Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukosefu wa Makao—Tatizo la Ulimwenguni Pote

Ukosefu wa Makao—Tatizo la Ulimwenguni Pote

Ukosefu wa Makao—Tatizo la Ulimwenguni Pote

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI POLAND

“WALEVI wachafu wanaonuka, wasio na chochote, na wasiojulikana na yeyote!” Hayo ni maneno yenye kushangaza, lakini kulingana na wajitoleaji ambao huwashughulikia watu wasio na makao huko Czestochowa, Poland, hivyo ndivyo watu wengi kwa kawaida huwaona watu wasio na makao.

Kulingana na ripoti iliyotolewa miaka michache iliyopita katika gazeti The Economist, maelfu ya watoto wa mitaani walikuwa wakiishi katika vijia vyenye uvundo vinavyoelekea kwenye mabomba ya maji machafu au kwenye mfumo wa kupasha jiji joto chini ya barabara za jiji la Ulaanbaatar, Mongolia. Ingawa Wamongolia walishtuka kusikia kuhusu watoto hao wasio na makao, wengi wao walikata kauli kwamba hali hiyo ilitokea “kwa sababu watu ni wavivu sana hivi kwamba hawawezi kuwatunza watoto wao,” lilisema jarida hilo.

Katika sehemu nyingine ya ulimwengu, watoto wa mitaani huuawa na vikundi vya kulinda usalama vinavyochukua sheria mikononi mwao. Kwa nini? Kichapo fulani cha Umoja wa Mataifa kinaeleza hivi: “Huko Amerika Kusini, wafanyakazi wengi wa idara ya mahakama, polisi, vyombo vya habari, wafanyabiashara, na jamii kwa ujumla wanaamini kwamba watoto wa mitaani ni tisho kwa maadili ya jamii iliyostaarabika.” Kichapo hichohicho kinasema: “Inaripotiwa kwamba kwa wastani watoto watatu wa mitaani huuawa kila siku katika jimbo la Rio de Janeiro.”

Watu wasio na makao “hufanya tuwe na woga na wasiwasi . . . , lakini wao ni wanadamu ambao huhisi njaa kama sisi. Watu hao ni wengi, na wana uhitaji wa kweli.” Ndivyo kinavyosema kituo cha Intaneti kilichoanzishwa na wafanyakazi wa kujitolea ambacho hushughulikia watu wasio na makao huko Czestochowa. Kituo hichohicho kinaongeza hivi: “Tunatumaini kwamba . . . kuna watu ambao watachukua hatua ya kushughulikia uhitaji huo mkubwa.” Uhitaji huo ni nini, nao ni mkubwa kadiri gani?

[Picha katika ukurasa wa 2, 3]

Watoto fulani wasio na makao huishi ndani ya shimo hili la maji machafu

[Hisani]

Jacob Ehrbahn/Morgenavisen Jyllands-Posten