Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Huwabagua Wanawake?

Je, Biblia Huwabagua Wanawake?

Maoni ya Biblia

Je, Biblia Huwabagua Wanawake?

KATIKA mojawapo ya vitabu vyake, Tertullian, mwanatheolojia wa karne ya tatu aliwataja wanawake kuwa “mlango ambao shetani hupitia.” Wengine wametumia Biblia kuonyesha kwamba wanawake si muhimu sana kama wanaume. Kwa sababu hiyo, watu wengi huhisi kwamba Biblia huwabagua wanawake.

Elizabeth Cady Stanton, mwanamke wa karne ya 19 ambaye alianzisha kampeni ya kupigania haki za wanawake huko Marekani alihisi kwamba “Biblia na Kanisa zimekuwa vizuizi vikubwa katika jitihada za kuwakomboa wanawake.” Pindi fulani, Stanton alisema hivi kuhusu vitabu vitano vya kwanza vya Biblia: “Sijawahi kusoma vitabu vingine ambavyo hufundisha kwamba mwanamke anapaswa kutiishwa na kushushiwa heshima kama vitabu hivyo.”

Ingawa leo watu fulani bado hushikilia maoni hayo yasiyosawazika, wengi huamini kwamba sehemu fulani za Biblia huunga mkono ubaguzi dhidi ya wanawake. Je, maoni hayo yana msingi?

Maandiko ya Kiebrania Huwaonaje Wanawake?

“Tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.” (Mwanzo 3:16) Wachambuzi husema kwamba andiko hilo ni hukumu ya Mungu kwa Hawa na kwamba Mungu alikubali mwanamke atumikishwe na mwanamume. Hata hivyo, andiko hilo halikuwa likitangaza kusudi la Mungu, bali lilikuwa taarifa sahihi iliyotaja matokeo yenye kusikitisha ya dhambi na kukataa utawala wa Mungu. Kutendewa vibaya kwa wanawake kunasababishwa moja kwa moja na kutokamilika kwa mwanadamu, wala si mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, wake kutoka utamaduni mbalimbali hutawaliwa na waume zao, na mara nyingi kwa ukatili. Lakini hilo halikuwa kusudi la Mungu.

Wote wawili, Adamu na Hawa waliumbwa kwa mfano wa Mungu. Isitoshe, wote walipokea amri kutoka kwa Mungu ya kuzaa, kujaza dunia, na kuiitisha. Walikuwa wafanye kazi kwa ushirikiano. (Mwanzo 1:27, 28) Kwa wazi, kufikia wakati huo, hakuna mtu yeyote aliyekuwa akimtawala mwenzake kwa ukatili. Andiko la Mwanzo 1:31 linasema: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.”

Katika visa fulani, masimulizi ya Biblia hayaonyeshi maoni ya Mungu kuhusu jambo fulani. Huenda yakawa masimulizi ya kihistoria tu. Biblia inaposimulia Loti akiwapa watu wa Sodoma binti zake haitaji kama jambo hilo lilikuwa sawa kiadili au ikiwa lilikubaliwa na Mungu. *Mwanzo 19:6-8.

Kwa kweli, Mungu huchukia aina zote za dhuluma na kuwatendea wengine vibaya. (Kutoka 22:22; Kumbukumbu la Torati 27:19; Isaya 10:1, 2) Sheria ya Musa ilishutumu kulalwa kinguvu kwa wanawake na ukahaba. (Mambo ya Walawi 19:29; Kumbukumbu la Torati 22:23-29) Uzinzi ulikatazwa, na wote waliohusika waliuawa. (Mambo ya Walawi 20:10) Badala ya kuwabagua wanawake, Sheria iliwakweza na kuwalinda kutokana na dhuluma iliyoenea sana katika mataifa jirani. Mke Myahudi mwenye uwezo aliheshimiwa na kuthaminiwa sana. (Methali 31:10, 28-30) Waisraeli ndio waliopaswa kulaumiwa kwa sababu ya kukosa kufuata sheria ya Mungu ya kuwaheshimu wanawake, hayo hayakuwa mapenzi ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Mwishowe, Mungu alilihukumu na kuliadhibu taifa hilo kwa sababu ya kukataa kimakusudi kumtii.

Je, Ujitiisho Ni Ubaguzi?

Jamii yoyote inaweza kufanya kazi vizuri kukiwa tu na utaratibu. Hilo linahitaji kuwe na watu wenye mamlaka wa kusimamia mambo. Wenye mamlaka wasipokuwapo, kunakuwa na mvurugo. “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”—1 Wakorintho 14:33.

Mtume Paulo anasema hivi kuhusu mpango wa ukichwa katika familia: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Kila mtu, isipokuwa Mungu hujitiisha kwa mamlaka ya juu zaidi. Kwa sababu Yesu yuko chini ya mamlaka fulani, je, hilo linamaanisha kwamba anabaguliwa? La, hasha! Kwa sababu tu Maandiko yamewapa wanaume daraka la kuongoza kutaniko na familia, hilo halimaanishi kwamba wanawake wanabaguliwa. Ili familia na kutaniko lifanikiwe, wote, wanawake kwa wanaume wanahitaji kutimiza majukumu yao kwa upendo na heshima.—Waefeso 5:21-25, 28, 29, 33.

Sikuzote, Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima. Alikataa kufuata mapokeo na sheria zilizowabagua wanawake ambazo zilifundishwa na Mafarisayo. Alizungumza na wanawake wasio Wayahudi. (Mathayo 15:22-28; Yohana 4:7-9) Aliwafundisha wanawake. (Luka 10:38-42) Alitoa kanuni ambazo ziliwalinda wanawake wasiachwe. (Marko 10:11, 12) Labda jambo lisilo la kawaida ambalo Yesu alifanya katika siku zake lilikuwa kukubali wanawake wawe marafiki wake wa karibu. (Luka 8:1-3) Akiwa mtu aliyeonyesha sifa zote za Mungu kikamilifu, Yesu alionyesha kwamba watu wa jinsia zote wana thamani ileile machoni pa Mungu. Kwa kweli, wote, wanaume na wanawake walikuwa miongoni mwa Wakristo wa kwanza waliopokea zawadi ya roho takatifu. (Matendo 2:1-4, 17, 18) Wale ambao wametiwa mafuta na ambao wanatarajia kuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo, hawatakuwa na tofauti zozote za kijinsia wanapofufuliwa ili waishi mbinguni. (Wagalatia 3:28) Mtungaji wa Biblia, Yehova, hawabagui wanawake.

[Maelezo ya Chini]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tofauti na watu wengi wa siku zake, Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima