Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Karibu Katika Tengenezo la Yehova”

“Karibu Katika Tengenezo la Yehova”

“Karibu Katika Tengenezo la Yehova”

Familia moja nchini Finland, ambayo ilikuwa imeshirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa muda fulani ilipatwa na upinzani kutoka sehemu mbalimbali. Watu waliwaonya hivi: “Watachukua pesa zenu.” Wengine wakasema, “Mtapoteza makao yenu.” Bila kutarajiwa, usiku mmoja moto uliharibu kabisa sehemu ya nyumba ya familia hiyo iliyokuwa na mfumo wa kupasha joto, ambao ndicho kitu muhimu zaidi katika eneo la kaskazini lenye baridi kali.

Bima yao haingeweza kulipia kabisa gharama za kununua vifaa vya kujenga upya nyumba yao. Ilionekana ni kama moto huo ulithibitisha matabiri yaliyokuwa yametolewa. Baba wa familia hiyo anakumbuka hivi kwa huzuni, “Tulihisi tumeshuka moyo kwelikweli.” Hata hivyo, wenzi hao wa ndoa hawakubadili mipango yao ya kubatizwa majuma matatu baadaye.

Kutaniko lao liliona hiyo kuwa nafasi ya kufuata shauri hili la Biblia: “Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:18) Washiriki wa kutaniko walianza mipango ya kurekebisha jengo hilo. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Finland ilitoa mashauri yanayofaa kuhusu jinsi ya kushughulikia jambo hilo. Ramani za ujenzi zilichorwa, leseni za kujenga zikapatikana, orodha ya vifaa vilivyohitajika ikaandikwa, na ombi la kupata wajitoleaji likatolewa.

Mwezi mmoja hivi baada ya moto huo, kazi ilianza. Jumatano moja, Mashahidi wa eneo hilo walibomoa sehemu iliyokuwa imeteketezwa. Kufikia Ijumaa, kwa msaada wa Mashahidi kutoka makutaniko mengine, jengo hilo jipya lilianza kuonekana. Aliposafiri hadi mjini, baba wa familia hiyo alikutana na ofisa wa eneo hilo ambaye alitaka kujua ikiwa alikuwa ameweka chandarua juu ya paa ili jengo hilo lililoharibiwa lisiingie mvua. “La, hakuna chandarua,” baba huyo alimjibu kwa furaha, “lakini kuna wanaume 30 juu ya paa!”

Jumamosi akina ndugu na dada 50 hivi wa kiroho walifika, wakiwa na shangwe kwa sababu ya kushiriki katika kazi hiyo. Jirani mmoja, ambaye alisaidia alisema hivi: “Jana usiku nilifikiria kwa muda fulani kuhusu jinsi ambavyo ninyi ni watu wa pekee! Ninyi mnahangaikiana na kutunzana.”

Kazi hiyo ilikamilika jioni. Jengo hilo jipya lilikuwa jibu la wazi kwa maonyo yote ambayo familia hiyo ilikuwa imepewa. Mzee mmoja wa kutaniko anakumbuka wakati ambapo yeye na baba wa familia hiyo walisimama umbali fulani ili watazame jengo hilo: “Nilihisi vizuri sana nilipoweka mkono wangu juu ya bega la ndugu yetu aliyebatizwa karibuni na kumwambia, ‘Karibu katika tengenezo la Yehova.’”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Jengo lililoharibiwa kwa moto

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kulijenga upya