Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wanawake Wanapaswa Kuficha Urembo Wao?

Je, Wanawake Wanapaswa Kuficha Urembo Wao?

Maoni ya Biblia

Je, Wanawake Wanapaswa Kuficha Urembo Wao?

“WANAWAKE wanapenda mitindo,” ndivyo alivyosema George Simonton, mbuni wa mitindo mwenye uzoefu ambaye ni profesa katika Taasisi ya Mitindo ya Teknolojia huko New York. Anaeleza hivi: “Wanawake hupenda kuonyesha kwamba wanaweza kujitegemea, wana ujasiri, nao hupenda kuboresha urembo wao . . . Ninafikiri kwamba kufanya hivyo kunaonyesha unajiheshimu na kuwaheshimu watu unaoshirikiana nao.” Naam, kwa muda mrefu kujipamba kumekuwa njia ya wanawake ya kuonyesha sifa zao, kuboresha sura zao, na kujiamini kwa kiasi fulani.

Hata hivyo, wakitumia dini kama kisingizio, watu fulani huona kuwa wanawake hawafai kujipamba. Tertullian wa karne ya tatu W.K., aliandika hivi: “Wanawake watakatifu . . . ikiwa . . . ni warembo kiasili, . . . hawapaswi kuboresha urembo wao, bali wajaribu kuupunguza.” Aliendelea kusema hivi kuhusu vipodozi: “Ni dhambi dhidi ya Mungu kwa wanawake kupaka nyuso zao mafuta, kupaka mashavu yao rangi, au kurefusha nyusi za macho yao.” Na alifafanua “mapambo” yaliyotengenezwa kwa dhahabu na fedha kuwa “mtego.”

Bado watu wengi leo wana maoni yanayopita kiasi kuhusu kujipamba kwa wanawake. Dini fulani hata huwakataza waumini wasijipake vipodozi, wasivae vito vya kujipamba, au mavazi yenye kuvutia. Je, mwanamke Mkristo anapaswa kuficha urembo wake, au anaweza kujipamba?

Maoni ya Mungu

Biblia haizungumzii kila jambo kuhusu vito na vipodozi. Hata hivyo, kuna uthibitisho wa kutosha kwamba Mungu hashutumu kujipamba katika njia hizo au katika njia nyingine.

Kwa mfano, akifafanua jinsi alivyobariki Yerusalemu, Mungu alifananisha jiji hilo na mwanamke, akisema: “Nikakupamba kwa mapambo . . . , nawe ukawa mrembo, mrembo sana.” (Ezekieli 16:11-13) Mapambo kama hayo, ingawa yalikuwa ya mfano, yalitia ndani bangili, mikufu, na vipuli. Maandiko pia hulinganisha kwa njia nzuri mapambo ya dhahabu na “mkaripiaji mwenye hekima” ambaye maneno yake hupokewa na mtu msikivu. (Methali 25:1, 12) Inaonekana kwamba ikiwa Maandiko hutoa ulinganifu huo mzuri, Mungu hawezi kuwa anapinga wanawake wasijipambe kwa kutumia vifaa hivyo maridadi ili kuboresha urembo wao.

Wanawake Wakristo Hujipamba

Maandiko fulani ya Biblia huzungumza hasa kuhusu kujipamba kwa wanawake. Mtume Paulo aliandika hivi: “Natamani wanawake wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri.” Wanapofanya hivyo kwa “kiasi na utimamu wa akili,” hilo linaweza kuonyesha kwamba wanamheshimu Mungu. (1 Timotheo 2:9, 10) Wanawake Wakristo wanapojirembesha kwa kiasi katika njia hiyo, hilo linaweza kutukuza mafundisho ya Mungu na kutaniko.

Watu fulani hubisha kwamba mistari hiyohiyo inasema kwamba kujipamba huko hakupaswi kuwa “kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mavazi yaliyo ghali sana, bali kwa njia inayowafaa wanawake wanaodai kumheshimu Mungu, yaani, kupitia matendo mema.” Je, hilo linamaanisha kwamba wanawake hawapaswi kupamba nywele zao au kuvalia vito?

La, haimaanishi hivyo; Biblia inazungumza kwa njia nzuri kuhusu kujipamba. Kwa hiyo, badala ya kupinga mapambo ya aina fulani, Paulo alikuwa akiwatia moyo wanawake wafikirie hasa kujipamba kwa sifa za Kikristo na matendo mema.

Sababu za Kujipamba

Mtume Paulo aliandika: “Sisi na tusiwe tukihukumiana tena, bali badala yake fanyeni hili kuwa uamuzi wenu, kutokuweka mbele ya ndugu kikwazo au sababu ya kujikwaa.” (Waroma 14:13) Hilo linahusianaje na mapambo tunayochagua?

Kwanza, Paulo anatuambia “tusiwe tukihukumiana.” Tunapaswa kujihadhari ‘tusiweke kikwazo mbele ya ndugu.’ Huenda mapambo yanayofaa yakatofautiana katika nchi na utamaduni mbalimbali. Kinachokubalika mahali fulani katika kipindi fulani huenda kisifae mahali pengine. Hatupaswi kuwakwaza au kuwaudhi wengine kwa kujipamba katika njia ambayo watu wa utamaduni wetu huhusianisha na maisha fulani yasiyofaa. Wanawake wanaomwogopa Mungu wanapaswa kujiuliza: Watu wengine katika jamii huonaje mavazi yangu? Je, washiriki wa kutaniko huona haya, kushangaa, au kuaibika kwa sababu ya vile mimi huvalia? Hata ikiwa mwanamke Mkristo ana haki ya kuvaa au kujipamba katika njia fulani, ataepuka kujipamba katika njia hiyo ikiwa kufanya hivyo kunaweza kuwaudhi wengine.—1 Wakorintho 10:23, 24.

Pia, kufikiria sana kuhusu jinsi mtu anavyojipamba kunaweza kumfanya awe na mtazamo usiofaa. Leo katika nchi nyingi wanawake fulani hujipamba kwa njia ya madaha ili wawavutie watu kwa njia isiyofaa kiadili. Hata hivyo, wanawake Wakristo huepuka kabisa kujipamba huko kusikofaa, huku wakijitahidi kuwa na utimamu wa akili na safi kiadili katika mahusiano yao ya kibinafsi, “ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Tito 2:4, 5.

Wanawake wanaomwogopa Mungu wanaelewa kwamba hata ingawa watajipamba, urembo wao wa kweli umo katika “yule mtu wa siri wa moyoni” na hivyo unaonekana katika mtazamo na mwenendo wao. (1 Petro 3:3, 4) Mwanamke ambaye hufanya maamuzi yanayofaa kuhusu mavazi, vipodozi, na vito atakavyovalia huheshimiwa na wengine naye humletea Muumba wake utukufu.