Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Urembo Nina umri wa miaka 11, nami nilifurahia sana makala yenye kichwa “Urembo Ulio Bora Zaidi.” (Desemba 22, 2004) Nyakati nyingine mimi huhangaikia sura yangu kupita kiasi. Makala hiyo imenisaidia kutambua kwamba watu hupendezwa hasa na yule mtu wa ndani.

A. L., Marekani

Sipendezwi kabisa na sura yangu. Lakini ninatumaini kwamba urembo wangu wa ndani unampendeza Yehova na kwamba anapendezwa nami na maisha yangu. Makala kama hizo ni zenye kuvutia sana na pia zenye kujenga.

M. G., Ujerumani

Vijana Huuliza Asanteni kwa kuchapisha “Vijana Huuliza . . . Vipi Akikataa?” (Desemba 22, 2004) Kama wale walionukuliwa katika makala hiyo, nilivutiwa na mwanamume fulani Mkristo lakini yeye hakupendezwa nami. Nilivunjika moyo sana. Kupatana na makala hiyo, ninasali kwa Yehova ili hasa anisaidie niwe na mambo mengi ya kiroho ya kufanya. Ningependa kupona uchungu niliopata kutokana na kisa hiki.

I. Y., Japani

Siwezi kueleza jinsi nilivyohisi niliposoma makala hiyo. Ilikuja kwa wakati unaofaa, na ilieleza hasa jinsi nilivyokuwa nikihisi! Haikuwa rahisi kuvumilia baada ya kukataliwa, lakini makala hiyo ilinisaidia nisifikirie sana jambo hilo.

M. P., Italia

Ingawa ni vigumu kufanya mambo fulani ambayo yalitajwa, ninafikiri kwamba makala hiyo imenisaidia kurudia hali yangu. Ninatumaini kwamba itawasaidia wengine wengi watambue kwamba wao ni wenye thamani machoni pa Yehova na waendelee na maisha yao!

J. E., Marekani

Makala hiyo ilinipa nguvu za kuvumilia hisia za kuvunjika moyo. Ingawa bado ninahisi vibaya kwa kukataliwa, makala hiyo ilinisaidia kupunguza uchungu niliokuwa nao. Inapendeza kujua kwamba Yehova anajali kila mmoja wetu.

M. L., Marekani

Siku ambayo nilipata gazeti hilo la Amkeni! nilipata pia barua kutoka kwa mwanamume fulani Mkristo ambaye alinikataa kwa njia ya fadhili lakini thabiti. Kwa siku nyingi sikuweza kula au kulala, lakini makala hiyo ilinisaidia kuona mambo kihalisi na kudumisha heshima yangu.

M. I., Japani

Baada ya kuumia kwa muda mrefu kwa sababu yule niliyependezwa naye hakuhisi kama mimi, nilitambua kwamba ni afadhali kukubali ukweli wa mambo. Sasa ninaona kwamba si mimi peke yangu ambaye nimeumia kwa sababu ya kukataliwa. Asanteni sana!

L. A. C., Brazili

Nilivunjika moyo na kuumizwa wakati mtu niliyependezwa naye aliponikataa. Nilitokwa na machozi niliposoma makala hiyo kwa sababu Yehova alinisaidia kupitia makala hiyo. Sasa ninajua kwamba alitaka kunisaidia nisiumie sana. Ninampenda Yehova hata zaidi.

D. O., Austria

Wazo lililotajwa katika makala hiyo ya “Vijana Huuliza” kwamba Yehova alitia ndani ya wanadamu tamaa ya kupendwa na kwamba anajua jinsi tunavyoweza kudhibiti upendo huo, lilikuwa jipya na lenye kufariji kwangu. Ningependa kuwa mtu ambaye, kama makala ya kwanza ya gazeti hilo ilivyosema, ni mrembo machoni pa Yehova, yaani, ni mrembo kwa ndani.

H. W., Japani