikizungumza kuhusu mambo ya ngono. Nilihisi vibaya baadaye.” Hata hivyo, huenda ukauliza, ‘Kuna ubaya gani kuzungumza kuhusu ngono kwenye kituo cha maongezi ikiwa watu ninaozungumza nao hawanijui?’

Je, Kuzungumzia Ngono Kwenye Intaneti Kuna Madhara?

Biblia huzungumza waziwazi kuhusu ngono. (Methali 5:18, 19) Ni kweli kwamba wanadamu hupendezwa sana na ngono wakati wa ujana. Kwa hiyo unapaswa kuzungumza kuhusu ngono. Unahitaji majibu kwa maswali yako kuhusu habari hii muhimu. * Hata hivyo, jinsi unavyopata majibu kwa maswali hayo kutaathiri furaha yako sasa na wakati ujao.

Ukiamua kuzungumza kuhusu ngono kwenye Intaneti, hata ikiwa unafanya hivyo na watu ambao wanadai kuwa rafiki zako, huenda ukapatwa na yale yaliyompata mwanamume mmoja kijana anayetajwa katika Biblia. Kwa sababu ya udadisi, alitanga-tanga karibu na nyumba ya kahaba. Mwanzoni, kahaba huyo alizungumza naye tu. Hata hivyo, tamaa yake ilipochochewa, hakuridhika tu na mazungumzo. “Ghafula kijana huyo akamfuata, kama ng’ombe-dume anayeenda machinjoni, . . . kama vile ndege anavyofanya haraka kuingia mtegoni.”—Methali 7:22, 23.

Vivyo hivyo, mazungumzo ya ngono kwenye Intaneti yanaweza kukusukuma utake kutosheleza tamaa zako. Kijana mmoja anayeitwa Philip anasema: “Nilikuwa nikizungumza na mtu fulani kwenye Intaneti wakati kwa ghafula, niliona picha chafu kwenye kompyuta yangu. Mtu niliyekuwa nikizungumza naye ndiye aliyenitumia picha hiyo.” Mara tamaa yako ya kutazama na kufikiria picha chafu inapochochewa, huenda ukashawishiwa kuchukua hatua nyingine kama vile kufungua kituo cha maongezi cha watu wazima pekee. * Wengi ambao huanguka katika mtego wa kutazama ponografia hufanya uasherati na kupatwa na matokeo yake yasiyoweza kuepukika.—Wagalatia 6:7, 8.

Watu wanaotaka kuzungumza nawe kuhusu ngono kwenye Intaneti hawajali masilahi yako. Watu hao usiowajua wanataka kukushawishi katika mazungumzo machafu na pengine wakuhusishe katika mambo machafu ili kutosheleza tamaa zao. * Akitaka kumlinda mwana wake dhidi ya watu ambao wangeweza kumtumia vibaya kingono, Mfalme Sulemani aliandika: “Itenge njia yako mbali naye, wala usiukaribie mlango wa nyumba yake, ili usije ukawapa wengine heshima yako, . . . ili wageni wasijishibishe kwa nguvu zako.” (Methali 5:8-10) Andiko hilo lina kanuni hii: Usikaribie vituo vya maongezi vinavyozungumzia habari za ngono ili usiwape heshima yako wageni wanaotaka tu kukutumia kutosheleza tamaa zao.

“Wale Wanaoficha Jinsi Walivyo”

Hata hivyo, huenda ukasema kwamba hutaki kuzungumza kuhusu ngono kwenye Intaneti. Kama Peter na Abigail, waliotajwa awali, huenda ukadhani kwamba kituo cha maongezi ni mahali ambapo unaweza kujieleza bila kujulikana au pasipo kuona haya. * Hata hivyo, unahitaji kujua hatari nyingine.

Kwa kuwa watu wanaowasiliana kwenye vituo vya maongezi hawajuani, basi mtu anaweza kudanganya. Abigail anasema: “Baada ya kuanzisha mazungumzo na watu, nilijifanya kuwa mtu fulani ili mazungumzo yetu yapatane.” Kama Abigail, huenda ukashawishiwa ujifanye kuwa mtu mwingine ili ukubaliwe katika kikundi fulani cha maongezi. Huenda ukaiga jinsi wanavyozungumza au kupendezwa na mambo yanayowapendeza ili tu uwe na rafiki wapya. Kwa upande mwingine, huenda ukaona kituo cha maongezi kuwa mahali pa kueleza maoni na hisia ambazo unadhani wazazi au rafiki zako hawatakubaliana nazo. Vyovyote vile, utakuwa unawadanganya wote. Kwa kujifanya kuwa mtu mwingine unapowasiliana kwenye Intaneti, unawadanganya wale unaowasiliana nao. Kwa upande mwingine, ikiwa huelezi familia au rafiki zako maoni au hisia zako za moyoni, unawadanganya.

Ingawa vituo vya maongezi vilianzishwa tu hivi majuzi, mwelekeo wa wanadamu wa kusema uongo na kudanganya umekuwako tangu kuumbwa kwa mwanadamu. Biblia inafunua kwamba mwongo wa kwanza, Shetani Ibilisi ndiye aliyeanzisha mbinu inayotumiwa na watu fulani katika vituo vya maongezi. Alijifanya kuwa mtu mwingine aliposema uwongo wa kwanza. (Mwanzo 3:1-5; Ufunuo 12:9, 10) Unaweza kuepuka kudanganywa na waongo kwa kufuata mfano wa Mfalme Daudi. Aliandika hivi: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—Zaburi 26:4.

Kama ilivyotajwa hapo awali, huenda vituo fulani vya maongezi vikawa na kusudi zuri. Hata hivyo, vijana wanaotaka kumpendeza Yehova wanapaswa kuwa waangalifu sana wanapotumia njia hiyo ya kisasa ya kuwasiliana. Ikiwa unahitaji kutumia mojawapo ya vituo hivyo kwa ajili ya kazi za shuleni, waombe wazazi wako au mtu mwingine mzima aliyekomaa awe karibu. Makala ya wakati ujao itakazia sababu nyingine mbili za kuwa mwangalifu unapotumia vituo vya maongezi. Pia itazungumzia jinsi ya kushughulikia matatizo hususa ambayo huenda yakatokea hata ikiwa wewe ni mwangalifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 15 Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kina mashauri yafaayo yanayotegemea Biblia kuhusu ngono kabla ya ndoa, kupiga punyeto, na habari nyingine kama hizo.

^ fu. 17 Vituo fulani vya maongezi vimetengwa kwa ajili ya watu wazima peke yake ili vitumiwe tu na watu wa umri fulani. Hii ni kwa sababu watu huzungumza na kutazama picha chafu. Hata hivyo, uchunguzi unaonyesha kwamba vijana, hata wengine walio na umri wa miaka tisa hudanganya kuhusu umri wao ili waruhusiwe kufungua vituo hivyo.

^ fu. 18 Kwa kuwa huwezi kujua unazungumza na nani katika kituo cha mazungumzo, huenda mtu unayezungumza naye akajitambulisha kuwa wa jinsia tofauti, lakini kwa kweli anaweza kuwa wa jinsia moja na wewe.

^ fu. 20 Kichapo A Parent’s Guide to Internet Safety kinapendekeza kwamba watu wanaotumia Intaneti wasifunue jina, anwani, au nambari zao za simu kwa watu wasiowajua ambao wanawasiliana nao kwenye vituo vya maongezi!

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Kuzungumza na watu kwenye Intaneti kunaweza kuwa hatari