Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kunufaika na Magazeti

Jinsi ya Kunufaika na Magazeti

Jinsi ya Kunufaika na Magazeti

“Mtu asiyesoma gazeti ni mpumbavu, na yule anayeamini mambo anayosoma kwa sababu tu yako katika gazeti ni mpumbavu hata zaidi.”—August von Schlözer, mwanahistoria na mwandishi wa habari Mjerumani aliyeishi mwishoni mwa karne ya 18.

KATIKA uchunguzi mmoja, maelfu ya watu huko Uingereza na Ufaransa waliulizwa walitumaini shirika gani zaidi kati ya mashirika 13. Vyombo vya habari vilivuta mkia, hata baada ya siasa na makampuni makubwa. Nchini Marekani, bado wasomaji wengi huamini magazeti ya kwao. Lakini uchunguzi uliofanywa na Kituo cha Utafiti cha Pew unaonyesha kwamba idadi ya watu wanaoamini magazeti imepungua.

Mara nyingi kuna sababu nzuri ya kushuku mambo yaliyoandikwa hasa ikiwa yanahusu masilahi ya nchi ambako gazeti hilo huchapishwa. Inakuwaje basi? Mara nyingi ukweli hupuuzwa. Kama vile mwanasiasa Mwingereza, Arthur Ponsonby, wa karne ya 20 alivyosema wakati mmoja: “Vita vinapotangazwa, Ukweli ndio huathiriwa kwanza.”

Hata wakati vita havijatangazwa, ni jambo la hekima kushuku kwa kadiri fulani habari unayosoma. “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno,” inasema methali moja ya Biblia, “lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Ukiwa mwangalifu kwa kiasi fulani, magazeti yanaweza kutosheleza tamaa yako ya habari unazohitaji.

Umuhimu wa Habari

Vyombo vya habari ni muhimu leo kwa sababu vinatusaidia tujue mambo yanayotendeka ulimwenguni. Na ni muhimu kujua habari hizo. Kwa nini? Kwa sababu mambo mengi yanayotukia leo yalitabiriwa na nabii mkubwa zaidi aliyepata kuishi, Yesu Kristo. Alipoulizwa kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo, alisema kwamba wakati wa mwisho kungekuwa na vita, ongezeko la uasi-sheria, upungufu wa chakula, tauni, matetemeko ya nchi, na matukio mengine yanayohusiana na hayo.—Mathayo 24:3-14; Luka 21:7-11.

Pia Biblia inasema: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Unabii huo unaongezea kusema kwamba katika ‘siku hizi za mwisho,’ watu watakuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa,” na “wasiotii wazazi.” Watakuwa “wasio na upendo wa asili” na “wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-5.

Bila shaka unaona unabii huo wa Biblia ukitimizwa mahali unapoishi. Na kwa kweli matukio ya ulimwenguni pote ambayo yanaripotiwa katika magazeti huthibitisha usahihi wa unabii wa Biblia. Je, hiyo inamaanisha kwamba tunaweza kuamini mambo yote tunayosoma katika magazeti? La, hata watu ambao wamejitoa kufanya kazi ya kuandika magazeti wanasema kwamba tunahitaji kuwa waangalifu.

Elewa Matatizo Yanayohusika

Kila mtu, hata watu walio stadi na wanyoofu zaidi, hukosea. Ariel Hart aliandika hivi katika gazeti Columbia Journalism Review: “Katika miaka mitatu ambayo nimefanya kazi ya kujiajiri ya kuthibitisha ukweli wa habari zinazotolewa sijawahi kupata habari ambayo haikuwa na makosa, iwe ilikuwa ya kurasa tano au mafungu mawili.” Anataja mifano ya makosa aliyopata kama vile “mwaka usio sahihi; habari za zamani; makosa ya herufi; habari iliyosambazwa sana ambayo ilitokana na vyanzo visivyotegemeka.”

Lazima waandishi wa habari wakabiliane na vyanzo vya habari visivyotegemeka. Nyakati nyingine, mizaha hutumwa kwenye vyumba vya habari. Mnamo 1999, mfanya-mizaha mmoja aliweka kwenye Intaneti hadithi fulani ya uwongo kuhusu “bustani ya burudani kwenye makaburi,” na kuthibitisha habari hiyo kwa kutaja kituo chenye kuvutia cha kampuni ambayo ingejenga bustani hiyo na nambari ya simu ambayo mdanganyi huyo alitumia kwa ajili ya mahojiano akidai kuwa ni msemaji wa kampuni hiyo. Huduma za satelaiti za shirika la habari la Associated Press hazikugundua mzaha huo, na magazeti mengi ya kila siku huko Marekani yalichapisha habari hiyo. Inasemekana kwamba siri ya kufanikiwa kwa mizaha hiyo ni “kutunga hadithi yenye kusisimua iliyo na picha nyingi za ajabu-ajabu lakini zenye kuaminika.”

Hata waandishi wa habari wenye nia nzuri sikuzote hawaelewi hadithi kwa usahihi. “Kwa kawaida, waandishi wa habari hufanya kazi haraka-haraka,” anasema mwandishi mmoja huko Poland. “Magazeti yanashindana. Kila moja linataka liwe la kwanza kuchapisha habari. Kwa sababu hiyo, ingawa wengi wetu tungependa kuandika makala iliyofanyiwa utafiti mzuri, hatuwezi.”

Mkazo wa Kufuata Mapendezi ya Watu

Kichapo Freedom of the Press 2003—A Global Survey of Media Independence kiliorodhesha nchi 115 kati ya 193 kuwa hazina uhuru au zina uhuru wa kiasi tu. Hata hivyo, hata katika nchi zenye uhuru wa kusambaza habari, vyombo vya habari vinaweza kutumiwa vibaya kwa hila.

Nyakati nyingine, waandishi fulani wa habari hunyimwa habari muhimu, huku wale ambao huwapendeza wanasiasa huruhusiwa kuwahoji na hata kuandamana nao wanaposafiri. Pia mapato yanayotokana na matangazo ya biashara yanaweza kuathiri kuripotiwa kwa habari. Mwandishi mmoja wa habari huko Poland alisema: “Kampuni inayodhamini matangazo fulani katika magazeti inaweza kutisha kuondoa matangazo hayo ikiwa mhariri atachapisha habari mbaya kuihusu.” Na mhariri mmoja wa gazeti fulani huko Japani, ambaye husahihisha habari kabla haijachapishwa alionya hivi: “Kumbuka kwamba si rahisi hata kidogo kuripoti habari zisizopendelea upande wowote.”

Basi huenda ukauliza, ‘ikiwa waandishi stadi wa habari hukabili matatizo kama hayo ili kutokeza habari zinazoaminika, msomaji atajuaje habari anazopaswa kuamini?’

Maoni Yaliyosawazika Yanahitajika

Bila shaka, utambuzi unahitajiwa. Mzee wa ukoo Ayubu aliuliza hivi: “Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?” (Ayubu 12:11) Msomaji anahitaji kuchunguza habari kwa uangalifu ili kuona kama ni ya kweli. Kwa hekima, yeye huipima na kuchagua habari ya kweli. Katika karne ya kwanza, mwanafunzi mmoja wa Yesu Kristo aliwasifu wale waliomsikiliza mtume Paulo lakini wakachunguza vyanzo vya habari ya Paulo ili kuthibitisha ukweli wa mafundisho yake.—Matendo 17:11; 1 Wathesalonike 5:21.

Vivyo hivyo, huenda msomaji wa gazeti akajiuliza maswali haya: Mwandishi wa habari ana uzoefu gani? Yeye huchukia mambo gani? Je, habari aliyoandika inataja mambo hakika ambayo watu wanaweza kuthibitisha? Je, kuna mtu yeyote ambaye angependa kupotosha ukweli wa habari hii? Kwa hekima, huenda msomaji akachunguza vyanzo mbalimbali ili kuthibitisha usahihi wa habari hiyo. Anaweza pia kuzungumza na wengine kuhusu mambo anayosoma. Methali moja ya Biblia inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—Methali 13:20.

Wakati huohuo tusitazamie magazeti yaseme mambo kwa usahihi kabisa. Kama tulivyoona, kuna mambo mbalimbali ambayo huzuia magazeti yasiandike habari zisizopendelea upande wowote. Hata hivyo, bado yanaweza kukusaidia kujua mambo yanayotendeka ulimwenguni. Ni muhimu kujua mambo hayo kwa kuwa Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu nyakati tunamoishi, alihimiza hivi: “Endeleeni kukesha.” (Marko 13:33) Magazeti yanaweza kukusaidia kukesha hata ingawa hayataji mambo kwa usahihi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

VYOMBO VYA HABARI VINAPOONYESHA UBAGUZI

Mara nyingi, habari zenye kupotosha hutokana na ripoti zilizotayarishwa haraka-haraka au habari zisizo sahihi. Hata hivyo, habari hizo zilizotolewa kwa nia nzuri zinaweza kueneza upesi uwongo mbaya. Kwa upande mwingine, nyakati nyingine habari zenye kupotosha hutolewa kimakusudi, kama ilivyotukia katika Ujerumani ya Nazi wakati uwongo ulipoenezwa kuhusu watu wa jamii na dini fulani.

Fikiria matokeo ya kampeni ambayo haikufaulu iliyofanywa hivi karibuni ya kuwaharibia sifa Mashahidi wa Yehova katika kesi ya kupigania haki za binadamu huko Moscow, Urusi. “Wasichana watatu walipojiua huko Moscow,” gazeti The Globe and Mail la Toronto, Kanada, liliripoti kwamba “mara moja vyombo vya habari vya Urusi vilidokeza kwamba walikuwa wafuasi shupavu wa Mashahidi wa Yehova.”

Habari hizo zilichapishwa Februari 9, 1999, siku ambayo mahakama iliendeleza kesi iliyokusudiwa kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova jijini Moscow. Geoffrey York, ripota kwenye Kituo cha gazeti The Globe and Mail huko Moscow aliripoti hivi: “Baadaye polisi walikiri kwamba wasichana hao hawakuwa na uhusiano wowote na madhehebu hayo. Lakini kufikia wakati huo, tayari kituo kimoja cha televisheni huko Moscow kilikuwa kimeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya madhehebu hayo, kikiwaambia watazamaji kwamba Mashahidi wa Yehova walishirikiana na Adolf Hitler katika Ujerumani ya Nazi licha ya uthibitisho wa kihistoria kwamba maelfu ya wafuasi wao waliuawa katika kambi za kifo za Nazi.”

Matokeo yalikuwa kwamba watu wengi wasiojua ukweli au wenye kuhofu waliwaona Mashahidi wa Yehova kuwa ama madhehebu ya kujiua au washirika wa Nazi!

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu Kristo alitabiri mambo mengi tunayoona yakiripotiwa katika magazeti leo

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mambo yanayoripotiwa katika magazeti huthibitisha unabii wa Biblia

[Hisani]

FAO photo/B. Imevbore

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Watu waliothibitisha vyanzo vya mafundisho ya mtume Paulo walisifiwa, hivyo basi ni jambo la hekima pia mtu kufanya hivyo anaposoma habari zisizo za kawaida