Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sayansi na Biblia Zilinisaidia Kupata Kusudi la Uhai

Sayansi na Biblia Zilinisaidia Kupata Kusudi la Uhai

Sayansi na Biblia Zilinisaidia Kupata Kusudi la Uhai

SIMULIZI LA BERND OELSCHLÄGEL

Nilitafuta kusudi la uhai kwa miaka 20. Mambo mawili yalinisaidia kulipata: sayansi na Biblia. Nilipojifunza sayansi nilikuwa na uhakika kwamba lazima uhai uwe na kusudi. Lakini Biblia ilifunua kusudi hilo na kunisaidia kulielewa.

HUENDA umewasikia watu fulani wakisema kwamba sayansi hupingana na Biblia. Nimejifunza zote mbili na sikubaliani na dai lao. Labda ungependa kujua sababu yangu.

Nilizaliwa mnamo 1962 huko Stuttgart, jiji lililoko Ujerumani kusini. Baba alifanya kazi ya kubuni mashini, na yeye na Mama walijihusisha sana na utendaji wa kanisa. Karin, dada yangu, alizaliwa miaka minne kabla yangu. Jambo moja muhimu lililotokea nilipokuwa mtoto lilikuwa kupewa vifaa vya sayansi vya kuchezea na Baba. Nilifurahia sana kujaribu mambo fulani ya msingi ya kemia na fizikia. Naam, nilifurahia kujifunza.

Baadaye niliacha kutumia vifaa hivyo vya kuchezea na nikaanza kutumia kompyuta. Hata nilipokuwa tineja nilitambua kwamba ubongo ndio uliokuwa kompyuta bora zaidi. Lakini nilijiuliza: ‘Ubongo unatoka wapi? Ni nani aliyetupa? Na kusudi la uhai ni nini?’

Kufuatia Elimu ya Juu

Niliacha shule nilipokuwa na umri wa miaka 16 na nikaanza kujifunza kazi nikiwa msaidizi katika duka la kusafisha picha. Kwa kuwa nilifurahia zaidi kujifunza, mradi wangu ulikuwa kujifunza fizikia katika chuo kikuu. Lakini ingechukua muda mrefu kabla ya kuanza masomo katika chuo kikuu. Ilinichukua miaka mitano kutimiza matakwa ya kustahili kuingia chuoni. Nilianza elimu yangu ya chuo kikuu huko Stuttgart mnamo 1983, na nikaendelea na masomo yangu huko Munich. Mwishowe, nilipata shahada ya juu kabisa katika fizikia kwenye Chuo Kikuu cha Augsburg mnamo 1993.

Mambo hayakuwa rahisi nilipoanza masomo yangu katika chuo kikuu. Kwa kawaida, jumba la mihadhara lilikuwa na wanafunzi 250 hivi, na wengi wao waliacha masomo hayo baada ya miezi michache. Nilikuwa nimeazimia sitavunjika moyo bali nitatimiza jambo nililoanza. Kwa kuwa niliishi katika bweni, nilishirikiana na wengi waliopenda hasa kuponda raha. Sikufaidika kwa kushirikiana na watu kama hao. Kwa sababu hiyo, nilianza kwenda karamu zisizo na maadili na kutumia dawa za kulevya.

Naelekea India Kutafuta Majibu

Nilipojifunza fizikia nilifahamu kwa undani sheria za asili za ulimwengu. Nilitumaini kwamba sayansi ingenifunulia kusudi la uhai. Hata hivyo, maswali yangu kuhusu kusudi la uhai hayangeweza kujibiwa na fizikia. Mnamo 1991, nilisafiri pamoja na kikundi fulani hadi India ili kujifunza kutafakari kama watu wa Mashariki. Ilipendeza sana kujionea nchi hiyo na watu wake! Lakini nilishangazwa na tofauti kati ya matajiri na maskini.

Kwa mfano, karibu na jiji la Pune, tulimtembelea mwalimu mmoja wa dini ya Kihindu ambaye alidai kwamba kutafakari kwa njia zinazofaa kungeweza kumsaidia mtu awe tajiri. Tulitafakari kila asubuhi tukiwa kikundi. Mwalimu huyo pia aliuza dawa kwa bei ya juu. Maisha yake yalionyesha wazi kwamba alikuwa anachuma pesa nyingi. Pia tuliwaona watawa ambao walionekana kuwa maskini, tofauti na huyo mwalimu. Nilijiuliza, ‘Kwa nini kutafakari hakukuwatajirisha wao pia?’ Ni kana kwamba safari yangu huko India ilitokeza maswali mengi zaidi kuliko majibu.

Mojawapo ya vitu nilivyorudi navyo kutoka India ilikuwa kengele ya kutafakari. Niliambiwa kwamba kengele hiyo inapogongwa vizuri inatoa sauti fulani ya muziki ambayo ingenisaidia kutafakari kwa njia nzuri. Niliporudi Ujerumani nilinunua kifaa cha kusoma habari za nyota kilichochorwa na mtu aliyedai kuwa na uwezo wa kujua wakati wangu ujao. Lakini kutafakari hakukunifunulia jambo lolote kuhusu uhai. Nilihuzunika sana kugundua kwamba kifaa hicho cha kusomea habari za nyota kilikuwa kijikaratasi ovyo tu. Kwa hiyo, bado maswali yangu kuhusu kusudi la uhai hayakujibiwa.

Nilipata Majibu Katika Biblia

Maisha yangu yalibadilika ghafula mwaka wa 1993. Nilikuwa nimemaliza masomo na utafiti wangu na nilikuwa nikiendelea kuandika insha fulani ya fizikia ili kupata shahada ya juu. Ili niimalize kwa wakati uliowekwa, nilifanya kazi karibu usiku na mchana bila kufanya jambo jingine. Kisha alasiri moja mlango wangu ukabishwa. Nilipoufungua, niliona wanawake wawili.

“Je, ulijua kwamba mwaka wa 1914 ulikuwa mwaka muhimu sana kulingana na Biblia?” wakaniuliza. Swali hilo lilinishangaza. Sikuwa nimewahi kusikia jambo kama hilo; wala sikuwa na wakati wa kufanya uchunguzi. Hata hivyo, nilivutiwa na swali hilo. Wangewezaje kudai eti Biblia ilitabiri zamani za kale kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa mwaka muhimu?

“Je, ungependa kujua zaidi?” wakauliza. Niliwaza hivi: ‘Bila shaka, nikiwasikiliza, nitapata jambo fulani linalojipinga katika hoja zao.’ Badala ya kujipinga, nilipata uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Biblia ni yenye kutegemeka. Nilijifunza kwamba unabii wa Biblia unaonyesha wazi kwamba Ufalme wa Kimasihi wa Mungu, yaani, serikali ya kimbingu ambayo wakati fulani itatawala juu ya dunia yote, ilisimamishwa mwaka wa 1914. *

Wanawake hao walikuwa Mashahidi wa Yehova, nao walinipa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. * Nilimaliza kukisoma baada ya siku chache na nikaona kuwa mambo yote yaliyoandikwa humo yanapatana na akili na yameandikwa kwa njia yenye usawaziko. Mashahidi walinionyesha kutoka katika Biblia kwamba ni mapenzi ya Yehova kwamba wanadamu waishi milele katika paradiso duniani. Kulingana na unabii wa Biblia, ahadi hiyo itatimizwa hivi karibuni. Hilo ni tumaini zuri ajabu la wakati ujao! Tumaini hilo lilinigusa moyo na kunifanya nitokwe na machozi. Je, hili ndilo jambo nililokuwa nikitafuta kwa miaka 20 iliyopita?

Nilitambua haraka kusudi langu la kuwa hai: kumjua Yehova Mungu na kumtumikia kwa moyo wote. Niliendelea kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, kwani nilihisi kwamba mambo niliyokuwa nikijifunza yalikuwa kweli. Kiu yangu ya mambo ya kiroho haingeweza kutoshelezwa. Nilipokuwa nikiandika insha yangu kuhusu mambo ya sayansi, nilisoma nusu ya Biblia kwa miezi mitatu.

Kupata Mengi Zaidi ya Majibu Tu

Mnamo Mei 1993, nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme huko Augsburg. Mafundisho niliyosikia huko yalisikika kuwa kweli. Isitoshe, nilijihisi nikiwa nimetulia nilipokuwa na Mashahidi. Walinisalimu kwa uchangamfu na kunifanya nitulie, ingawa nilikuwa mgeni. Mwanamke mmoja mzee aliketi karibu nami naye alijitahidi kunitafutia kitabu cha wimbo. Majuma yaliyofuata, mwanamume mmoja Shahidi pamoja na mwana wake mchanga walinibeba kwa gari lao hadi kwenye Jumba la Ufalme. Marafiki hawa wapya walianza kunikaribisha kwenye nyumba zao. Baada ya muda, nilitamani kuwaeleza wengine yale niliyokuwa nikijifunza kuhusu kusudi la uhai.

Kufuata kwa uangalifu yale niliyokuwa nikijifunza kutoka katika Biblia kulinichochea kufanya mabadiliko maishani. Kwa mfano, sikutaka tena kuweka vitu vilivyohusiana na uchawi. Kwa hiyo, niliharibu kifaa changu cha kusoma habari za nyota pamoja na ile kengele ya kutafakari na vitu vingine vya kidini nilivyokuwa nimetoa India. Nilifanya maendeleo katika funzo langu la Biblia, nikajiweka wakfu kwa Yehova Mungu, na kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova huko Munich mnamo Juni 1994. Kwa kufanya hivyo nilikubali kwa moyo wote kusudi halisi la uhai.

Mnamo Septemba 1995, nilikuwa painia wa kawaida, mtumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Hilo lilimaanisha kutumia wakati mwingi zaidi kuzungumza na watu kuhusu makusudi ya Mungu. Ili kufanya hivyo nilitegemea nguvu za Yehova. Mara nyingi nilirudi nyumbani jioni baada ya kutumia saa kadhaa katika utumishi, nikiwa na shangwe na uradhi ambao sikuwa nimepata kabla ya kumjua Yehova. Mnamo Januari 1997, nilialikwa nitumikie katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani iliyoko Selters, inayoitwa Betheli, na huko ndiko ninaishi sasa. Wazazi wangu wamenitembelea mara kadhaa, na ingawa imani yao ni tofauti na yangu, siku hizi wao huheshimu Betheli na wanafurahi kwamba niko huko.

Sayansi na Biblia

Huenda wengine wakajiuliza, mtu ambaye amejifunza sayansi kwa miaka mingi anawezaje kuamini yale ambayo Biblia husema. Kwa maoni yangu, sayansi na Biblia hazipingani. Nikiwa mwanafizikia, nimejifunza sheria zinazoongoza uhai, na sheria hizo hutoa uthibitisho kwamba zimebuniwa na Mtu mwenye akili nyingi zaidi kuliko ya mwanadamu.

Kwa mfano, kuna nadharia nyingi katika fizikia, kemia, na biolojia. Ingawa nadharia hizo zinaweza kuwa rahisi, huenda hesabu inayohusika ikawa ngumu sana. Wanasayansi wenye akili nyingi hupendekeza nadharia fulani nao hupewa Tuzo ya Nobeli kwa kazi yao. Basi lazima iwe kwamba Mtu mwenye akili nyingi sana ndiye aliyebuni na kutokeza ulimwengu, ambao hata unawatatanisha wanasayansi.

Kudokeza eti uhai ulijitokeza wenyewe, kama wanasayansi wasemavyo, si jambo linalopatana na akili. Kwa kielelezo: Panga mipira kumi katika mstari mmoja kwenye uwanja wa mpira, kila mpira ukiwa umbali wa meta moja kutoka kwa mwingine. Piga mpira wa kwanza na ujaribu kufanya mipira yote kumi igongane kwa mfululizo. Isitoshe, jaribu kutabiri mahali ambapo kila mpira utasimama. Uwezekano wa kufaulu ni mdogo sana hivi kwamba watu wengi wanaweza kusema kwamba jambo hilo haliwezekani.

Ikiwa ndivyo, mtu anaweza kusemaje kwamba chembe za mwanadamu zilijitokeza zenyewe, ilhali kuzitokeza kunahitaji ustadi wa hali ya juu kuliko tu kupiga mipira? Jibu linalopatana na akili ni kwamba wanadamu na viumbe vingine vyote duniani viliumbwa na Mtu mwenye akili nyingi sana kuliko mwanadamu. Je, Mtu huyo, ambaye ndiye Muumba, angefanya jambo kama hilo bila kuwa na kusudi? Sivyo hata kidogo. Lazima awe na kusudi, na kusudi hilo limefunuliwa na kuelezwa katika Biblia.

Kama uonavyo, sayansi na Biblia zilinisaidia kupata majibu ya maswali yangu ya muda mrefu kuhusu uhai. Je, unaweza kuwazia utulivu na furaha ya kupata kitu ulichotafuta kwa zaidi ya miaka 20? Ni tamaa yangu ya moyoni kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo wapate nilichopata mwishowe, yaani, majibu kwa maswali yangu, na jambo muhimu hata zaidi, wapate njia inayofaa ya kumtumikia Mungu wa pekee wa kweli, Yehova!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kwa maelezo zaidi kuhusu habari hii, ona sura ya 10, “Ufalme wa Mungu Watawala,” katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 90 hadi 97.

^ fu. 18 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Sasa hakichapishwi tena.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Nikiwa mwanafizikia, nimejifunza sheria zinazoongoza uhai, na sheria hizo hutoa uthibitisho kwamba zimebuniwa na Mtu mwenye akili nyingi zaidi kuliko ya mwanadamu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilipokuwa na umri wa miaka 12

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nilipokuwa nikitafuta kusudi la uhai, nilianza kutafakari kama watu wa Mashariki

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mimi hupata shangwe ya kweli na uradhi kwa kuwahubiria wengine

[Hisani]

Cover of book: J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA