Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Hupendelea Mataifa Fulani?

Je, Mungu Hupendelea Mataifa Fulani?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Hupendelea Mataifa Fulani?

WATU wengi huhisi kwamba Mungu hupendelea taifa lao kuliko mataifa mengine. Lakini wakiulizwa watoe uthibitisho, watasema nini? Huenda wengine wakataja mambo ambayo taifa lao limetimiza, kama vile ushindi wa kijeshi au ukuzi wa kiuchumi. Huenda hata wakataja miradi iliyofanikiwa ambayo imekusudiwa kulisha wenye njaa, kulinda maskini, au kutetea haki na usawa. Wengine hukata kauli kwamba Mungu anapendelea nchi yao kwa sababu ni maridadi.

Katika nchi zote watu hujivunia taifa lao. Lakini, je, Biblia inaunga mkono wazo la kwamba Mungu hupendelea mataifa fulani?

Sifa Muhimu ya Mungu

Jibu ni wazi ikiwa tunaelewa sifa fulani muhimu ya Mungu Mweza Yote, ambayo inakaziwa katika Biblia. Mungu hana ubaguzi. Kwa mfano, andiko la Matendo 10:34 linasema hivi waziwazi: “Mungu hana ubaguzi.” Pia Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ‘hamtendei yeyote kwa upendeleo’ na kwamba “hakuna ukosefu wowote wa uadilifu wala ubaguzi . . . kwa upande wa Yehova Mungu wetu.” (Kumbukumbu la Torati 10:17; 2 Mambo ya Nyakati 19:7) Mungu anachukia ubaguzi; hata anaulinganisha na ukosefu wa uadilifu.

Hata hivyo, huenda ukajiuliza: ‘Je, Mungu hakupendelea taifa la Israeli la kale? Je, huo haukuwa ubaguzi?’ Kwa kweli, Mungu alichagua taifa la Israeli katika nyakati za Biblia, na mara kwa mara aliwalinda Waisraeli walipopigana na mataifa mengine. Isitoshe, Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Anamtangazia Yakobo neno lake, na Israeli masharti yake na maamuzi yake ya hukumu. Hajafanya hivyo kwa taifa lingine lolote.” (Zaburi 147:19, 20) Lakini je, jinsi ambavyo Mungu alishughulika na Waisraeli inaonyesha kwamba alikuwa na ubaguzi? La. Fikiria sababu tatu.

Kwanza, Mungu alichagua Israeli ili anufaishe mataifa yote. Alifanya agano na babu wa taifa hilo, Abrahamu, akisema: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.” (Mwanzo 22:17, 18) Naam, kusudi la Mungu katika kushughulika na Israeli lilikuwa kutokeza “uzao” ambao ungeleta baraka nyingi, si kwa watu wa taifa moja tu bali kwa watu wa “mataifa yote ya dunia.”

Pili, si Waisraeli peke yao waliopata baraka za Mungu. Alifanya iwezekane kwa watu wa mataifa mengine wajiunge na watu wake wateule kumwabudu. (2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33) Wengi walikubali mwaliko huo na wakabarikiwa. Ruthu, mwanamke Mmoabu alikuwa mmoja wa watu hao.—Ruthu 1:3, 16.

Tatu, uhusiano wa kipekee kati ya Mungu na Israeli wa kidunia ulikuwa wa muda. Mnamo mwaka wa 29 W.K., Israeli lilitokeza “uzao” ulioahidiwa kupitia Masihi, Yesu Kristo. (Wagalatia 3:16) Lakini watu wa taifa la Yesu walimkataa kuwa Masihi. Aliwaambia hivi: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38) Baada ya hapo, Mungu amekuwa akijishughulisha na wanadamu katika njia tofauti sana bila kujihusisha na vita vyao. Amefanya iwezekane kwa wanadamu wote kupata baraka. Fikiria mifano kadhaa.

Zawadi ya Mungu kwa Watu Wote

Dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ndiyo zawadi kubwa zaidi ambayo Mungu amewapa wanadamu. (Waroma 6:23) Imefanya watu wawe huru kutokana na dhambi na kifo, na kutupa sote fursa ya kupata uzima wa milele. Zawadi hiyo ni kwa ajili ya watu “kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.” (Ufunuo 5:9) Naam, Mungu anataka “kila mtu anayemwamini” Yesu apate “uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Habari njema ya Ufalme wa Mungu huleta baraka kwa wote wanaosikiliza. (Ufunuo 14:6, 7) Inatoa tumaini kwa ajili ya wakati ujao na shauri linaloweza kumfanya mtu aishi maisha yenye furaha sasa. Bila kubagua, Yehova amepanga ‘hii habari njema ya ufalme ihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 16:10) Habari njema hiyo iko katika Biblia, kitabu ambacho kinaweza kupatikana angalau kwa sehemu, katika lugha zaidi ya 2,300. Akiwa Baba mwenye upendo, Yehova amefanya iwezekane kwa karibu kila mtu duniani kupata “maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:68; Yoshua 1:8.

Zawadi hizo na nyingine kutoka kwa Mungu zinapatikana kwa watu wote, naam, kwa watu wa mataifa, jamii, na lugha zote. Kwa hiyo, kupata kibali na baraka za Mungu hakutegemei mahali tulipozaliwa au kabila letu.

Ni Nani Walio na Kibali cha Mungu?

Hivyo basi, tunahitaji kufanya nini ili tupate kibali cha Mungu? Mtume Petro anajibu kwa kusema: “Katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Bila shaka, haitoshi tu kupendezwa na Mungu bila kuchukua hatua yoyote. Tunahitaji kumpenda Mungu kikweli, na kuogopa kumchukiza. Pia tunahitaji “kutenda uadilifu,” au kujitahidi kufanya mema machoni pa Mungu.

Kwa mfano: Katika nchi nyingi, kuna shule nyingi za umma, lakini wale tu wanaoenda shuleni na kujitahidi ndio watakaonufaika. Vivyo hivyo, watu wote wanaweza kupata kibali cha Mungu, lakini jitihada inahitajiwa. Jitihada hiyo inatia ndani kusoma Biblia kwa ukawaida, kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, na kuishi kupatana na kanuni za Biblia. ‘Tukimtafuta Yehova’ kikweli, tutajikuta katika njia itakayofanya tupate kibali chake.—Zaburi 105:3, 4; Methali 2:2-9.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mungu amefanya iwezekane kwa watu wa mataifa yote kupata “maneno ya uzima wa milele”