Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nasimama Imara Licha ya Ulemavu

Nasimama Imara Licha ya Ulemavu

Nasimama Imara Licha ya Ulemavu

Simulizi la Kouamé NʹGuessan

Mimi na mwenzangu tuling’ang’ana kusukuma baiskeli yetu juu ya kilima fulani. Ilikuwa Novemba 2002, na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilikuwa vimechacha nchini Ivory Coast, Afrika. Kwa hiyo, barabara tuliyotumia haikuwa na watu na ilikuwa na hatari nyingi. Mbele yetu kulikuwa na kituo cha ukaguzi cha wanajeshi. Kwa nini nilikuwa nimefunga safari hiyo hatari wakati huo wa vita?

NILIZALIWA mwaka wa 1978 nikiwa na ugonjwa ambao ulikuwa ukidhoofisha afya yangu polepole. Kwanza nilipata tatizo la kusikia na maumivu makali sana miguuni. Nilipoendelea kukua, familia yetu ilinidhihaki, ikisema kwamba ‘miguu yangu haikufaa kitu na masikio yangu yalijaa uchafu.’ Watu wazima walinidharau, na watoto walisema kwa sauti kubwa kwamba nilikuwa kilema na miguu yangu imevunjika.

Nilianza shule nikiwa na umri wa miaka minane na mara moja wanafunzi wenzangu na walimu wakaanza kunidhulumu. Mara nyingi nilitamani kujificha. Kwa kuwa watu walijua kwamba niliogopa sana, walinifanyia mzaha. Nilitoka nje nilipokuwa tu nikienda shuleni.

Mara nyingi nilijiuliza, ‘kwa nini nilipatwa na ugonjwa huo?’ Mama yangu alisema kwamba ni kwa sababu mtu fulani aliniroga. Nyakati nyingine, nilipowaona watu wengine wakiwa na ulemavu kama wangu nilijiuliza kama wao pia walirogwa.

Katika mwaka wa 1992, nilianza kuwa na maumivu makali kwenye viwiko vyangu. Baada ya maumivu hayo kupungua, sikuweza tena kunyoosha mikono yangu. Miaka miwili baadaye, jicho langu la kushoto lilipofuka. Wazazi wangu walinipeleka kwa waponyaji wengi lakini sikupata nafuu. Ilibidi niache shule afya yangu ilipozidi kuzorota.

Natafuta Majibu

Mwanadarasa mwenzangu aliyependa dini alinialika twende kanisani. Familia yetu iliabudu maumbile; hata hivyo, nilienda kanisani kwa mwaka mmoja. * Sikujifunza mengi kuhusu Biblia huko kanisani, hivyo nilianza kujiuliza ikiwa dini ina manufaa yoyote.

Niliogopeshwa na mafundisho fulani ya kanisa, hasa fundisho la moto wa mateso. Sikudhani nilikuwa mtu mbaya sana hivyo kustahili kuteketezwa milele motoni. Wakati huohuo, sikuamini kwamba nilikuwa mzuri sana kustahili kupata furaha milele mbinguni. Kwa kuwa sikupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali yangu, niliacha kupendezwa na dini.

Mwaka uliofuata nilialikwa kwenye kusanyiko la uponyaji huko Abidjan, mji mkuu wa Ivory Coast. Jiji hilo liko kilometa 150 hivi kutoka mji wetu mdogo wa Vavoua. Kabla hatujaondoka, niliwaambia wasimamizi wa kanisa kwamba sikuwa na pesa za kutosha kulipia ada ya kuingia au chakula. Walidokeza kwamba mahitaji yangu yangeshughulikiwa huko Abidjan, lakini haikuwa hivyo. Ingawa nilikuwa nimezungukwa na umati mkubwa wa watu 40,000 hadi 50,000, nilihisi upweke na kushuka moyo. Hakuna mtu aliyejishughulisha nami.

Nilirudi Vavoua nikiwa bado mgonjwa lakini sasa nilikuwa pia nimekata tamaa. Viongozi wa kanisa waliniambia kwamba Mungu hakuniponya kwa sababu sikuwa na imani. Baada ya tukio hilo, niliacha kabisa mambo ya dini.

Hatimaye, Nafarijiwa Kiroho

Mnamo 1996, Shahidi wa Yehova alitembelea familia yetu. Sikuwa nimewahi kuzungumza na Mashahidi, lakini nilisikiliza kaka yangu alipokuwa akizungumza kwa shauku na Shahidi huyo. Kaka yangu hakupendezwa, lakini mimi nilipendezwa. Kila neno ambalo Shahidi huyo alisema lilinigusa moyo sana.

Shahidi huyo alieleza kwamba dhambi iliwapata wanadamu kwa sababu ya kutotii kwa mwanadamu wa kwanza. Uasi huo ulisababisha hali ya kutokamilika na kifo kwa wanadamu wote. Hata hivyo, Yesu alitoa uhai wake uwe fidia ili dhambi zetu zisamehewe na tupate uzima wa milele. (Waroma 3:23; 5:12, 17-19) Isitoshe, Shahidi huyo alinionyesha kutoka katika Biblia kwamba hivi karibuni kupitia Ufalme wake, Yehova Mungu atageuza dunia iwe paradiso na kuondoa dhambi na matokeo yake yote yenye kuhuzunisha.—Isaya 33:24; Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4.

Niliguswa moyo sana na jinsi mafundisho ya Biblia yalivyopatana na akili. Shahidi huyo ambaye baadaye nilijua anaitwa Robert alipanga kujifunza Biblia nami mara mbili kwa juma. Baada ya miezi michache, nikiwa na ujuzi wa Biblia niliopata karibuni, nilistahili kuambatana na Mashahidi katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Ilikuwa vigumu sana kwangu kufanya hivyo kwa kuwa ilinibidi nishinde woga wa kuchangamana na watu.

Vizuizi Vyatokea

Familia yetu haikufurahi nilipoanza kujifunza Biblia. Ili kunikasirisha, kaka yangu alivuta sigara usiku katika chumba changu cha kulala. Asubuhi niliumwa na kichwa na kujihisi mgonjwa. Tatizo lingine lilikuwa chakula tulichokula. Baba alikuwa mwindaji stadi, kwa hiyo tulikula nyama kwa ukawaida. Nilimweleza kwamba Biblia inakataza kula nyama ambayo haijatolewa damu. (Matendo 15:28, 29) Lakini bado alikataa kutoa damu ya wanyama hao. Mara kwa mara mama alinipa wali mkavu, lakini mara nyingi nililala njaa.

Ingawa Jumba la Ufalme la Vavoua lilikuwa upande ule mwingine wa mji, sikuruhusu umbali au hali mbaya ya hewa inizuie kuhudhuria mikutano. Nilibatizwa Septemba 1997 kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Imani Katika Neno la Mungu,” nchini Ivory Coast. Hatimaye nikaongeza muda niliotumia kuhubiri hivi kwamba nilistahili kuwa painia, jina ambalo Mashahidi wa Yehova huwaita wahudumu wao wa wakati wote.

Matatizo Mengine

Msukosuko wa kisiasa ulisababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe mnamo Septemba 2002. Katika muda wa majuma machache, jeshi la kitaifa lilikaribia Vavoua. Wakihofia usalama wao, watu fulani, kutia ndani Mashahidi wengi wa Yehova walikimbia. Siku tano baada ya watu kuondoka, wanajeshi walitwaa mji huo na mara moja wakapiga marufuku utendaji wote wa umma. Kwa sababu hiyo, wakazi wengi wa Vavoua kutia ndani Mashahidi waliokuwa wamebaki walikimbia.

Kwa kuwa hakukuwa na usafiri wa umma, ilibidi watu watembee kilometa kadhaa hadi miji jirani. Singeweza kutembea kwa muda mrefu, kwa hiyo mimi tu ndiye Shahidi aliyebaki huko Vavoua. Niliendelea kuhubiri, na kufanya mikutano ya kutaniko ambayo baadhi ya wakazi wa mji huo walihudhuria.

Jitihada za Kuhudhuria Kusanyiko

Kusanyiko la pekee la Mashahidi wa Yehova lilikuwa limepangwa kufanywa Novemba katika mji wa Daloa. Nilisali kwa Yehova kuhusu tamaa yangu ya kuhudhuria kusanyiko hilo. Bila kutarajiwa, Shahidi mmoja ambaye alikuwa amekimbia alirudi mjini. Nilimwomba anibebe kwenye baiskeli yake hadi kwenye mji wa kusanyiko uliokuwa umbali wa kilometa 50 hivi. Alikubali mara moja, ingawa hata yeye alikuwa na matatizo mabaya ya afya.

Watu walikuwa na wasiwasi mwingi kwa hiyo huo haukuwa wakati mzuri wa kusafiri. Magari yalizuiwa kusafiri kutoka Vavoua hadi Daloa. Msafiri yeyote asiyejulikana angeweza kushukiwa kuwa mwanajeshi wa upinzani na kupigwa risasi. Licha ya hayo, Jumamosi asubuhi, Novemba 9, 2002, tulisafiri kwa baiskeli kutoka Vavoua kuelekea Daloa kama nilivyotaja mwanzoni mwa simulizi hili.

Punde si punde tulifika kwenye kituo cha kwanza cha ukaguzi. Tulipekuliwa kabisa kisha tukaruhusiwa kuendelea na safari yetu. Safari hiyo ilikuwa ndefu na yenye kuchosha. Tulitembea hadi kwenye kilele cha kilima kisha tukateremka kwa baiskeli upande ule mwingine.

Baada ya muda, mwendesha-baiskeli mwingine alijitolea kutusaidia. Niliketi kwenye kiti kidogo cha nyuma cha baiskeli yake. Tulipokuwa tukisafiri na mgeni huyo mkarimu, nilitumia nafasi hiyo kumweleza kuhusu Ufalme wa Mungu. Nilimweleza kwamba serikali ya Mungu ni ya kimbingu na kwamba hivi karibuni italeta amani ya kudumu duniani. Alishangazwa na yale niliyomwambia na akaniuliza maswali mengi sana. Tulipofika Daloa, alitununulia chakula na akaahidi kuhudhuria kusanyiko la pekee siku iliyofuata.

Tuliwasili Daloa jioni, tukiwa wachovu lakini wenye furaha kwa kuwa tulikuwa tumefika mwisho wa safari yetu. Safari hiyo iliyochukua muda wa saa tisa haikuwa rahisi. Familia moja ya Mashahidi iliyokuwa ikiishi huko ilitukaribisha kwa uchangamfu na kutuambia tukae kwao hadi hali itulie. Kwa kusikitika, ilibidi kusanyiko livunjwe kwa sababu ya msukosuko huo wa kisiasa. Hata hivyo, safari yetu haikuwa ya bure. Ilifanya nipate pendeleo la kuwatumikia Wakristo wenzangu huko Daloa.

Azimio Langu Limeniletea Baraka

Sasa ninatumika nikiwa mtumishi wa huduma na painia wa kawaida katika kutaniko moja mjini Daloa. Ninasaidia pia kutunza Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Daloa. Ili kujiruzuku, mimi huchonga na kuuza vipepeo vya mbao na pia kuchora vibandiko vya ishara.

Kwa miaka mingi nilitoka nyumbani nilipokuwa tu nikienda shuleni, lakini sasa mimi husafiri kilometa nyingi nikitafuta wale wanaotaka sana kujua sababu zinazofanya kuwe na magonjwa na kuteseka. Ninapongojea Ufalme wa Mungu uondoe magonjwa yote, ninaendelea kuwaambia watu wa Ivory Coast habari njema zenye kufariji kuhusu makusudi ya Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Waabudu-maumbile huamini kwamba wanyama, mimea, na vitu vingine vya asili vina uhai na ufahamu.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa njiani kuelekea Daloa kuhudhuria kusanyiko

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nasaidia kutunza Jumba letu la Kusanyiko la Daloa

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ili nijiruzuku, mimi huchonga na kuuza vipepeo vya mbao