Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Mfadhaiko Mfululizo wa makala, “Kukabiliana na Mfadhaiko,” ulinifaa sana! (Februari 8, 2005) Nilipokea makala hizo nilipokuwa karibu kuchanganyikiwa kabisa kwa sababu ya matatizo ya kihisia. Sikuwa nikipambana ifaavyo na mfadhaiko. Mapendekezo katika makala hizo yamenisaidia sana.

Jina limebanwa, Marekani

Madaktari waligundua hivi majuzi kwamba ninaugua ugonjwa wa kushuka moyo. Kwa hiyo, maneno, “Inafaa kushughulikia mahitaji yako,” yalinitia moyo. Nilithamini mfano unaohusisha kuhifadhi nguvu kana kwamba unaziweka “akiba katika benki.” Nilikuwa nimeishiwa na nguvu za kihisia, lakini kuanzia leo nitajitahidi kujua mipaka yangu.

Y. O., Japani

Nimerudi sasa hivi kutoka katika mkutano fulani kuhusu jinsi ya kushughulikia mfadhaiko. Nilitoa hotuba fupi kwenye mkutano huo, na nilitaja visababishi vya mfadhaiko na athari zake, na vilevile masuluhisho. Nilipata habari zote katika gazeti hili zuri sana!

J. L., Ujerumani

Simu za Mkononi Asanteni kwa makala “Je, Simu za Mkononi Zina Faida au Hasara?” (Februari 8, 2005) Nina umri wa miaka 14, na nilikuwa nimezoea mno simu yangu ya mkononi. Makala hiyo ilinisaidia kuelewa kwamba simu hiyo haipaswi kuwa kitu muhimu zaidi maishani mwangu, hasa kwa sababu inaweza kuathiri afya. Asanteni kwa makala zenye kupendeza.

M. B., Rumania

Sili wa Harp Ninathamini sana makala za Amkeni! zenye kufurahisha na kuelimisha. Baada ya kusoma makala, “Watoto wa Sili wa Visiwa vya Magdalen,” nilianza kuwapenda wanyama hao wazuri. (Januari 8, 2005) Picha zilinisaidia kuelewa jinsi wanyama hao wanavyokua. Mbali na kunisukuma nimshukuru Yehova aliyewaumba wanyama hao, makala hiyo iliimarisha tamaa yangu ya kuishi katika Paradiso. Nimekuwa na matatizo mazito sana, na siwezi kusema jinsi makala hiyo ilivyonitia moyo. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala kama hizo.

N. S., Japani

Farasi wa Baharini Mashahidi wa Yehova walinipa gazeti lenu, na ningependa kuwashukuru kwa makala “Farasi Wanaocheza Dansi Baharini.” (Desemba 22, 2004) Nilipata maksi nzuri sana nilipoandika insha kuwahusu farasi wa baharini kwa kutumia habari katika makala hiyo. Nimejifunza mengi kuhusu sayansi na teknolojia katika gazeti la Amkeni!, na hasa kumhusu Mungu. Asanteni Mashahidi wa Yehova kwa magazeti yenu mazuri!

T. P., Indonesia

Imeandikwa . . . Ninafurahi sana kwamba nilisoma makala “Imeandikwa Kwamba Nitamwona”! (Desemba 22, 2004) Nina miaka 11 na hadi leo nimekosa ujasiri wa kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Lakini baada ya kusoma simulizi la maisha ya Rosalía Phillips nimejua kwamba Yehova atanisaidia. Ninataka kuwa mhubiri jasiri wa habari njema kama Rosalía.

P. P., Poland

Nina miaka 27, na mama yangu alikufa miaka 24 iliyopita. Tangu niwe Shahidi wa Yehova, nimekuwa na tumaini thabiti la kumwona tena. Ninamshukuru Yehova na wachapishaji wa Amkeni! kwa kutuandalia makala kama hizo, na ninamshukuru Rosalía kwa kutueleza kuhusu maisha yake.

A. F., Venezuela