Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukomesha Tatizo la Kutumia Kileo Vibaya

Kukomesha Tatizo la Kutumia Kileo Vibaya

Kukomesha Tatizo la Kutumia Kileo Vibaya

“Baba yangu alikuwa mraibu wa kileo nami nilifuata kielelezo chake. Nilianza kunywa kileo nikiwa na umri wa miaka 12. Kufikia wakati nilipooa, nilikuwa nikilewa kila siku. Nilikuwa mwenye jeuri; mara nyingi polisi walikuja kusaidia familia yangu. Afya yangu ilizorota. Kileo kiliniletea tatizo la kuvuja damu nyingi tumboni, na karibu nife. Kisha ini langu likanyauka na nikapatwa na anemia. Nilijiunga na vikundi vya kujisaidia kuacha zoea hilo, lakini sikufaulu. Nilihisi kana kwamba nimenaswa katika utando wa buibui na singeweza kuponyoka.”—VÍCTOR, * ARGENTINA.

TENA na tena masimulizi kama hayo hutolewa na watu walionaswa na kileo. Kama Víctor, wanahisi kuwa wamenaswa na hawawezi kuponyoka. Je, matatizo yanayosababishwa na kileo yanaweza kushindwa au hata kuepukwa? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?

Kutambua Tatizo

Kwanza, ni muhimu kwa mtu anayekunywa kileo na kwa wale walio karibu naye kutambua kwamba kuna tatizo. Uraibu ni sehemu ndogo tu ya tatizo lenyewe. Huenda tatizo hilo likakua kadiri muda unavyopita kutokana na zoea la kunywa kwa kiasi. Kwa kushangaza, aksidenti, visa vingi vya jeuri, na matatizo ya kijamii yanayotokana na kileo, hayasababishwi na watu ambao ni waraibu wa kileo. Ona yale ambayo Shirika la Afya Ulimwenguni linasema: “Njia bora ya kupunguza matatizo yanayosababishwa na kileo katika jamii ni kushughulika hasa na watu wanaokunywa kwa kiasi badala ya wale wanaokunywa sana.” (Italiki ni zetu.) Je, wewe hunywa kupita kiwango kilichowekwa na wizara ya afya? Je, wewe hunywa kileo wakati unapopaswa kuwa macho na kutenda kwa haraka? Je, mazoea yako ya kunywa yanasababisha matatizo katika familia yako au hata kazini? Kwa kweli, “njia bora” ya kuepuka matatizo mazito baadaye ni kukubali kwamba kiasi cha kileo ambacho mtu anakunywa kinaweza kuwa hatari na kukipunguza ifaavyo. Baada ya mtu kuwa mraibu, inakuwa vigumu zaidi kubadilika.

Ni kawaida kwa watu wanaotumia kileo vibaya kukana kwamba wana tatizo hilo. Wao hudai, “mimi hunywa kama watu wengine,” au “ninaweza kuacha ninapotaka.” Konstantin, anayeishi Urusi anasema, “hata ingawa nilikuwa karibu kufa kwa sababu ya kileo sikujiona kuwa mraibu, kwa hiyo sikuchukua hatua za kuacha.” Marek anayeishi Poland, anasema: “Nilijaribu mara nyingi kuacha kunywa lakini sikukubali kwamba nilikuwa mraibu. Nilipuuza matatizo yanayohusiana na kileo.”

Mtu anaweza kusaidiwaje atambue kwamba ana tatizo la kutumia kileo vibaya kisha achukue hatua inayofaa? Kwanza, anapaswa kukubali kwamba matatizo yake yanatokana na kutumia kileo vibaya na kwamba kuacha kukitumia kutaboresha maisha yake. Kulingana na jarida La Revue du Praticien—Médecine Générale, mtu anapaswa kuacha kufikiri kwamba, “ninakunywa kileo kwa sababu mke wangu aliniacha na nikapoteza kazi,” na badala yake afikiri, “mke wangu aliniacha na nilipoteza kazi kwa sababu ya kunywa kileo.”

Ukitaka kumsaidia mraibu wa kileo abadili fikira zake huenda ukataka kufuata madokezo haya: Sikiliza kwa makini, tumia maswali yatakayomfanya mtu huyo aeleze hisia zake kwa uhuru, mwonyeshe huruma ambayo itamsaidia ahisi kwamba unaelewa hali yake, mtie moyo hata anapofanya maendeleo madogo, usimshutumu au kuwa na mtazamo utakaomzuia asijieleze waziwazi na kutafuta msaada. Huenda ikafaa pia kumwambia aandike orodha mbili zinazotegemea maswali haya, ‘Ni nini kitakachotokea nikiendelea kunywa kileo?’ na ‘Ni nini kitakachotokea nikiacha?’

Kutafuta Msaada

Mtu anapoanza kutumia kileo vibaya haimaanishi kwamba yeye ni bure au hawezi kusaidiwa. Wengine hata hufaulu kuacha zoea hilo bila msaada. Hata hivyo, huenda waraibu wa kileo wakahitaji msaada kutoka kwa wataalamu ili kuacha zoea hilo. * Watu fulani hutibiwa bila kulazwa hospitalini, lakini huenda ikafaa mtu alazwe hospitalini ikiwa kuacha kunywa kunatokeza athari mbaya. Baada ya athari za kwanza kuisha kati ya siku mbili hadi tano, huenda mtu akapewa dawa za kupunguza tamaa ya kileo, na kuendelea kujiepusha nacho.

Hata hivyo, hakuna uhakika kwamba matibabu hayo yote ya kumsaidia mraibu yatafaulu. Dawa hutoa kitulizo cha muda tu wala haziwezi kuponya. Alain anayeishi Ufaransa, alipata matibabu ya uraibu mara kadhaa. Anasema hivi: “Mara tu nilipotoka hospitali nilianza kunywa tena kwa kuwa nilishirikiana na watu walewale niliokuwa nikinywa nao. Kwa kweli, sikuwa na kichocheo cha kunifanya niache.”

Kujaza Pengo

Kwa watu wengi, kuacha kunywa huacha pengo kama lile linalotokea mtu anapopoteza rafiki wa karibu. Vasiliy anayeishi Urusi anasema: “Kila wakati nilifikiria kunywa kileo. Ikiwa siku ingepita bila kunywa kileo, basi siku hiyo ingekuwa bure.” Mraibu huona kutosheleza tamaa ya kunywa kuwa muhimu kuliko jambo lingine lolote. Jerzy anayeishi Poland anakumbuka: “Kusudi langu kuu maishani lilikuwa kunywa na kutafuta pesa za kileo.” Kwa wazi, ni muhimu mraibu anayetibiwa apate kusudi jipya maishani ili aache kunywa.

Kichapo cha Shirika la Afya Ulimwenguni chenye mashauri kwa wale wanaojaribu kubadili mazoea yao ya kunywa kileo kinakazia umuhimu wa kufanya kazi zinazofaa ili kuepuka kurudia zoea hilo. Kwa mfano, kinapendekeza kujihusisha na mambo ya kidini.

Kujishughulisha na mambo ya kiroho kunaweza kumsaidia mtu asiwe mraibu wa kileo. Kwa mfano, baada ya kukaa jela kwa mara ya tatu kwa sababu ya mambo fulani aliyofanya akiwa mlevi, Alain alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Anasema: “Nilipata kusudi maishani nilipojifunza Biblia na kufanya hivyo kulinisaidia nisirudie tatizo la kutumia kileo. Sikutaka tu kuacha kileo lakini pia nilitaka hasa kumpendeza Yehova.”

Jambo la Kufanya Zoea la Kunywa Linaporudi

Watu wanaotoa mashauri kuhusu tatizo la kutumia kileo vibaya wanakazia umuhimu wa kuwasaidia na kuwatia moyo watu wanaopambana na tatizo hilo. Wengi wamepoteza familia na marafiki kwa sababu ya hali yao yenye kusikitisha. Wanaweza kushuka moyo na hata kujiua kwa sababu ya upweke unaotokana na hali hiyo. Kichapo kilichotajwa awali kinatoa shauri lifuatalo kwa wale wanaomsaidia mtu aliye na tatizo la kileo: “Usimchambue mtu unayemsaidia hata kama tabia yake inakuudhi na kukufadhaisha. Kumbuka kwamba si rahisi kubadili mazoea. Kutakuwa na nyakati nzuri na mbaya. Utahitaji kumtia moyo, kumsaidia anywe kwa kiasi au ajiepushe na kileo, na kumpa mbinu za kumsaidia.”

Hilario ambaye alikuwa akilewa kwa miaka 30 hivi anaeleza: “Jambo lililonisaidia ni upendo na kuwa na marafiki walionijali katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Nilirudia tatizo hilo mara nyingi lakini sikuzote walinisaidia, wakanitia moyo na kunipa shauri la wakati unaofaa kutoka katika Biblia.”

Ikiwa unajitahidi kuacha kutumia kileo, kumbuka kwamba mara kwa mara utarudia zoea hilo, na kwamba unapaswa kuona jambo hilo kuwa hatua ya kuacha. Usivunjike moyo! Changanua mambo yaliyofanya urudie zoea hilo ili uweze kuyaepuka wakati ujao. Tambua hali hususa ambazo huchochea tamaa yako ya kunywa. Je, huenda ikawa ni kukosa jambo la kufanya, kushuka moyo, upweke, mabishano, mfadhaiko, au kuwa katika sherehe au mahali ambapo wengine hunywa? Basi epuka mambo hayo! Jerzy, ambaye ilimchukua miaka miwili kuacha kutumia kileo kabisa anasema hivi: “Nilijifunza kutambua na kuelewa hisia ambazo zingenichochea ninywe. Sasa mimi huepuka hali zozote zinazoweza kunifanya nitamani kunywa. Mimi huepuka mahali ambapo watu wanakunywa kileo. Sili chakula chochote chenye kileo, nami huepuka vipodozi au dawa zenye kileo. Pia sitazami tangazo lolote la kibiashara la kileo.” Wengi wameona kwamba kusali kwa Mungu awape “nguvu zinazopita zile za kawaida” kumewasaidia sana wadhibiti tamaa yao ya kunywa.—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:6, 7.

Kuwa Huru!

Ingawa inaweza kuwa vigumu kuacha uraibu wa kileo, bado inawezekana kufanya hivyo. Watu wote waliotajwa katika makala hii wamefaulu. Wana afya nzuri nao wanapata faida katika familia na kazini. Alain anasema, “Sasa nimeacha kuwa mtumwa wa kileo.” Konstantin anasema: “Kumjua Yehova kumeokoa familia yangu. Sasa nina kusudi maishani. Furaha yangu haitegemei kileo.” Víctor anasema: “Ninajihisi nikiwa huru. Sasa ninajiheshimu na nina kusudi maishani.”

Mtu anaweza kubadilika iwe anahatarishwa na kutumia kileo vibaya, anapatwa na matatizo kwa sababu ya kutumia kileo vibaya, au ni mraibu wa kileo. Ikiwa mazoea yako ya kunywa yanakuhatarisha, usisite kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Unaweza kunufaika wewe mwenyewe na kuwanufaisha wale wanaokupenda.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 10 Kuna vituo vingi vya matibabu, hospitali, na programu za kuwasaidia waraibu. Mashahidi wa Yehova hawapendekezi matibabu yoyote hususa. Mtu anapaswa kuwa mwangalifu ili asijihusishe na utendaji ambao utapingana na kanuni za Biblia. Hata hivyo, baada ya kufikiria mambo yote, kila mtu atajiamulia mwenyewe matibabu anayohitaji.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Hatua ya kwanza ni kukubali kwamba una tatizo

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wengi wanahitaji msaada wa wataalamu ili kuacha uraibu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Sala inaweza kusaidia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Unaweza kupata nguvu za kutotumia kileo!