Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulihisi Msaada wa Mungu Wenye Kuimarisha

Tulihisi Msaada wa Mungu Wenye Kuimarisha

Tulihisi Msaada wa Mungu Wenye Kuimarisha

SIMULIZI LA ESTHER GAITÁN

“Tumemteka nyara mama yako. Usijaribu kuwaita polisi. Subiri tu tutakupigia simu kesho asubuhi na mapema.”

DADA yangu mdogo, alipokea simu hiyo kumhusu mama yetu, Esther, Jumanne fulani mwaka jana. Mimi na mume wangu Alfredo tulikuwa tumetoka tu mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova nilipopata habari hiyo. Tulipofika kwa wazazi wetu huko Mexico City, tayari jamaa zetu walikuwa wamewasili. Dada yangu mdogo na ndugu yangu walikuwa na majonzi tele, nao dada za Mama walikuwa wakilia.

Baba na kaka yangu walikuwa wamesafiri kwa shughuli za kibiashara. Baada ya kuzungumza nao kwa simu, sote tulikubaliana kwamba ingefaa kuwajulisha polisi. Tulisali usiku kucha ili kupata msaada. Tulihisi kwamba Mungu alikuwa akitupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Wakorintho 4:7.

Asubuhi iliyofuata, mimi ndiye niliyeongea na watekaji-nyara kwa simu. Ingawa nilikuwa na wasiwasi mwingi, niliweza kuzungumza kwa utulivu. Mtekaji-nyara huyo alitaka kuzungumza na baba, lakini nikamwambia kwamba amesafiri. Kisha mtu huyo akasema kwamba watasubiri hadi Baba arudi ndipo waanze mashauriano. Alionya kwamba kama hatungelipa kiasi kikubwa cha pesa, wangemuua mama.

Siku iliyofuata nilijibu simu hiyo tena. Kwa kuwa nilisikika kuwa mtulivu licha ya vitisho vyake, mtekaji-nyara huyo aliuliza: “Je, hutambui uzito wa jambo hili?”

Nilimjibu: “Bila shaka ninatambua. Mmemteka nyara mama yangu. Lakini sisi ni Mashahidi wa Yehova, na tuna hakika kabisa kwamba Mungu wetu atatusaidia. Nayo Biblia hututayarisha kuvumilia nyakati hizi ngumu tunamoishi.”

“Ndiyo. Ndiyo. Ninajua yote hayo,” akajibu. “Mama yenu anasema mambo hayohayo. Anamtumaini Mungu na kuitumaini familia yake sana.” Kwa hiyo tulijua kwamba Mama anaendelea kushikilia imani yake, na jambo hilo lilituimarisha.

Msaada wa Kuvumilia

Siku zilipoendelea kupita, Wakristo wenzetu walitupigia simu na kututumia kadi na ujumbe. Tuliendelea kuhudhuria mikutano yetu na kuhubiri. Pia tulifarijika kwa kusoma Biblia kila siku na vichapo vinavyotegemea Biblia. Zaidi ya yote, sala ilitupa “amani ya Mungu.”—Wafilipi 4:6, 7.

Polisi mmoja alisema hivi: “Katika miaka tisa ambayo nimekuwa katika idara ya polisi, nimeona familia nyingi zikikata tamaa, lakini ninyi ni tofauti. Mmeonyesha utulivu wa hali ya juu. Nina hakika ni kwa sababu ya Mungu mnayemwabudu.”

Tulimwonyesha gazeti la Amkeni! la Desemba 22, 1999, lililokuwa na kichwa “Utekaji-Nyara—Sababu Ni Tisho la Tufeni Pote,” ambalo tulikuwa tumelisoma tena. Alilisoma na kuomba nakala zaidi, huku akisema kwamba angependa kuwafahamu Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi.

Hatimaye, baada ya majadiliano yaliyochukua siku 15, watekaji-nyara hao walimwachilia mama. Alikuwa mzima, ingawa walikuwa wameweka kwenye chumba kidogo huku miguu yake ikiwa imefungwa. Hata hivyo, walimtendea kwa heshima na kumpa dawa alizokuwa akitumia kwa ajili ya ugonjwa wa kisukari na kupanda kwa shinikizo la damu.

Mama alieleza jinsi alivyokabiliana na hali hiyo kwa mafanikio. Alisema: “Mwanzoni, niliogopa sana; lakini nikaanza kusali kwa Yehova, naye hakuacha nivunjike moyo. Sikujihisi mpweke katika chumba hicho kidogo. Nilitambua jinsi Yehova alivyo halisi kwangu; hakuniacha kamwe. Nilimwomba anisaidie kuonyesha matunda ya roho yake, na zaidi ya yote, niwe na subira.

“Kwa msaada wa Mungu, sikulia kamwe au kuwa na hofu. Nilitumia wakati huo kukumbuka maandiko yote ya Biblia niliyojua, na vilevile kuimba nyimbo zetu za Ufalme kwa sauti. Nyakati nyingine niliwazia kwamba niko kwenye mikutano ya Kikristo na ninashiriki kutoa maelezo. Pia niliwazia kwamba ninawahubiria watu na kuongoza mafunzo ya Biblia. Nilijishughulisha sana na mambo hayo hivi kwamba wakati ulisonga upesi.

“Hata nilipata nafasi ya kuwaeleza watekaji-nyara hao kuhusu imani yangu. Kila mara mmoja wao aliponiletea chakula, nilimhubiria hata ingawa nilikuwa nimefunikwa macho. Kwa mfano, pindi moja nilimwambia mtekaji-nyara mmoja kwamba Biblia ilitabiri nyakati ngumu tunamoishi na kwamba nilielewa kuwa lazima wawe walikuwa na uhitaji mkubwa wa pesa. Nilimwambia kwamba Yehova Mungu ana nguvu zisizo na mipaka lakini hazitumii vibaya kamwe. Kisha nikamwomba wasitumie uwezo wao vibaya kunidhuru bali wanitendee kwa haki.

“Mtekaji-nyara huyo alinisikiliza na kuniambia nisiwe na wasiwasi, hawatanidhuru. Ninamshukuru Yehova kwa kunitegemeza katika pindi hizo ngumu, na sasa kuliko wakati mwingine wowote, nimeazimia kuendelea kumtumikia nikiwa painia wa kawaida [mweneza-injili wa wakati wote] kwa kadiri niwezavyo.”

Bila shaka, jaribu hilo lilimfanya Mama na sisi sote tumkaribie Yehova zaidi. Tunashukuru sana kwamba Mama amerudi nyumbani. Tunafarijika kujua kwamba chini ya Ufalme wa Mungu mambo hayo maovu hayatakuwako tena. Sasa, mimi na familia yangu tunaweza kushuhudia ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi wa Biblia: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.”—Zaburi 34:19.