Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kurekebisha Wafungwa Katika Magereza ya Mexico

Kurekebisha Wafungwa Katika Magereza ya Mexico

Kurekebisha Wafungwa Katika Magereza ya Mexico

Na mwandishi wa Amkeni! nchini Mexico

IMESEMEKANA kwamba wafungwa hutiwa gerezani ili warekebishwe. Hata hivyo, kifungo pekee hakiwezi kumrekebisha mfungwa. Kichocheo cha kubadilika kinapaswa kutoka akilini na moyoni, pamoja na toba ya kweli kwa makosa ambayo mtu alifanya na tamaa ya kutenda kwa njia tofauti. Katika magereza mengi ulimwenguni, wafungwa wengi wameweza kurekebishwa kwa kufunzwa Biblia na Mashahidi wa Yehova. Na tuchunguze kazi yao huko Mexico.

Mashahidi wa Yehova hutembelea magereza 150 huko Mexico, wakiwatolea wafungwa programu ya kusoma Biblia na kuwafunza kuhusu maadili na mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, katika gereza moja huko Ciudad Juárez, Chihuahua, Mashahidi wa Yehova huwahubiria kwa ukawaida wafungwa 1,200 hivi. Wafungwa huwaheshimu sana na hata huwalinda kunapokuwa na hali hatari. Wakati mmoja ghasia zilipotokea katika gereza hilo, baadhi ya wafungwa hatari zaidi waliutuliza umati ili Mashahidi waweze kuondoka kwa usalama.

Toleo la Amkeni! la Mei 8, 2001 lenye kichwa, “Je, Wafungwa Wanaweza Kurekebishwa?” liliwavutia wafungwa na vilevile wasimamizi wa magereza. Mashahidi 12 waligawa nakala 2,149 za gazeti hilo katika gereza la San Luis Río Colorado, Sonora.

Watu wanapopendezwa kikweli na Biblia, Mashahidi wa Yehova hurudi juma baada ya juma ili kuwafundisha Biblia na kuongoza ibada ya kidini. Programu hiyo ya kuwafunza watu Biblia imefanikiwa kwa kadiri gani kubadili maisha ya wafungwa?

Wafungwa Wawa Wahudumu wa Kikristo

Tayari Jorge alikuwa ameanza kujihusisha na uhalifu kabla ya kufikia umri wa miaka 20. Baada ya kutumikia kifungo cha miaka 13 katika gereza la Islas Marías, aliachiliwa. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, alianza tena biashara ya ulanguzi wa madawa ya kulevya. Akaanza kulipwa ili awaue watu na mwishowe akawa amewaua watu 32. Alipokuwa gerezani tena, alielezwa na mawakili wake kwamba watu waliokuwa wamemwajiri kazi ya uhalifu walikuwa tayari kulipa pesa nyingi ili aachiliwe. Waajiri hao walitaka aachiliwe ili akamuue mtu mwingine tena. Lakini wakati huo, Jorge alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alikuwa amefanya maendeleo ya kiroho kufikia kubatizwa na alikuwa mhubiri wa wakati wote, au mhudumu painia huko gerezani. Je, angekubali kuwa huru na kuwatumikia tena wafanyabiashara hao wa dawa za kulevya au kubaki gerezani na kumtumikia Yehova? Jorge alijibu: “Ningependa kubaki gerezani na kuadhibiwa kwa mambo mabaya ambayo nilifanya. Sasa ninamtumikia Yehova Mungu, Bwana Mwenye Enzi Kuu.” Jorge alibaki mwaminifu kwa Mungu na akafa akiwa na tumaini la kufufuliwa. Wenzake waliokuwa pia wakijifunza Biblia husema hivi kumhusu: “Yeye ‘alijua kweli, nayo kweli ikamweka huru.’”—Yohana 8:32.

David, ambaye anatumikia kifungo cha miaka 110 kwa mauaji, utekaji nyara, na wizi, amezuiliwa katika gereza la wahalifu hatari lenye ulinzi mkali. Hata hivyo, kwa sababu ya mabadiliko makubwa aliyofanya katika mwenendo wake tangu aanze kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alipewa idhini ya pekee ya kuhudhuria mikutano chini ya ulinzi nje ya gereza hilo. Amepatanisha maisha yake na matakwa ya Biblia na sasa anashiriki katika kazi ya kuhubiri na anaongoza mafunzo manane ya Biblia pamoja na wafungwa wengine gerezani. Familia yake imevutiwa sana na mabadiliko ambayo amefanya hivi kwamba wao huenda kwake ili kufundishwa Biblia. David anasema: “Mimi sichoki kumshukuru Yehova kwa kuniweka huru kiroho.”

Kwa sababu ya mafundisho ya Biblia yanayotolewa na Mashahidi wa Yehova, wafungwa 175 waliorekebishwa katika magereza 79 ya Mexico wamekubaliwa kuhubiri, na 80 kati yao wamebatizwa. Wanaongoza jumla ya mafunzo ya Biblia 703 pamoja na wafungwa wengine. Isitoshe, wafungwa wapatao 900 wanahudhuria mikutano ya Kikristo inayofanywa katika magereza hayo.

Wasifiwa na Wenye Mamlaka

Wasimamizi wa magereza wanatambua kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, maofisa katika gereza la Tekax, Yucatán waliwapa cheti cha kuwashukuru kwa sababu ya “kujitolea kwao bila ubinafsi ili kuwasaidia” wafungwa katika mwaka wa 2002.

Mafundisho ya Biblia yalipoanzishwa na Mashahidi kwa mara ya kwanza katika gereza hilo, mikutano yao ilifanywa chini ya ulinzi mkali wa walinzi kadhaa. Lakini, baada ya muda wafungwa walipoanza kubadili nyutu zao, kikundi hicho kiliheshimiwa na walinzi hivi kwamba ni mlinzi mmoja tu aliyetumwa kuwasimamia.

Gereza la Ciudad Juárez lina Jumba la Ufalme. Ruhusa ilitolewa ya kupeleka vifaa vya ujenzi ili kurekebisha kibanda fulani cha chuma kiwe mahali pa ibada. Wafungwa 13 waliobatizwa pamoja na mafunzo yao ya Biblia ndio waliofanya kazi yote ya ujenzi. Jumba hilo lina mfumo wa sauti, choo, viti kama vya jumba la sinema, na linaweza kutoshea watu 100. Watu 50 hivi huhudhuria kwa ukawaida mikutano mitano ya kila juma.

Naam, wafungwa wanaweza kurekebishwa kupitia mafundisho ya Biblia. Kama vile Manase anayetajwa katika Biblia, aliyekuwa mfalme wa Yuda ambaye alifanya mambo mabaya sana na kufungwa gerezani huko Babiloni alivyotubu na kuomba msamaha, leo wafungwa wanaweza kubadili nyutu zao na kuwa watu wanaomwogopa Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 33:12, 13.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Ubatizo ndani ya gereza

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Wahudumu wa wakati wote na walimu wao kwenye Shule ya Utumishi wa Painia ndani ya gereza