Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoa Faraja Wakati wa Msiba

Kutoa Faraja Wakati wa Msiba

Kutoa Faraja Wakati wa Msiba

Dolores Gómez, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika mji mdogo karibu na Barcelona, Hispania, alikuwa na umri wa miaka 44 alipoambiwa na daktari wake kwamba alikuwa na uvimbe katika ubongo. Alisema kwamba hataishi kwa zaidi ya miezi minane. Wakristo wenzake walimwonyesha upendo mwingi sana. Siku chache kabla ya kifo chake, watu wake wa ukoo, ambao si Mashahidi, walikuja kutoka sehemu mbalimbali za Hispania.

Mashahidi wa eneo hilo waliwatunza, wakawapa mahali pa kulala, chakula, usafiri, na vitu vingine walivyohitaji. Imani yake thabiti na utulivu ambao Dolores alidumisha hadi mwisho na pia ukaribishaji ambao Mashahidi wa eneo hilo walionyesha, uligusa mioyo ya watu wa familia yake. Barua ifuatayo ilieleza hisia zao.

“Barua hii ni kwa ajili ya kikundi cha wanaume na wanawake ambao hawahubiri tu kwamba wanawapenda wanadamu wenzao bali pia wao huonyesha kwa matendo upendo wao wa kutoka moyoni. Tumejifunza jambo hilo wakati wa hali ya pekee maishani mwetu, yaani, wakati wa ugonjwa wa dada yetu Loli [Dolores].

“Kwa hiyo, sisi sote (watu wake wa ukoo kutoka sehemu za mbali za Hispania) tukiwa na uchungu uleule wa kumpoteza tungependa kuwashukuru sana na kuwaeleza hisia zetu nyinyi nyote mliokuwa pamoja naye wakati wa shangwe na wa majonzi, na katika hali nzuri na mbaya, hadi mwisho wa maisha yake duniani.

“Pia, tungependa kuwajulisha kwamba tumeona watu wenye umoja na wanaopendana sana. Tunarudi kwetu, kwa familia zetu na kwa shughuli zetu lakini hali zitabadilika, kwani tumeguswa moyo na upendo wenu na wa dada yetu Loli, ambao unatutia nguvu za kuendelea kuishi siku baada ya siku.

“Tunawaaga kwa hisia nyingi na shukrani za kutoka moyoni. Hadi tutakapoonana tena, enyi marafiki, Yehova na awape shangwe.”

Imetiwa sahihi na familia na ndugu na dada za Dolores Gómez

[Picha katika ukurasa wa 31]

Baadhi ya Mashahidi wa huko