Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makaburi Hutufunulia Imani za Kale

Makaburi Hutufunulia Imani za Kale

Makaburi Hutufunulia Imani za Kale

HEBU wazia kwamba unaishi maelfu ya miaka iliyopita. Uko katika jiji la Uru, ambalo ni jiji la kifalme lenye ufanisi huko Sumer, Babilonia. Msafara mkubwa wa Wasumeria umeondoka jijini, umefika kwenye eneo la makaburi, na sasa unateremka kuelekea kwenye kaburi la mfalme fulani aliyekufa hivi karibuni. Kuta na sakafu ya kaburi hilo zimefunikwa kwa mikeka, na chumba kimepambwa kwa vitu vya kisanaa vyenye kupendeza vya Wasumeria. Wanamuziki wanaandamana na msafara huo wa askari, watumishi, na wanawake kwenye kaburi hilo. Wote wamevalia mavazi mazuri yanayovutia. Maofisa wanafurahia kubeba nembo zinazoonyesha vyeo vyao. Kwenye msafara huo wenye kuvutia, kuna magari yanayoendeshwa na wanadamu na kukokotwa na mafahali au punda, huku watunzaji wa wanyama hao wakitembea karibu na vichwa vyao. Wote wanasimama mahali pao, na ibada ya kidini inafanywa huku muziki ukichezwa kwa ala.

Msafara huo wa kidini unapomalizika, kila mtu, kuanzia mwanamuziki hadi mtumishi, anachukua kikombe kidogo cha udongo, mawe, au chuma alichobeba kwenye sherehe hiyo, anakichovya ndani ya chungu cha shaba, na kunywa kinywaji fulani kilichotayarishwa kwa njia maalumu. Kisha wote wanalala chini wakiwa wamejipanga kwa utaratibu, wanajistarehesha kwenye mikeka yao, wanalala usingizi, na kufa. Mtu fulani anachinja wanyama harakaharaka. Wafanyakazi waziba kijia kinachoelekea kaburini na kuliziba kaburi hilo. Wasumeria wanaamini kwamba mfalme wao aliye mungu, sasa anaelekea kwenye ulimwengu mwingine akiwa katika gari lake, pamoja na watumishi wake na askari wa kumlinda.

Alipokuwa akifanya kazi kusini mwa Iraq, mwakiolojia, Bwana Leonard Woolley, alichimbua makaburi 16 ya wafalme katika eneo la makaburi la Uru la kale, kama lile lililotajwa. Huo ulikuwa ugunduzi wenye kutisha na usio wa kawaida. “Mali zilizo katika makaburi hayo, ambazo hazina kifani katika akiolojia ya Mesopotamia zilitia ndani baadhi ya vifaa maarufu zaidi vya kisanaa vya Wasumeria ambavyo sasa vimebandikwa kwenye kuta za Jumba la Makumbusho la Uingereza na Jumba la Makumbusho la Chuo Kikuu cha Pennsylvania,” asema Paul Bahn katika kitabu chake Tombs, Graves and Mummies.

Hata hivyo, dhabihu za kutisha za wanyama na wanadamu kutia ndani makaburi ya Uru la kale hayakuwa ya kipekee. Katika nchi nyingi za kale zilizostaarabika, matajiri na wafalme walifanya jitihada kubwa sana na kutumia mali nyingi sana, nyakati nyingine kwa njia ya ukatili, kujitayarishia kifo na maisha yao ya baadaye. Mara nyingi makaburi yao yalifanana na majumba ya wafalme walio hai kwani yalijaa vifaa vya kisanaa vyenye kuvutia na hazina nyingi. Hata hivyo, siku hizi makaburi hayo na pia makaburi mengine mengi ya kawaida, hutupa habari kuhusu mambo ya kale, na kutuwezesha kuchunguza imani, utamaduni, ustadi wa kisanaa na kiteknolojia wa watu wa kale na staarabu zilizotoweka.

Kuoza Pamoja na Wengine Kwenye Makaburi ya Kifahari

Mnamo 1974, maskini karibu na jiji la Xi’an, huko China, walikuwa wakichimba kisima. Lakini badala ya kupata maji, walipata nyuta za shaba, vichwa vya mishale, na vipande vya watu waliotengenezwa kwa udongo. Bila kujua, walikuwa wamefukua askari-jeshi wakubwa waliotengenezwa kwa udongo miaka 2,100 iliyopita. Askari hao zaidi ya 7,000 pamoja na farasi, walizikwa wakiwa wamesimama na wamejipanga kwenye gwaride! Askari-jeshi hao wa udongo wa Ch’in ambao ni sehemu ya kaburi kubwa zaidi la kifalme huko China, wamepewa jina la Ch’in Shih Huang Ti, maliki aliyeunganisha majimbo ya China yaliyokuwa yakipigana mnamo mwaka wa 221 K.W.K.

Kaburi la Ch’in linaweza kutajwa kuwa jumba la mfalme lililo chini ya ardhi. Lakini kwa nini alizikwa na askari hao wa udongo? Katika kitabu chake The Qin Terracotta Army, Zhang Wenli anasema kwamba “kaburi [la Ch’in] liliwakilisha milki ya Qin [nalo] lilikusudiwa kumpa Qin Shi Huangdi [Ch’in Shih Huang Ti] fahari na mamlaka aliyokuwa nayo akiwa hai wakati ambapo angekufa.” Sasa kaburi hilo ni sehemu ya jumba la makumbusho lililo kwenye eneo kubwa sana lenye makaburi 400 na mashimo yaliyo karibu nalo.

Ili kujenga kaburi hilo, “zaidi ya watu 700,000 kutoka sehemu zote za milki hiyo waliandikishwa,” asema Zhang. Kazi iliendelea baada ya Ch’in kufa mwaka wa 210 K.W.K. na iliendelea kwa muda wa miaka 38. Hata hivyo, si msafara wote wa Ch’in uliozikwa pamoja naye ulikuwa wa udongo. Wanahistoria wanasema kwamba mrithi wa Ch’in aliagiza masuria wa Ch’in ambao hawakuwa na watoto wazikwe pamoja naye, na hivyo kusababisha vifo vya watu “wengi sana.” Kulikuwa na mazoea kama hayo katika nchi nyingine pia.

Kuna magofu ya jiji la kale la Teotihuacán huko kaskazini-mashariki ya Mexico City. Jiji hilo lilikuwa na barabara iliyoitwa Barabara ya Wafu. Bahn aliyenukuliwa mapema anaandika hivi: “Baadhi ya sanamu kuu zaidi za ukumbusho ulimwenguni ziko kwenye barabara hiyo.” Sanamu hizo zinatia ndani Piramidi ya Jua na Piramidi ya Mwezi, ambazo zilijengwa katika karne ya kwanza W.K., na magofu ya Hekalu la Quetzalcoatl.

Inaonekana kwamba sehemu ya ndani ya Piramidi ya Jua ilikuwa mahali pa kuzikia watu wenye vyeo, labda kutia ndani makuhani. Mabaki ya binadamu yaliyopatikana katika makaburi ya ujumla yaliyo karibu yanadokeza kwamba huenda wapiganaji walitolewa kama dhabihu ili kulinda wale waliokuwa ndani. Mitindo tofauti-tofauti ya kuzika watu imefanya waakiolojia waamini kwamba eneo hilo lina mabaki ya watu 200 hivi, kutia ndani watoto ambao huenda walitolewa kama dhabihu katika programu ya kuzindua sanamu za ukumbusho.

Kwenda Ulimwengu Mwingine kwa Mashua au Farasi

Maharamia wa Skandinavia waliokuwa wapiganaji wa baharini ambao walihangaisha Ulaya yapata miaka 1,000 iliyopita, pia walitazamia kuwa na vitu bora ambavyo wangehitaji ili kufurahia maisha baada ya kifo. Waliamini kwamba watu wao waliokufa waliendesha farasi au mashua zao hadi kwenye ulimwengu mwingine. Kwa hiyo, vitu kama mizoga ya farasi waliouawa na mbao zilizooza za mashua kubwa zinaweza kupatikana katika eneo la makaburi la Maharamia hao. Katika kichapo A History of the Vikings, Gwyn Jones anaandika hivi: “Mwanamume au mwanamke aliyekufa alipewa kila kitu ambacho kingefanya maisha ya baadaye yawe yenye kustarehesha na kuheshimika kama yalivyokuwa akiwa duniani . . . Meli hiyo [iliyozikwa] huko Ladby, Denmark . . . ilikuwa na nanga, tayari kushushwa mwishoni mwa safari yake.”

Maharamia wa Skandinavia walikuwa watu waliopenda vita na waliamini kwamba ikiwa wangekufa wakipigana wangeenda nyumbani kwa miungu, mahali panapoitwa Asgard. “Wakiwa huko, wangeweza kupigana kwa siku nzima na kula usiku mzima,” kinasema kichapo World Book Encyclopedia. Pia mazishi ya Maharamia hao yalitia ndani dhabihu za wanadamu. “Mkuu anapokufa, watumwa na watumishi huulizwa ni nani aliye tayari kufa pamoja naye,” kinasema kitabu The Vikings.

Hata Waselti wa kale wa Ulaya kaskazini waliamini kwamba deni linaweza kulipwa katika maisha ya baadaye. Labda hiyo ilikuwa mbinu ya ujanja ya kuahirisha kulipa deni! Huko Mesopotamia, watoto walizikwa pamoja na vitu vya kuchezea. Katika sehemu fulani za Uingereza ya kale, vyakula kama vile miguu ya kondoo ilizikwa pamoja na askari ili wasianze safari yao ya maisha ya baadaye wakiwa na njaa. Huko Amerika ya Kati, wafalme wa Maya walizikwa na vitu vilivyotengenezwa kwa shohamu, ambayo ni jiwe lenye thamani la kijani-kibichi linalowakilisha unyevu na pumzi nzito. Huenda nia ilikuwa kuhakikisha kwamba uhai utaendelea baada ya kifo.

Muda fulani baada ya mwaka wa 1,000 K.W.K., Wathrasi, watu walioogopewa, lakini waliojulikana kuwa wafuaji dhahabu walio stadi, waliishi katika eneo ambalo leo ni sehemu ya Bulgaria, kaskazini mwa Ugiriki na Uturuki. Makaburi ya Wathrasi yanafunua kwamba wakuu wao walizikwa kifahari pamoja na magari ya kukokotwa, farasi, silaha, naam, na wake zao pia. Kwa kweli, mwanamke Mthrasi aliona kuwa ni heshima kutolewa kuwa dhabihu na kuzikwa pamoja na mume wake!

Muda mfupi baadaye, karibu na eneo hilo kaskazini tu ya Bahari Nyeusi, kuliishi Wasikithe. Watu hao waliopenda vita walitumia vikombe vilivyotengenezwa kwa mafuvu ya watu waliowashinda nao walivaa mavazi yaliyotengenezwa kwa ngozi ya vichwa vya watu hao. Katika kaburi moja la Wasikithe, bangi ilipatikana kando ya mifupa ya mwanamke fulani. Fuvu lake lilikuwa na mashimo madogo matatu, labda ya kutuliza uvimbe na maumivu. Labda bangi hiyo iliwekwa kando yake ili awe na kitu cha kumsaidia kutuliza maumivu ya kichwa katika maisha ya baadaye.

Maisha ya Baadaye ya Wamisri

Piramidi za Misri karibu na Cairo na vyumba vya kuzikia watu katika Bonde la Wafalme karibu na Luxor ni miongoni mwa makaburi maarufu zaidi kati ya makaburi yote ya kale. Neno ambalo Wamisri wa kale walitumia kwa “kaburi” lilimaanisha pia “nyumba”—per. “Kwa hiyo, mtu alikuwa na nyumba wakati alipokuwa hai na baada ya kufa,” asema Christine El Mahdy katika kitabu chake Mummies, Myth and Magic in Ancient Egypt. Pia anasema kwamba “kulingana na imani [ya Wamisri], ilikuwa lazima mwili uendelee kuishi ili sehemu nyingine, yaani, ka, ba, na akh pia ziendelee kuwa hai.”

Ka ilikuwa nakala ya kiroho ya mwili nayo ilitia ndani matarajio, tamaa, na mahitaji yake. Baada ya kifo, ka ilitengana na mwili na kuishi kaburini. Kwa kuwa ka ilihitaji kila kitu ambacho mtu alihitaji maishani, “vitu vilivyowekwa kaburini viliwekwa hapo hasa ili kutosheleza mahitaji ya ka,” aandika El Mahdy. Ba inaweza kulinganishwa na sifa za mtu au utu, nayo iliwakilishwa na ndege mwenye kichwa cha binadamu. Ba iliingia mwilini mtu alipozaliwa na kutengana na mwili wakati wa kifo. Sehemu ya tatu, yaani, Akh, “iliibuka” kutoka kwenye mwili uliotiwa mumiani wakati maneno ya kichawi yalipokuwa yakitamkwa. * Akh iliishi katika ulimwengu wa miungu.

Kwa kugawanya mwanadamu katika sehemu tatu, Wamisri walipiga hatua moja zaidi kuliko wanafalsafa Wagiriki wa kale ambao waligawanya mwili wa binadamu katika sehemu mbili, yaani, mwili na “nafsi” yenye ufahamu. Ingawa fundisho hilo lingali linapendwa, haliungwi mkono na Biblia ambayo inasema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5.

Kwa Nini Wanahangaikia Kifo Kupita Kiasi?

Katika kitabu chake Prehistoric Religion, E. O. James anaandika hivi: “Kati ya hali zote . . . ambazo zimemkabili mwanadamu, kifo ndicho kimekuwa chenye kusumbua na kudhuru zaidi . . . Kwa hiyo haishangazi kwamba watu wengi huabudu wafu na hilo limekuwa jambo muhimu tangu mwanzo wa jamii ya kibinadamu.”

Kitabu cha kale zaidi chenye hekima ya kweli, Biblia, kinaita kifo adui wa wanadamu. (1 Wakorintho 15:26) Huo ni ufafanuzi unaofaa sana. Kila kabila na taifa limekataa kukubali kwamba kifo ni mwisho wa mambo yote. Kwa upande mwingine, kwenye Mwanzo 3:19, Biblia inasema hivi kwa usahihi kuhusu jambo ambalo hutukia katika kila kaburi: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” Hata hivyo, Biblia pia hutumia usemi “kaburi la ukumbusho” kuhusiana na wanadamu wengi waliokufa. Kwa nini? Kwa sababu watu wengi walio makaburini, hata wale ambao wameoza kabisa wako katika kumbukumbu la Mungu, wakisubiri wakati ambapo Mungu atawafufua na kuwapa nafasi ya kupata uzima wa milele katika paradiso duniani.—Luka 23:43; Yohana 5:28, 29.

Kwa sasa, wafu hawajui lolote. Yesu alilinganisha hali yao na usingizi. (Yohana 11:11-14) Mtu anapokuwa katika hali hiyo, hahitaji vitu vya kuzikwa navyo au watumishi. Kwa kweli, mara nyingi watu wanaofaidika na hazina zilizozikwa si wafu, bali ni watu walio hai, wale wanaopora makaburi! Kupatana na fundisho lake kuhusu hali ya wafu, Biblia inasema hivi: “Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje.” (1 Timotheo 6:7) Wakristo wanashukuru kama nini kwa kweli hiyo ambayo ‘imewaweka huru’ kutokana na mazoea ya kikatili ya zamani, na nyakati nyingine ya kisasa, yaani, kuabudu wafu.—Yohana 8:32.

Ingawa mazoea ya kuabudu wafu hayana maana yoyote, makaburi ya kifahari ya zamani yamesaidia katika njia fulani. Kama vitu vingi vya kale na hata mabaki ya wafu kwenye makaburi hayangepatikana, hatungefahamu kikamili mambo yaliyotukia zamani na baadhi ya ustaarabu wa wakati huo ambao umetoweka.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Neno “mumiani” linatokana na neno la Kiarabu mummiya, linalomaanisha “lami” au “bereu.” Hapo awali neno hilo lilitumiwa kwa maiti iliyopakwa utomvu kwa sababu ya weusi wake. Sasa neno hilo hutumiwa kurejelea mwili wowote ule uliohifadhiwa, wa mwanadamu au wa mnyama hata kama umehifadhiwa kiaksidenti au kwa kusudi fulani.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

Watu wa Zamani Walikuwa na Afya Kadiri Gani?

Kwa kuchunguza mabaki, hasa mabaki ya miili iliyohifadhiwa makaburini na ile iliyohifadhiwa kwa njia ya asili kwenye vinamasi vilivyojaa mimea iliyooza, mchanga wenye joto wa jangwani, na kwenye barafu na theluji, wanasayansi wamejifunza mengi kuhusu afya ya babu zetu wa kale. Maendeleo ambayo yamefanywa katika sayansi ya chembe za urithi hasa yamewawezesha wanasayansi kuelewa habari nyingi kama vile uhusiano wa kifamilia kati ya Mafarao na malkia wao na pia kujua wasichana Wainka walikuwa na damu ya aina gani. Uchunguzi huo umeonyesha kwamba watu wa kale walipatwa na magonjwa mengi yanayotupata leo, kama vile yabisi-kavu na vipele vigumu.

Inaonekana kwamba Wamisri wa kale walipatwa na magonjwa mengi, hasa kwa sababu ya kuambukizwa vimelea wengi wanaotokana na guinea worm, minyoo ya matumbo na maini kutoka Mto Nile na mifereji ya unyunyiziaji maji. Hilo linatukumbusha ma- neno haya ambayo Mungu aliambia Israeli baada tu ya taifa hilo kukombolewa Misri mwaka wa 1513 K.W.K.: “Yale magonjwa mabaya ya Misri unayoyajua, [Yehova] hatayaweka juu yako.”—Kumbukumbu la Torati 7:15.

[Hisani]

© R Sheridan/ANCIENT ART & ARCHITECTURE COLLECTION LTD

[Picha katika ukurasa wa 20]

Vazi la kichwani na kito cha mjakazi Msumeria aliyezikwa katika kaburi la kifalme huko Uru

[Hisani]

© The British Museum

[Picha katika ukurasa wa 21]

Jeshi la udongo la Ch’in, kila askari alitengenezwa akiwa na uso wa kipekee

[Hisani]

Inset: Erich Lessing/Art Resource, NY; © Joe Carini / Index Stock Imagery

[Picha katika ukurasa wa 23]

Piramidi ya Jua na Barabara ya Wafu huko Teotihuacan, Mexico

[Hisani]

Top: © Philip Baird www.anthroarcheart.org; painting: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 23]

Kushoto: Kifuniko cha mazishi cha dhahabu cha Mfalme Tutankhameni wa Misri; chini: Mchoro wa “ba” kwenye kaburi, akiwa kama ndege mwenye kichwa cha binadamu