Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hadithi za Biblia Zasimuliwa kwa Barafu na Theluji

Hadithi za Biblia Zasimuliwa kwa Barafu na Theluji

Hadithi za Biblia Zasimuliwa kwa Barafu na Theluji

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI UJERUMANI

“NI MARIDADI wee!” Hivyo ndivyo Anja alivyosema. Georg alisema, “Inashangaza kuona vitu ambavyo watu wanaweza kutengeneza kwa kutumia barafu na theluji.” Hamu yetu ikiwa imechochewa, tulisafiri hadi Lübeck huko kaskazini mwa Ujerumani kuona maonyesho ya sanamu za barafu yaliyoitwa Ice World. Maonyesho hayo yalikuwa na kichwa, “Hadithi za Biblia Kutoka Agano la Kale na Agano Jipya.”

Tulipofika Lübeck, lango maarufu la Holstein Gate lilikuwa limefunikwa na mawingu ya mvua. Karibu na lango hilo kulikuwa na hema kubwa la kawaida. Lakini ndani tuliona sanamu za theluji na barafu ambazo ziling’aa kwa rangi tofauti-tofauti zilipopigwa na nuru.

Hata kabla ya kuanza kuzunguka, tulikumbuka kwamba tulikuwa tumeonywa tuvalie mavazi yenye joto. Ndani kulikuwa na baridi! Ingawa mtu anayeishi sehemu zenye baridi anaweza kuona nyuzi 10 Selsiasi chini ya sufuri kuwa si baridi sana, wengine wetu tulifadhaika kwa kuwa tulikuwa tumesahau kubeba skafu na glavu. Hata hivyo, tulipoona sanamu zenye kupendeza za barafu zilizokuwa na rangi mbalimbali hatukuhisi baridi.

Mandhari za Biblia Zilizochongwa Kwenye Barafu

Tuliona malaika akiwa na nguo yenye mikunjo maridadi, akipiga tarumbeta. Sanamu hiyo ilionekana kana kwamba inaelea juu ya theluji. Kulikuwa na sanamu zilizoonyesha hatua mbalimbali za uumbaji, kutia ndani kuumbwa kwa Adamu. Mbele kidogo, tuliona safina ya Noa. Tulicheka tulipoona kiboko akijaribu kumsukuma mwenzake aingie kwenye mlango wa safina huku mnyama fulani mdogo akijaribu kujipenyeza kwenye safina chini ya tumbo la kiboko aliyekwama mlangoni. Noa alikuwa karibu akiwa amesimama kando ya rundo la mbao za barafu.

Kisha tuliona mandhari ya shamba la Edeni, iliyoonyesha dhambi ya Adamu na Hawa. Halafu tukasimama mbele ya sanamu kubwa tuliyokuwa na hamu ya kuichunguza kwa makini: Musa akiwa amebeba mabamba mawili ya Sheria. Ni nini hasa kilichofanya tuvutiwe na sanamu hiyo?

Mabamba hayo ya barafu hayakuwa yameandikwa zile Amri Kumi, bali ile Tetragramatoni, yaani, jina la Mungu la kibinafsi, Yehova! Tulisisimka kuona jina la Mungu katika Kiebrania likiwa limeandikwa waziwazi. Hata broshua ya maonyesho hayo ilionyesha sanamu hiyo ya Musa kwenye jalada, Tetragramatoni ikionekana wazi katikati. Tulipiga picha nyingi za mandhari hiyo. Karibu na sanamu hiyo kulikuwa na sanamu ya ndama ambayo ilimetameta kama dhahabu ilipopigwa na nuru. Ilitukumbusha ibada ya sanamu isiyo ya maadili ambayo Waisraeli walijihusisha nayo muda mfupi tu baada ya kukombolewa kutoka Misri.

Kwa kusikitisha, ilikuwa vigumu kutambua sanamu ya Yakobo na Esau na ile ya Yosefu na Farao zilizokuwa zimechongwa kwenye ukuta wa theluji. Sanamu fulani ziliharibika kwa sababu zilikuwa zimetazamwa na wageni wapatao 100,000 katika majuma matatu ya kwanza ya maonyesho hayo. Hata hivyo, sanamu kubwa ya Samsoni aliyekuwa akiangusha nguzo za hekalu la Wafilisti haikuwa imeharibika. Kulikuwa na sanamu nyingine ya Samsoni wakati Delila alipofanya anyolewe.

Pia kulikuwa na sanamu ya Daudi anayetajwa katika Biblia, kwanza baada ya kumshinda Goliathi kisha aliposhindwa kujizuia kumtazama Bath-sheba akioga. Kwenye pembe nyingine kulikuwa na sanamu ya kuzaliwa kwa Yesu. Iliangaliana na sanamu iliyochongwa kwenye ukuta wa theluji iliyoonyesha Mlo wa Jioni wa Bwana.

Baada ya kutazama sanamu hizo zote, tulihisi baridi sana. Kwa hiyo, tulitoka na kwenda kwenye mkahawa ulio karibu na Holstein Hall. Video kuhusu jinsi ambavyo sanamu hizo zilitengenezwa ilionyeshwa kwenye televisheni kadhaa kwenye jumba hilo.

Jinsi Sanamu Hizo Zilivyotengenezwa

Kwanza, tani 350 za vipande vya barafu vyenye urefu wa meta 2 hivi upana wa meta 1 na kimo cha meta 0.6 vilikuwa vimesafirishwa kwa malori kutoka Ubelgiji na kupangwa kulingana na ukubwa wa sanamu ambazo vipande hivyo vingetengeneza. Mashini kubwa ilitengeneza tani 200 za theluji na kuipuliza kwenye katoni kubwa. Kwa kutumia misumeno ya umeme, patasi, miswaki, na mirija, wachongaji sanamu walitengeneza sanamu kwa kutegemea masimulizi ya Biblia.

Kulingana na msimamizi wa mradi huo, Jana Kürbis, kazi kubwa zaidi ilikuwa kutokeza na kudumisha hali inayofaa ya hewa. Kazi yote iliyofanywa ili kutayarisha maonyesho hayo ilithaminiwa sana. Mwanamke mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Siamini macho yangu!” Mwanamume mmoja alisema kwamba maonyesho hayo yalikuwa “bora sana.” Hata hivyo, mke wake alisikitika kwamba hakuijua Biblia vizuri.

Wengi, kutia ndani wachanga, walitembelea sanamu mbalimbali huku wakisoma maandishi yaliyochapwa yaliyoeleza kuhusu mandhari zilizotolewa katika Biblia. Tulipoondoka kwenye maonyesho ya Ice World, tulikuwa tumepiga picha nyingi sana lakini pia tutakumbuka daima hadithi za Biblia zilizosimuliwa kwa kutumia theluji na barafu.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Jina la kibinafsi la Mungu, Yehova katika Kiebrania, lilionyeshwa kwenye broshua ya maonyesho hayo

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Kuumbwa kwa Adamu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Samsoni akiangusha nguzo za hekalu la Wafilisti

[Picha katika ukurasa wa 17]

Daudi na Goliathi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Safina ya Noa

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 16]

Moses in ice: Foto von: Nils Bergmann; snow crystal: snowcrystals.net; creation of Adam: Foto von: Nils Bergmann