Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutosheleza Uhitaji wa Habari

Kutosheleza Uhitaji wa Habari

Kutosheleza Uhitaji wa Habari

“WAATHENE wote na wageni waliokuwa wakikaa huko kwa muda hawakuwa wakitumia wakati wao wa starehe wakifanya chochote ila kuambiana jambo au kusikiliza jambo jipya,” akaripoti Luka, mwandishi wa Biblia, miaka 2,000 hivi iliyopita. (Matendo 17:21) Karne moja mapema, serikali ya Roma ilipotambua hamu ya watu ya kupata habari, ilianza kubandika Acta Diurna, yaani, matangazo ya kila siku, mahali ambapo watu wengi wangeweza kuyaona.

Kufikia karne ya saba, Wachina walikuwa wakichapisha gazeti la kwanza lililoitwa, Dibao (Pao). Huko Ulaya, ambapo watu wengi bado walikuwa hawajui kusoma na kuandika, watu waliokuwa wakisafiri na kusimulia hadithi walieneza habari kuhusu vita, misiba, uhalifu, na mambo mengine. Baadaye, habari kuhusu mambo hayo iliandikwa na picha kuchorwa kwa mikono kwenye vipande vya mbao ambavyo viliuzwa kwenye masoko na maonyesho.

Hatimaye, kampuni za kibiashara ziliboresha barua zao rasmi kwa kutia ndani habari muhimu. Mwishowe, habari hizo zilichapishwa kwenye ukurasa wa ziada ulioitwa nova (habari), ambao ungeweza kusambazwa.

Mwanzo wa Magazeti

Mwanzoni mwa karne ya 17, magazeti mawili ya Ujerumani yalianza kuchapishwa kwa ukawaida. Lile lililoitwa Relation (kusimulia habari), la huko Strasbourg, lilichapishwa mara ya kwanza mnamo 1605; nalo Avisa Relation oder Zeitung (habari zenye mashauri), la huko Wolfenbüttel, lilianza kuchapishwa mwaka wa 1609. Gazeti la kwanza la kila siku huko Ulaya liliitwa Einkommende Zeitungen (Habari Motomoto), nalo lilichapishwa huko Leipzig, Ujerumani, mwaka wa 1650.

Gazeti hilo la kwanza la kila siku huko Leipzig lilikuwa na kurasa nne zenye ukubwa wa kutoshea mfukoni. Kurasa hizo zilikuwa na habari ambazo hazikuwa na mpangilio wowote. Nakala mojamoja za gazeti hilo hazikuwa ghali, lakini andikisho la mwaka mzima lingeweza kugharimu mshahara wa mwezi moja wa mfanyakazi aliyelipwa vizuri. Hata hivyo, uhitaji wa magazeti uliongezeka haraka. Kufikia mwaka wa 1700, Ujerumani peke yake ilikuwa na magazeti ya kawaida 50 hadi 60 ambayo yalisomwa na mamia ya maelfu ya watu.

Mwanzoni, vyanzo vya habari vilikuwa barua, magazeti mengine, wakuu wa posta waliopokea habari kupitia barua na kuinakili, au uvumi uliosikiwa tu na waleta-habari katika sehemu za umma. Hata hivyo, kwa sababu ya kutokea kwa makampuni mengi ya magazeti, wachapishaji walijitahidi kuongeza kiasi cha habari na kuiboresha. Waliajiri wahariri wao wa kwanza stadi. Na kwa kuwa wachapishaji wengi hawangeweza kugharimia mfumo mkubwa wa kupata habari na waandishi wa habari, hamu ya kupata habari ilifanya mashirika ya habari yaanzishwe ili kukusanya na kueneza habari kwa wachapishaji waliojiandikisha.

Uvumbuzi Muhimu

Biashara ya magazeti haingekuwapo bila uvumbuzi muhimu, hasa ule wa Johannes Gutenberg wa mashini iliyochapa herufi mojamoja. Uvumbuzi zaidi ulirahisisha na kupunguza gharama za uchapishaji wa magazeti. Kwa mfano, katika miaka ya 1860, matbaa pana zinazozunguka zilifanya iwezekane kuchapisha habari kwa mfululizo kwenye makaratasi yaliyovingirishwa badala ya kuchapa kurasa mojamoja. Muda mfupi baadaye, mashini ya Linotype ilitumiwa kupanga herufi za chapa za chuma katika kurasa ili kuchapishwa. Kisha, katika sehemu ya mwisho ya karne ya 20, kupanga kurasa kwa kutumia kompyuta kulichukua mahali pa kazi iliyogharimu sana na iliyofanywa kwa mkono.

Wakati huohuo, habari zilisambazwa haraka sana wakati telegramu ilipoanza kutumiwa katika miaka ya 1840, taipureta katika miaka ya 1870, na simu karibu wakati huohuo. Hivi karibuni zaidi, wakati ambapo kuna mamilioni ya watu, magazeti hutumia kompyuta, barua-pepe, na faksi. Maripota hufika mahali penye tukio fulani haraka zaidi kwa gari-moshi, gari, na ndege. Magazeti mengi zaidi husambazwa kupitia njia ya usafiri wa haraka.

Ni Habari Gani Huripotiwa Magazetini?

Katika sehemu nyingi, si tatizo kupata habari za kutosha katika ulimwengu huu unaozidi kuwa mdogo. Kulingana na wahariri wa gazeti Frankfurter Allgemeine Zeitung, “Tatizo ni kuchagua habari kutoka vyanzo vingi sana visivyo na kikomo.” Mashirika ya habari huletea magazeti ya Ujerumani hadithi na habari 2,000 hivi kila siku. Maripota, waleta-habari, habari za televisheni, na vyanzo vingine huwaletea wahariri wa magazeti habari chungu nzima.

Thuluthi mbili ya habari huwa matangazo, yaani, taarifa kwa waandishi wa habari na ripoti kuhusu matukio yaliyopangwa kama vile tamasha, michezo, na mikutano. Wahariri wanapaswa kujua mahitaji ya wasomaji wao ili kuandaa habari ambazo watu wanahitaji kujua kama vile matokeo ya mavuno, siku za kukumbukwa, na maadhimisho.

Watu hupenda sana kurasa zenye habari za michezo, safu za vichekesho, katuni kuhusu siasa, na tahariri. Habari kuu, ripoti kutoka nchi za kigeni, na mahojiano na watu mashuhuri na wataalamu wa masuala hususa zinaweza kuwa zenye kuelimisha na kuburudisha.

Magazeti Yanakumbwa na Matatizo

Gazeti Die Zeit liliripoti hivi mwaka wa 2002: “Biashara ya magazeti huko Ujerumani inakabili matatizo makubwa zaidi ya kifedha katika historia yake.” Na Shirika la Habari la Uswisi liliripoti kwamba katika mwaka wa 2004 idadi ya magazeti yaliyosambazwa ilikuwa chini sana, kwani hiyo ilikuwa idadi ndogo zaidi ambayo shirika hilo limesambaza katika miaka kumi. Kwa nini uhitaji wa magazeti umepungua?

Sababu moja ni kuzorota kwa uchumi ulimwenguni pote, na hivyo kupunguza matangazo ya biashara ambayo yalichangia thuluthi mbili ya mapato ya magazeti mengi. Kati ya mwaka wa 2000 na 2004, gazeti la Marekani, Wall Street Journal lilipoteza asilimia 43 ya mapato yake ya matangazo ya biashara. Je, mapato yanayotokana na matangazo hayo yataongezeka uchumi ukiboreka? Matangazo mengi madogo kuhusu mashamba na nyumba, kazi, na magari sasa hutangazwa kwenye Intaneti. Leo magazeti hushindana na vyombo vingine vya habari kama vile redio, televisheni, na Intaneti.

Kwa upande mwingine, bado kuna uhitaji mkubwa wa habari. Axel Zerdick, profesa wa masuala ya kiuchumi ya vyombo vya habari aliliambia hivi gazeti moja la Frankfurt, Ujerumani: “Tatizo hilo si baya sana kama waandishi wengi wa habari wanavyodhani.” Mhariri mkuu wa gazeti moja la kila siku la Ujerumani alikubaliana na maoni hayo aliposema: ‘Gazeti tunalochapisha bado linatia fora.’

Hata kama magazeti yana habari nyingi sana na yana uwezo wa kuathiri maoni ya watu, bado swali ni: Je, unaweza kutegemea habari yanayotoa? Unawezaje kunufaika na yale unayosoma magazetini?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

WAANDISHI WA HABARI WANA KAZI NGUMU

Huenda mtu akatamani kazi ya uandishi wa habari. Mtu mmoja ambaye amekuwa mwandishi wa habari kwa muda mrefu huko Ufaransa alisema: “Mwandishi wa habari anaweza kujitukuza anapoona jina lake kwenye gazeti.” Hata hivyo, anaweza kupata mfadhaiko kwa sababu ya kazi hiyo. Kwa mfano, hadithi ambayo mtu alitaka kuchapisha inaweza kuripotiwa na mwandishi wa gazeti lingine, mahojiano yakataliwe, na anaweza kungojea kwa muda mrefu tukio fulani kisha likose kutokea.

Mwandishi fulani wa magazeti huko Poland alitaja tatizo lingine. “Hatujui ni lini tutakuwa kazini na ni lini tutakuwa tukipumzika. Nyakati nyingine wakati wetu wa faragha huingiliwa, na huenda kazi ikavuruga maisha yetu ya familia.” Na aliyekuwa mwandishi wa habari katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti alitaja jambo ambalo labda hufadhaisha hata zaidi: “Nilifanya kazi kwa bidii, lakini mwishowe habari hiyo haikuchapishwa.”

Mwandishi wa habari za michezo wa gazeti linalosomwa na watu wengi zaidi nchini Uholanzi alisema hivi: “Mara nyingi mimi huambiwa kwamba sijui chochote. Wasomaji fulani hukasirika au kufadhaika, na kwa kuwa nyakati nyingine michezo hufanya hisia za watu kupanda, wengine hata wametisha kuniua.” Hivyo basi, ni nini huwachochea waandishi wa habari kuendelea na kazi yao?

Bila shaka, kwa wengine ni mshahara wanaopata. Lakini si wote. Mwandishi wa habari anayeandika makala katika gazeti fulani nchini Ufaransa alisema kwamba yeye hufurahia sana kuandika. Mwandishi mmoja wa habari huko Mexico alisema: “Angalau sisi hufaulu kutoa habari ambazo watu wanahitaji kujua.” Na huko Japani, mhariri mkuu wa gazeti la kila siku la pili kusomwa na watu wengi zaidi ulimwenguni alisema: “Mimi hufurahi ninapohisi kwamba nimewasaidia watu na haki inapotekelezwa.”

Bila shaka, si waandishi wa habari pekee wanaohusika katika uchapishaji wa magazeti. Ikitegemea ukubwa na mpangilio wa kampuni ya uchapishaji, huenda kukawa na wahariri, wasomaji wa nakala za masahihisho, wale wanaothibitisha ukweli wa habari zinazotolewa, wahifadhi-nyaraka, na wengine wengi wasiotajwa ambao hufanya kazi kwa bidii ili uweze kupata gazeti.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Gazeti la zamani la Ujerumani na magazeti ya kisasa

[Hisani]

Early German newspaper: Bibliothek für Kunst - und Antiquitäten-Sammler, Vol. 21, Flugblatt und Zeitung, 1922