Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanahitaji “Wakati wa Kuwasiliana na Mtu Mzima”

Vijana Wanahitaji “Wakati wa Kuwasiliana na Mtu Mzima”

Vijana Wanahitaji “Wakati wa Kuwasiliana na Mtu Mzima”

KILA mzazi anayejali anajua kwamba watoto wachanga huwa na afya nzuri wanapoonyeshwa upendo na wanapotaka kupakatwa wao hupanda kwenye paja la mzazi. Hata hivyo, kufikia wakati wanapobalehe, inaelekea kwamba vijana watajitenga na wazazi wao, asema Dakt. Barbara Staggers, ambaye ni mkurugenzi wa matibabu ya vijana wanaobalehe katika Hospitali ya Watoto na Kituo cha Utafiti huko Oakland, California, Marekani. Lakini, huo ndio wakati katika maisha yao ambapo wanahitaji uangalifu wa wazazi hata zaidi. Kwa nini inakuwa hivyo?

Kulingana na Dakt. Staggers, vijana wanapoanza kubalehe huanza kufanya mambo bila usimamizi mwingi, na hilo linaweza kuwa hatari. Katika ripoti moja ya gazeti Toronto Star, daktari huyo anasema: “Wakati wa kubalehe, vijana wanajifunza kuhusu wao ni nani na jinsi wanavyoweza kuwa sehemu ya ulimwengu unaowazunguka. Unapohusianisha hilo na mwelekeo wa asili wa kujihusisha na hatari na uvutano wa marika, utaona kwamba wanakabili hatari kubwa.” Kubalehe hakutegemei tu umri wa kijana bali hatua nyingi zinazohusika. Kama vile Staggers anavyosema, kubalehe “kunahusisha jinsi [vijana] wanavyotenda na kuelewa habari na kujaribu mambo mbalimbali.” Katika hatua ya mapema ya kubalehe vijana hujifikiria sana, huhangaishwa na mabadiliko ya mwili, na kufanya mambo kwa kushtukia. Katika hatua ya pili ya kubalehe kijana hujaribu mambo mbalimbali ili kuona matokeo, na katika hatua ya mwisho yeye hufanya maamuzi bila kuongozwa.

Ndiyo, miaka ya ujana inaweza kusisimua, lakini pia inaweza kuwa yenye kutatanisha, kwa wazazi na watoto pia. Staggers, ambaye amewachunguza vijana kwa zaidi ya miaka 20, anasema kwamba wengi wao “wanahitaji wakati wa kuwasiliana na mtu mzima anayewajali.” Hilo linaweza kutimizwaje?

Mnapaswa kuwasiliana! Wazazi, wahakikishieni watoto wenu kwamba mnawajali kwa kuwasikiliza. Waonyeshe vijana wako kuwa unajali kwa kuwauliza maswali yatakayowasaidia wafikiri vizuri na kuwasaidia watambue matokeo ya maamuzi yoyote mabaya watakayofanya. Taja matokeo mazuri wanayoweza kupata kwa kufanya maamuzi mazuri. Wasaidie wajue tabia inayokubalika.

Wazazi wakifuata maoni ya watu wengi kwamba watoto wanapaswa kujifunza kushughulikia matatizo yao wenyewe, watoto wanaweza kuathiriwa na watu wapotovu na wasio na maadili. (Methali 13:20) Kwa upande mwingine, wazazi ambao hufuata mashauri ya Biblia watawapa watoto wao nafasi bora zaidi ya kubalehe na kuwa watu wazima wenye kutegemeka. Kwa hiyo, wazazi wanapaswa kujifunza ‘kumlea mvulana kulingana na njia inayomfaa.’—Methali 22:6.

Habari zinazofaa kuhusu njia bora ya kuwasiliana na kuwazoeza vijana inapatikana katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. * Pia kitabu hicho hutoa mashauri yanayofaa kwa ajili ya kila mtu katika familia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.