Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Tufanye Arusi?

Je, Ni Lazima Tufanye Arusi?

Vijana Huuliza . . .

Je, Ni Lazima Tufanye Arusi?

“Mchumba wangu Cindy, ndiye aliyekuwa wa kwanza kutaja kwamba inawezekana kufunga ndoa kisiri bila kuwajulisha wengi kati ya marafiki na watu wetu wa ukoo. Baada ya kujadiliana, tulikata kauli kwamba kufanya hivyo kungeokoa wakati, kungepunguza shughuli, na hatungechoka sana.”—Allen. *

IWAPO una umri wa kutosha kufunga ndoa na una mpenzi, huenda ukavutiwa na wazo la kufunga ndoa kisiri bila kuwajulisha watu wengi. Nyakati nyingine, wachumba wanaweza kufikiria kutoroka na kufunga ndoa kisiri bila kuwajulisha hata wazazi wao. Ni kanuni gani zinazoweza kukusaidia kuamua?

Je, Kufuata Desturi Ndilo Jambo Muhimu Zaidi?

Ijapokuwa kufunga ndoa ni jambo la kawaida katika jamii nyingi, sherehe za arusi hutofautiana sana. Hangaiko kuu la Wakristo si kufuata kila desturi ya kwao wanapofanya arusi. (Waroma 12:2) Badala yake, lililo muhimu zaidi kwao ni kuwa na uchumba na ndoa inayomletea Yehova Mungu heshima.—1 Wakorintho 10:31.

Kwa kuwa ndoa inaheshimiwa, watu wengi hawapendi kufunga ndoa kisiri. Katika nchi nyingi, Mashahidi wengi wa Yehova hufunga ndoa kwenye Majumba ya Ufalme. * Baadaye, wanaweza kuwaalika watu wa familia na marafiki kwenye mlo na burudani. Sherehe hizo hazihitaji kuhusisha mambo mengi. Hata hivyo, tunakubali kwamba kupanga arusi ni jambo lenye kuchosha na lenye gharama. Kwa mfano, mara nyingi nchini Marekani sherehe za arusi hugharimu maelfu ya dola.

Ili kupunguza mfadhaiko na gharama, wachumba fulani wamechagua njia rahisi. Cindy anasema: “Tuliwaambia wazazi wetu kwamba hatutafanya arusi kupatana na desturi za kwetu kwa kuwa hatukutaka arusi yetu ihusishe mambo mengi wala gharama kubwa. Wazazi wangu walituhakikishia kwamba wanaelewa hali yetu nao wakakubaliana nasi. Walituunga mkono kabisa.” Lakini Allen, mchumba wa Cindy aliyetajwa mapema, alipowaeleza wazazi wake kuhusu mipango yao ya arusi, hawakuelewa sababu zao za kufanya uamuzi huo. Allen anasema: “Wazazi wangu walifikiri kwamba lilikuwa kosa lao. Walidhani tuliamua kufanya hivyo kwa sababu ya jambo fulani ambalo walikuwa wamefanya. Lakini haikuwa hivyo hata kidogo.”

Huenda wazazi wako pia wakavunjika moyo ukiamua kufanya arusi isiyohusisha mambo mengi, kwa kuwa huenda wanataka watu wengi iwezekanavyo washangilie pamoja nao pindi hiyo ya pekee. Lakini vipi ikiwa unafikiria kufunga ndoa bila hata kuwajulisha wazazi wako kwa kuwa unajua kwamba familia yenu itapinga mpango wako wa kufunga ndoa?

Fikiria Hisia za Familia Yenu

Wazazi wako wanaweza kupinga mpango wako kwa sababu wanaona kwamba hupaswi kufanya uamuzi mzito jinsi hiyo kwa kuwa ungali mchanga. Huenda wakahofu kuwa mapendezi yako yatabadilika kadiri unavyokomaa na kwamba muda si muda, utajutia uchaguzi wako wa mwenzi wa ndoa. Kwa upande mwingine, huenda wakaona kwamba una umri wa kutosha kufunga ndoa, lakini wakatambua udhaifu fulani wa mpenzi wako. Au wanaweza kukuzuia usifunge ndoa kwa kuwa mtu unayetaka kuoana naye si mwamini mwenzako.

Ikiwa wazazi wako ni Wakristo wa kweli, huenda wanahangaika kwa sababu fulani za Kimaandiko. Inafaa wakueleze mahangaiko yao. Bila shaka, Yehova angeona kuwa wamepuuza daraka lao na kwamba hawana upendo, ikiwa hawangekueleza mahangaiko yao. Ukiwasikiliza utanufaika.—Methali 13:1, 24.

Kwa mfano: Ikiwa unataka kununua nguo, yaelekea utawaomba watu wengine maoni yao ili ujue kama nguo hiyo inakufaa. Huenda usikubaliane nao kila mara, lakini bado utawatazamia marafiki wako wa karibu wakuambie iwapo wanafikiri kwamba nguo hiyo haikufai. Unafurahi wanapokupa maoni yao kwa kuwa yanaweza kukuzuia usipoteze pesa. Unapaswa kufurahi hata zaidi watu wako wa familia wakikupa maoni yao kuhusu yule unayetarajia kufunga ndoa naye. Unaweza kubadili au kutupa nguo uliyonunua, lakini Yehova anakutarajia uishi na mume au mke wako kwa maisha yako yote. (Mathayo 19:5, 6) Ukichagua mume au mke asiyefaana sana na utu wako au hali yako ya kiroho, utataabika zaidi katika ndoa kuliko jinsi ambavyo ungetaabika ukivaa nguo isiyokufaa. (Mwanzo 2:18; Methali 21:9) Pia, kwa kufanya hivyo, huenda ukapoteza nafasi ya kupata furaha ya kweli. —Methali 5:18; 18:22.

Ni kweli kwamba huenda wazazi fulani wakapinga ndoa kwa sababu za ubinafsi. Kwa mfano, wanaweza kufanya hivyo ili waendelee kumdhibiti mtoto wao. Hata hivyo, kwa nini usiyachunguze maoni ya wazazi wako kabla hujayatupilia mbali ukidai kwamba ni ya ubinafsi, na kukimbilia kufunga ndoa?

Kwa Nini Ujihadhari?

Bila shaka mapendezi yako yatabadilika kadiri unavyokomaa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Hali kadhalika, mambo yanayokuvutia kumhusu mtu mwingine ukiwa kijana yanaweza kutofautiana sana na yale yatakayokuvutia utakapokuwa na umri mkubwa zaidi. Ndiyo sababu Biblia hupendekeza ungoje hadi uwe “umepita upeo wa ujana,” yaani, ile miaka unapokuwa na tamaa kubwa ya ngono, ndipo uchukue hatua hiyo nzito ya kuchagua mume au mke.—1 Wakorintho 7:36.

Vipi wazazi wako wakimchambua mpenzi wako? Kwa kuwa wazazi wako wamejionea mambo mengi maishani, nguvu zao za ufahamu zinaweza kuwa zimezoezwa vizuri zaidi kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia. (Waebrania 5:14) Hivyo, wanaweza kuona udhaifu fulani mkubwa wa mtu unayetaka kufunga ndoa naye hata ikiwa wewe huuoni. Fikiria kanuni iliyo katika maneno haya yaliyoandikwa na Sulemani mwenye hekima: “Mtu wa kwanza katika kesi yake ni mwadilifu; mwenzake huingia naye hakika humchunguza kwa undani.” (Methali 18:17) Vivyo hivyo, huenda mpenzi wako amekusadikisha kwamba yeye tu ndiye anayekufaa. Hata hivyo, baada ya wazazi wako ‘kumchunguza,’ huenda wakataja mambo fulani yanayofaa kufikiriwa.

Kwa mfano, huenda wakakukumbusha kwa uthabiti kwamba Biblia inawaagiza Wakristo waoe au waolewe “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Unaweza kubisha kwamba unajua watu fulani ambao hawakufunga ndoa na waamini wenzao, lakini ambao sasa wanamtumikia Yehova kwa furaha pamoja na wenzi wao. Ni kweli kwamba kuna visa kama hivyo. Hata hivyo, vinatukia mara chache sana. Ukifunga ndoa na mtu asiyeamini, hutapuuza tu viwango vya Yehova, bali pia utajihatarisha sana kiroho.—2 Wakorintho 6:14. *

Kufunga Ndoa kwa Sababu Isiyofaa

Vijana fulani hutoroka na kufunga ndoa kwa sababu walijihusisha katika ukosefu wa adili na kufikiri kwamba wakioana dhamiri itaacha kuwasumbua. Au huenda wakafanya hivyo ili kujaribu kufunika matokeo ya dhambi yao, kama vile mimba ambayo haikukusudiwa.

Ikiwa ungefunga ndoa ili ufunike dhambi yaelekea ungezidisha tatizo. Sulemani alionya hivi: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Methali 28:13) Baba na mama ya Sulemani, Daudi na Bathsheba, walitambua ubatili wa kujaribu kuficha dhambi yao. (2 Samweli 11:2–12:25) Badala ya kuficha dhambi, waeleze wazazi wako na wazee wa kutaniko. Utahitaji ujasiri, lakini uwe na hakika kwamba ukitubu, Yehova atakusamehe. (Isaya 1:18) Ukiisha kupata tena dhamiri njema, utakuwa na uwezo wa kufanya uamuzi mzuri kuhusu ndoa.

Epuka Majuto

Allen anasema hivi anapokumbuka arusi yao: “Kufanya arusi isiyohusisha mambo mengi kulifanya tusihangaike sana. Nasikitika tu kwamba sikuweza kuwasaidia watu wa familia yetu waelewe vizuri kwa nini tulifanya uamuzi huo.”

Kwa kweli, uamuzi wa kufanya au kutofanya arusi kupatana na desturi za mahali ni wa mtu binafsi. Hata hivyo, unapofanya uamuzi wowote kuhusu ndoa, usiharakishe, zungumza na familia yenu kuhusu jambo hilo, na ‘uzifikirie hatua zako.’ Ukifanya hivyo, utaepuka majuto.—Methali 14:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 7 Majumba hayo ya ibada hufaa sana kwa ajili ya arusi za Mashahidi wa Yehova. Arusi hizo hazihusishi mambo mengi. Katika pindi hiyo, kanuni za Biblia ambazo ndizo msingi wa ndoa yenye mafanikio huzungumziwa. Hakuna malipo yoyote wanayotozwa wanapotumia Jumba la Ufalme kwa ajili ya arusi.

^ fu. 18 Unaweza kupata habari zaidi katika Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2004, ukurasa wa 30-31, na Novemba 1, 1989, ukurasa wa 18-22.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Zungumza na familia yenu unapotaka kufanya uamuzi wowote kuhusu kufunga ndoa