Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suluhisho Halisi kwa Umaskini

Suluhisho Halisi kwa Umaskini

Suluhisho Halisi kwa Umaskini

MAMIA ya mamilioni ya watu ulimwenguni pote hujitahidi kujiruzuku kila siku licha ya ufukara. Ni wazi kwamba wanadamu wanahitaji serikali yenye uadilifu na isiyo na ufisadi ambayo inatamani kubadili ukosefu wa haki uliopo. Pia serikali hiyo lazima iwe na uwezo wa kutimiza makusudio yake mazuri. Je, ni jambo linalopatana na akili kutazamia wanadamu watokeze serikali kama hiyo?

Historia inathibitisha ukweli wa onyo hili la Biblia: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” (Zaburi 146:3) Je, umeona kwamba mara nyingi kutumaini serikali au viongozi wa kibinadamu hukatisha tamaa? Hata hivyo, tunaweza kumtumaini nani mwingine?

Kwa kweli, mamilioni ya watu wameomba wapate serikali yenye uadilifu itakayobadili hali hiyo ya ukosefu wa haki. Labda wewe pia umetoa sala hii ya kielelezo ambayo Yesu alifundisha: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii; na utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu. Na usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.”—Mathayo 6:9-13.

Je, huo ndio Ufalme tunaohitaji? Je, ni wenye uadilifu na usio na ufisadi? Je, una uwezo wa kutosha kutimiza makusudio yake mazuri? Bila shaka, ndiyo! Mungu aliyeanzisha serikali hiyo, yaani, ‘Baba yetu aliye mbinguni,’ ni “Mungu mwadilifu na Mwokozi,” ambaye ni “mwadilifu katika kazi zake zote.” (Isaya 45:21; Danieli 9:14) Inasemekana hivi kumhusu: “Wewe umetakata sana usiweze kuona lililo baya,” kwa hiyo tunaweza kuwa na uhakika kwamba serikali yake haitakuwa na ufisadi kamwe. (Habakuki 1:13) Na kwa kuwa “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake,” tunajua kwamba anapendezwa na hali njema ya kila mwanadamu duniani bila kumbagua yeyote.—Matendo 10:34, 35; Waroma 2:11.

Tayari Umesimamishwa na Unatenda!

Ingawa Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu, itaongoza mambo duniani ili kutimiza makusudi ya Mungu. Hilo linatia ndani kuondoa serikali za wanadamu zisizo kamilifu na mahali pake pachukuliwe na serikali kamilifu ya Mungu. Ahadi hii inatolewa katika andiko la Danieli 2:44: “Katika siku za wafalme hao [serikali], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

Chini ya uongozi wa Ufalme huo, hatimaye mapenzi ya Mungu yatafanywa mbinguni na duniani pia. Inatia moyo sana kujua kwamba serikali hiyo inaweza kuondoa kabisa ukosefu wa usawa uliopo ambao umechangia pengo kubwa kati ya walio matajiri zaidi na maskini zaidi. Hakutakuwa tena na matajiri wachache na maskini wengi.

Inafurahisha sana kujua kwamba tayari serikali ya Mungu ya kimbingu imesimamishwa ili isuluhishe matatizo hayo milele. Kronolojia ya Biblia na matukio ya ulimwengu yanaonyesha wazi kwamba mwaka wa 1914 ndio wakati ambapo serikali ya Mungu ilisimamishwa mbinguni. * Hivyo, kwa karne moja hivi, imekuwa ikiweka msingi wa ulimwengu mpya wenye uadilifu.

Wale ambao wametambua kwamba Ufalme huo umesimamishwa na wanaotii mwongozo wake, hawana ubaguzi. Mashahidi wa Yehova wanahubiri karibu katika nchi zote. Raia wa nchi hizo, wawe ni matajiri au maskini wanapewa nafasi ya kujifunza jinsi wanavyoweza kupata uzima wa milele. (Yohana 17:3) Mashahidi wa Yehova hawaruhusu tofauti za kiuchumi ziamue daraka ambalo mtu atapewa katika makutaniko yao. Watu hawaheshimiwi kwa sababu ya mali zao. Badala yake, wanaheshimiwa kwa sababu ya sifa zao. Viwango vya kiroho huonwa kuwa muhimu zaidi kuliko viwango vya kimwili.

Je, ungependa kujua jinsi unavyoweza kuishi chini ya serikali hiyo yenye uadilifu? Basi anza kufanya uchunguzi leo. Jifunze jinsi unavyoweza kutazamia kuishi kwa shangwe wakati ambapo ulimwengu hautagawanywa tena na utajiri.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, ukurasa wa 95 hadi 107, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wote Ni Ndugu, Wawe Matajiri au Maskini

▪ Mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wengi wa Yehova huko Ulaya na Asia walihitaji chakula, mavazi, na makao. Mashahidi wa nchi nyingine walituma mavazi na chakula kingi sana kwa ndugu zao wa kiroho huko Ulaya, Ufilipino, na Japani. Mashahidi nchini Marekani na Kanada walitoa misaada ambayo ingetumwa nchini Austria, Chekoslovakia (ambayo sasa ni Jamhuri ya Cheki na Slovakia), Finland, Hungaria, Italia, Poland, Rumania, Ubelgiji, Ufaransa, Ugiriki, Uholanzi, Uingereza, na Ujerumani.

[Picha]

Marekani

Uswisi

Ujerumani

▪ Hivi karibuni zaidi, katika kiangazi cha 1994, kikundi cha wajitoleaji Mashahidi kutoka Ulaya walisafirisha upesi misaada ambayo ndugu na dada zao Wakristo walihitaji barani Afrika. Kambi na hospitali zilizopangwa vizuri zilijengwa kwa ajili ya wakimbizi wa Rwanda. Kiasi kikubwa sana cha nguo, blanketi, chakula, na vichapo vya Biblia kilitumwa ili kuwasaidia watu zaidi ya 7,000 walioathiriwa. Idadi hiyo ilikuwa karibu mara tatu ya idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Rwanda wakati huo.

▪ Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1996, vita vilizuka katika eneo la mashariki la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Mazao yaliharibiwa, maghala ya chakula yakaporwa, na misaada ikazuiwa isifike mahali ilipohitajiwa. Watu wengi wangeweza kupata mlo mmoja tu kwa siku, na hivyo walipatwa na utapiamlo na magonjwa. Mashahidi wa Yehova huko Ulaya walichukua hatua haraka. Kikundi cha kutoa msaada cha Mashahidi kilichotia ndani madaktari, walisafirishwa kwa ndege wakiwa na dawa na pesa. Kufikia Juni 1997, Mashahidi nchini Ubelgiji, Ufaransa, na Uswisi walikuwa wamechanga kilogramu 500 za dawa, tani 10 za biskuti zenye protini nyingi, tani 20 za vyakula vingine, tani 90 za nguo, jozi 18,500 za viatu, na blanketi 1,000. Vitu hivyo viligharimu karibu dola 1,000,000.

▪ Mbali na kutosheleza mahitaji ya kimwili, Mashahidi wa Yehova hupendezwa hata zaidi kuwasaidia watu kiroho. Hilo linaonyeshwa na tamaa yao ya kujenga Majumba ya Ufalme yanayotumiwa kama mahali pa kujifunzia Biblia. Iliripotiwa hivi mwaka wa 1997: “Kwa msaada wa akina ndugu kutoka nchi nyingine, Sosaiti [ya Mnara wa Mlinzi] imesaidia kujenga Majumba mapya ya Ufalme 413 na kurekebisha majumba mengine 727 katika muda wa miezi minne tu katika nchi 75.” Iliripotiwa hivi kufikia mwaka wa 2003: “Kati ya nchi za Ulaya ambazo zimenufaika na mpango wa kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi zenye uhitaji ni Rumania, ambako Majumba ya Ufalme 124 yamejengwa tangu Julai 2000. Kwa kutumia muundo uleule kwa ajili ya karibu Majumba yake yote ya Ufalme, Ukrainia ilijenga majumba 61 katika mwaka wa 2001, na mengine 76 katika mwaka wa 2002. Kwa msaada wa pesa zilizochangwa kwa ajili ya Hazina ya Majumba ya Ufalme, mamia ya Majumba ya Ufalme yamejengwa nchini Bulgaria, Kroatia, Makedonia, Moldova, Serbia na Montenegro, na Urusi.”

[Picha]

Bulgaria

Kroatia

Romania

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mjitoleaji akiwatunza wakimbizi wawili mayatima

[Hisani]

© Liba Taylor/Panos Pictures

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mashahidi wa Yehova wanaeneza ujumbe unaotoa tumaini

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ufalme wa Mungu utamaliza umaskini