Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Usio na Njaa

Ulimwengu Usio na Njaa

Ulimwengu Usio na Njaa

HEBU wazia jinsi ambavyo baba anayejali huhisi anapoona watoto wake wakiwa na utapiamlo. Hilo humuumiza sana. Ikiwa hivyo ndivyo mzazi wa kibinadamu huhisi, fikiria jinsi Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo huhisi. Anajua kwamba mamia ya mamilioni ya watu wanateseka.

Licha ya jitihada zinazofanywa na wanadamu kwa nia nzuri za kuwaandalia chakula watu wenye njaa ulimwenguni, bado njaa inaongezeka mwanzoni mwa karne hii ya 21. Hata hivyo, Baba yetu wa kimbingu, Yehova anaweza, naye atamaliza njaa milele. Tunajuaje?

Biblia inaeleza kwamba wakati Mungu alipowaweka Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni, aliwaandalia kila kitu walichohitaji ili wawe salama, wawe na uradhi, na chakula cha kutosha. Mungu aliwaambia hivi: “Nimewapa mimea yote inayozaa mbegu iliyo juu ya uso wa dunia yote.” Yehova alikusudia watoto wa Adamu na Hawa ‘waijaze dunia’ na wanadamu wote wawe na vyakula vingi vyenye kupendeza.—Mwanzo 1:28, 29.

Ingawa wanadamu wawili wa kwanza walimwasi Muumba wao na kupoteza kibali chake, kusudi la Mungu la awali kwa wanadamu halijabadilika. Biblia inamtaja Yehova kuwa “Yeye anayewapa wenye njaa mkate,” na ina unabii mwingi unaoonyesha kwamba ataondoa matatizo yote yanayohusiana na kupata chakula.—Zaburi 146:7.

Wanafunzi wa Yesu walipomwomba ishara, au uthibitisho wa kuonyesha wakati ambapo atausimamisha Ufalme wake na kuingilia mambo duniani, Yesu aliorodhesha mambo ambayo yangetukia kabla ya yeye kufanya hivyo. Mojawapo ya mambo hayo ni “upungufu wa chakula.” Kuchunguza kwa makini maneno Yesu kunatuhakikishia kwamba kuteseka kwa wanadamu kutakwisha hivi karibuni. *Mathayo, sura ya 24.

Zaburi 72:16 inatabiri hivi kuhusu Paradiso ambayo Mungu anaahidi: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” Katika Israeli la kale, kwa kawaida nafaka ilikua kwenye mabonde. Hata hivyo, katika hali nzuri zinazotajwa katika unabii huo, mbegu inayopandwa hata katika ardhi isiyozaa, iliyo kame, na isiyo na rutuba, yaani, ardhi ambayo kwa kawaida haingetokeza chochote, itazaa kwa wingi. Msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Wakati wa Masihi, itakuwa kana kwamba kuna mashamba mazuri ya nafaka kila mahali, hata juu ya milima, au ni kana kwamba nafaka zimepandwa hadi kwenye vilele vya milima, hivi kwamba ardhi yote itafunikwa na mazao manono yenye kupendeza.”

Kutakuwa na tofauti kubwa sana kati ya wakati ujao ambao Biblia inatabiri na maisha ya mamilioni ya watu leo! Naam, bila shaka, Mungu anaahidi kwamba wakati ujao, “dunia itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.”—Zaburi 67:6.

Ikiwa ungependa kujua jinsi wewe na wapendwa wako mnavyoweza kufurahia baraka hizo na nyingine nyingi zinazotajwa katika unabii wa Biblia wenye kuchangamsha, usisite kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo unaloishi au kuwaandikia barua kwa kutumia anwani inayofaa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kuona jinsi ambavyo unabii wa Yesu umetimizwa, ona sura ya 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 10]