Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhukumiwa Mara Mbili Kifungo cha Miaka 25 ya Kazi Ngumu

Kuhukumiwa Mara Mbili Kifungo cha Miaka 25 ya Kazi Ngumu

Kuhukumiwa Mara Mbili Kifungo cha Miaka 25 ya Kazi Ngumu

SIMULIZI LA EFREM PLATON

Karibu na mwisho wa 1951, nilihukumiwa kwa mara ya pili kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu. Wakati huo nilitumwa katika kambi yenye sifa mbaya ya Sovieti huko Vorkuta, juu ya Mzingo wa Aktiki. Hebu nieleze jinsi nilivyofika huko na jinsi nilivyoponea chupuchupu kifo chenye jeuri.

NILIZALIWA Julai 16, 1920, katika familia maskini huko Bessarabia, katika eneo ambalo sasa ni Jamhuri ya Moldova. Baba alikufa muda mfupi kabla sijazaliwa, naye Mama alikufa nilipokuwa na umri wa miaka minne. Hivyo sisi watoto sita tukawa mayatima. Ninawashukuru sana ndugu zangu wakubwa ambao walichukua jukumu la wazazi wetu na kututunza.

Nilipokuwa kijana, nilipendezwa sana na mambo ya kidini na nilijihusisha sana na mambo ya Kanisa Othodoksi la kwetu. Hata hivyo, baada ya muda nilitamaushwa na kanisa, hasa na makasisi wake ambao walibariki jitihada za mataifa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu ambavyo vilianza mnamo Septemba 1939.

Vita vilizuka mapema katika miaka ya 1940 kati ya Rumania na Muungano wa Sovieti, nayo Bessarabia ilijikuta katikati ya makabiliano hayo. Jenerali Ion Antonescu, aliyekuwa akitawala Rumania wakati huo, aliteka tena Bessarabia. Serikali ilianzisha mazoezi ya kijeshi kwa wanaume wenye umri wa miaka 20 au zaidi. Nilikuwa kati ya wale waliochaguliwa kushiriki mazoezi hayo. Mazoezi yetu yalifanywa Boroşeni, karibu na kijiji ambacho mimi na mke wangu Olga tulikuwa tukiishi.

Kujifunza Ukweli wa Biblia

Siku moja wakati wa mapumziko ya mchana, niliona kikundi cha wanaume wakizungumza kwa uchangamfu; niligundua kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova. Mazungumzo yangu mafupi pamoja nao yaliongoza kwenye mazungumzo mengine. Baada ya muda, niligundua kwa shangwe kwamba nilikuwa nimepata ukweli wa Biblia na nikamweleza Olga na wazazi wake.

Mazungumzo yaliyonivutia siku hiyo yalihusu suala la kutokuwamo. Mashahidi hao walikubaliana kwamba walihitaji kuwa na msimamo kuhusu jambo hilo. Waliamua watashiriki katika mafunzo ya kijeshi lakini wakatae kula kiapo cha uaminifu, jambo lililokuwa lazima ili kuandikishwa katika jeshi.

Nilimwambia Olga na wazazi wake kwamba nilikusudia pia kukataa kula kiapo hicho, nao wakaunga mkono uamuzi wangu. Siku ya kuandikishwa ilipofika, Januari 24, 1943, uliwadia wakati wa kula kiapo cha uaminifu. Sisi wanane tulimwendea kasisi aliyekuwa akiwaandikisha watu. Badala ya kula kiapo, tulisema kwamba hatutashiriki katika vita kwa sababu sisi hatuungi mkono upande wowote.

Tulikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi huko Boroşeni. Tukiwa huko tulipigwa kikatili sana hivi kwamba mke wangu hangeweza kunitambua baadaye. Tulihamishwa hadi Chişinău (iliyokuwa Kishinev), jiji kuu la nchi hiyo, ili tufikishwe mbele ya mahakama ya kijeshi.

Tulilazimika kutembea kilometa 140 hivi, safari iliyochukua siku 21 kwa sababu ya baridi kali. Sisi wanane tulifungwa pamoja na kuongozwa na askari wenye silaha ambao hawakutupa chakula au maji. Tulisimama katika vituo 13 tukiwa njiani na kila wakati tulipofika katika kituo kingine cha polisi tulichapwa! Tuliendelea kuwa hai kwa sababu wenyeji walitupa chakula na maji katika vituo ambavyo tulilala. Tuliona kwamba Mungu alitutunza kupitia matendo yao ya fadhili.

Twaimarishwa Licha ya Kuvunjika Moyo

Tulipokuwa kifungoni huko Chişinău tukisubiri kufikishwa mbele ya mahakama ya kijeshi, sisi wanane tuliteswa tena vibaya. Wenye mamlaka walijaribu kuvunja imani yetu kwa kutuambia eti Mashahidi wa Zăicani, kijiji kilichokuwa kaskazini mwa Moldova, walikuwa wamekana imani yao na kuruhusiwa kurudi nyumbani. Baadaye tuligundua kwamba walikuwa wamerudi nyumbani ili wasubiri kufikishwa mbele ya mahakama. Pia, polisi mmoja, akinukuu makala moja katika gazeti, alisema kwamba mahakama ya jeshi nchini Ukrainia ilikuwa imewahukumu kifo Mashahidi 80.

Wengine kati yetu walikuwa wameanza kuvunjika moyo, wakifikiri kwamba hawatawaona watoto wao tena. Tuliahidiwa kwamba tungeachiliwa ikiwa tungekana imani yetu. Ili tufikiri kuhusu wakati wetu ujao, sote tuliruhusiwa kwenda nyumbani kukaa na familia zetu kwa juma moja. Baadaye, ni watatu tu kati yetu tuliodumisha msimamo wa kutokuwamo.

Februari 20, 1943, nilipelekwa kwenye kituo kilekile cha polisi huko Boroşeni ambako nilikuwa nimepigwa sana mbeleni. Huko niliwapata Mashahidi wenzangu wawili ambao walikuwa wamedumisha msimamo wao wa kutokuwamo. Tulifurahi sana kukutana tena! Baadaye, tulipelekwa Bălţi kwa gari lililokokotwa na farasi. Tukiwa safarini, nilikuwa mgonjwa sana, na hilo likawa baraka kwani tokea hapo tulisafiri kwa basi hadi Chişinău.

Tulipowasili, walinzi walitambua kwamba sisi watatu ndio tuliokuwa tumedumisha msimamo wa kutokuwamo. Ili kutukaribisha walitupiga tena. Mwezi mmoja baadaye tulihukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Rumania.

Nabatizwa Katika Shimo Lililochimbwa na Bomu

Mwishowe tulitumwa mji wa Cugir, nchini Rumania, ambako tulifanya kazi ya kukata miti msituni. Ikiwa tungekata miti kiasi fulani, tungeongezewa kiasi cha chakula. Kikundi chetu cha Mashahidi kumi kilikuwa na bidii, kwa hiyo tulikula vizuri zaidi kuliko tulivyokula katika magereza mengine.

Mnamo 1944 majeshi ya Marekani yalianza kulipua eneo lililokuwa karibu na kambi yetu. Siku moja bomu lililipua shimo kubwa karibu na kijito. Shimo hilo likaanza kujaa maji, na baada ya muda kulikuwa na kidimbwi kikubwa. Mnamo Septemba 1944, nilizamishwa hapo ili kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu niliokuwa nimefanya zaidi ya mwaka mmoja na nusu mapema.

Huru Hatimaye!

Majuma machache baadaye, jeshi la Urusi liliwaachilia mamia ya Mashahidi katika eneo lote, nasi tuliweza kurudi nyumbani. Kwa mara ya kwanza nilimwona mwanangu Vasile, ambaye alizaliwa mwaka wa 1943 nilipokuwa katika kambi ya kazi ngumu.

Kufikia mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu mnamo Mei 1945, Bessarabia ilikuwa imefanywa kuwa jimbo la Muungano wa Sovieti na kuwa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Moldavia. Wenye mamlaka hawakuchukua hatua mara moja dhidi ya shughuli zetu za Kikristo. Hata hivyo, walitambua kwamba hatukupiga kura, nayo Serikali ya Sovieti iliona jambo hilo kuwa kosa kubwa sana.

Katika mwaka wa 1946 tulipata mwana wetu wa pili, Pavel, na mnamo 1947, binti yetu Maria, akazaliwa. Tulifurahia sana maisha yetu ya familia! Lakini miaka miwili hivi baadaye tulipatwa na msiba. Msichana wetu mdogo Maria akawa mgonjwa na kufa ghafula. Alizikwa Julai 5, 1949. Lakini huo ulikuwa mwanzo tu wa mambo yenye kutuhuzunisha.

Kuhamishwa Hadi Siberia

Saa chache tu baada ya kumzika Maria, kulipokuwa kungali na giza asubuhi iliyofuata, askari-jeshi watatu walituamsha. Walitujulisha kwamba tungehamishwa kwa sababu ya ‘tabia yetu ya kupinga Serikali ya Sovieti.’ Tuliruhusiwa kubeba kiasi fulani cha chakula na mavazi, na Julai 6, 1949, tukasafirishwa umbali wa kilometa 4,000 hivi hadi Kurgan, Siberia, kaskazini ya Kazakhstan.

Safari hiyo ilichukua siku 18. Tulisafirishwa kama ng’ombe, ndani ya mabehewa ya gari-moshi. Tulipewa chakula mara mbili tu tulipokuwa njiani. Tulitumia chakula chetu kwa uangalifu ili kiweze kututosha muda wote wa safari. Wote waliokuwa katika behewa letu walikuwa Mashahidi wa Yehova. Tulidumisha hali yetu ya kiroho kila siku kwa kuwa na mazungumzo mengi ya Biblia. Kitu muhimu zaidi tulichokuwa nacho kilikuwa nakala ya Maandiko Matakatifu.

Hatimaye tulipofika Kurgan, tuligundua kwamba ingawa tuliishi katika kambi ya kazi ngumu, kulikuwa na uhuru wa kwenda sehemu mbalimbali. Nilifanya kazi katika duka la uhunzi na niliweza kuwaambia wafanyakazi wenzangu kuhusu tumaini langu la Biblia. Miaka miwili baadaye, katika Septemba 27, 1951, nilikamatwa na kupelekwa mahakamani tena. Waendesha-mashtaka waliwaleta watu 18 waliosema kwamba nilikuwa nimetabiri kuangamizwa kwa Taifa letu. Lakini kwa kweli, nilikuwa nimetumia unabii wa Danieli 2:44 kuonyesha kwamba Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za wanadamu.

Kuongezea, wenye mamlaka walikuwa wamefanya msako wa nyumba yetu na kupata gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokuwa limetumwa kwa siri kutoka Moldova. Kwa kawaida, wenye mamlaka wangepata nakala za magazeti zilizoandikwa kwa mkono au zilizochapishwa nchini humo. Hata hivyo, nakala hiyo ilikuwa imechapwa nje ya Muungano wa Sovieti. Kwa hiyo, nilihukumiwa kwa mara ya pili kifungo cha miaka 25 cha kazi ya kulazimishwa. Wakati huu nilipelekwa katika migodi ya makaa ya mawe ya Vorkuta, iliyokuwa kambi ya kazi ngumu yenye sifa mbaya sana kwenye mwisho wa upande wa kaskazini wa Milima Ural, juu ya Mzingo wa Aktiki.

Kuepuka Kifo Huko Vorkuta

Vorkuta lilikuwa gereza kubwa lenye kambi 60 za kazi ya kulazimishwa. Katika kambi yetu tu, kulikuwa na zaidi ya wafungwa 6,000. Watu wengi walikufa kutokana na baridi kali sana, hali mbaya sana za maisha, na kwa sababu ya kuchimba makaa ya mawe chini ya ardhi. Karibu kila siku kulikuwa na watu waliokufa waliohitaji kuzikwa. Afya yangu ilikuwa mbaya sana hivi kwamba singeweza kufanya kazi ngumu ya mikono. Nilipewa kazi iliyosemekana kuwa rahisi zaidi, yaani, kuchota makaa ya mawe na kuyajaza ndani ya tramu zilizokuwa zikingoja.

Hali zilikuwa mbaya sana huko Vorkuta hivi kwamba wachimba-migodi walipanga mgomo, lakini uligeuka na kuwa uasi. Wachimba-migodi walichagua wasimamizi wao na kupanga kikosi cha wanaume 150 ambao wangekabiliana askari iwapo wangekuja. Walitaka mimi na Mashahidi wengine 30 hivi tujiunge na “jeshi” lao lakini tulikataa.

Uasi huo uliendelea kwa majuma mawili hadi askari waliokuwa na silaha walipowasili na kuwapiga risasi waasi wote. Tuliambiwa kwamba waasi hao walikuwa wamepanga kutunyonga ndani ya chumba cha kufanya kazi! Inafurahisha kwamba hawakufaulu kutekeleza mipango yao. Unapofikiria mbinu zenye mpango za Wasovieti za kuvunja imani yetu, unaweza kuelewa sababu iliyotufanya tuone kwamba Mungu wetu mkuu, Yehova ndiye aliyetuokoa!

Kutumia Vizuri Uhuru Uliongezeka

Kifo cha Stalin mnamo Machi 1953 kilitokeza mabadiliko mazuri kwa hali yetu. Katika mwaka wa 1955, nilifunguliwa kutoka Vorkuta na kuruhusiwa nirudie familia yangu, ambayo ilikuwa ikiishi katika kambi ya msitu wa Kurgan. Tuliendelea kuwahubiria watu wa huko tumaini letu zuri.

Kufikia mwaka wa 1961, tulitamani kuhamia eneo jipya kuhubiri. Kwa hiyo, tulimwandikia barua mkuu wa nchi, Nikita Khrushchev, tukiomba ruhusa ya kuhama, na tukamwambia kuwa hakukuwa na shule kwa ajili ya watoto wetu, na hilo lilikuwa kweli. Tuliruhusiwa kuhamia mji mdogo wa Makushino, ambako pia kulikuwa na kambi ya kazi. Tulipata shangwe kubwa sana kusaidia familia nne kubwa kuwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu.

Mwishowe, mnamo 1965, nilifunguliwa kutoka kambi hiyo. Ingawa bado hatukuruhusiwa kurudi Moldova, tungeweza kuhamia mahali popote pale katika Muungano wa Sovieti. Mwaka uliofuata tulihamia Qostanay (iliyokuwa Kustanai), huko Kazakhstan, ambako tayari kulikuwa na makutaniko mawili ya Mashahidi. Kwa kuwa eneo hilo lilihubiriwa sana, miaka mitatu baadaye tulihamia Chirchik, nchini Uzibekistani. Wakati huo wana wetu Vasile na Pavel walikuwa wameoa. Kwa hiyo, tulikazia fikira zetu kusaidia kiroho watoto waliosalia, Dumitru, aliyekuwa na umri wa miaka 10, na Liuba, aliyekuwa na umri wa miaka 7.

Tuliishi Uzibekistani kwa miaka kumi, na katika muda huo tuliweza pia kuwasaidia wengine wamjue Yehova. Mnamo 1979 tulihama zaidi ya kilometa 1,600 kutoka hapo na kuelekea upande wa magharibi kwenye jiji la Krasnodar lililoko karibu na Bahari Nyeusi kusini mwa Urusi. Huko mimi na Olga tulitumikia kwa miaka miwili katika utumishi wa wakati wote tukiwa mapainia, na tuliwasaidia wengine wawe Mashahidi.

Kurudi Moldova

Mwishowe, katika kiangazi cha 1989, miaka 40 baada ya kupelekwa uhamishoni, tuliamua kurudi nyumbani Moldova. Mara moja, tulianza tena upainia, hadi mwaka wa 1993. Tuliwasaidia watu zaidi ya 30 kuwa Mashahidi wa Yehova wenye bidii. Moyo wangu hujaa shangwe ninapowazia jinsi ambavyo Yehova amebariki familia yetu! Hata hivyo, kwa kuhuzunisha mke wangu mpendwa alikufa mnamo Mei 2004.

Lakini, mimi hufarijiwa kwa sababu watoto wetu wote 4, kutia ndani wajukuu wetu 14 na vitukuu 18, wanamtumikia Yehova kwa bidii. Ni kweli kwamba maisha yetu yalikuwa magumu, lakini inapendeza sana kujua kwamba Yehova ametusaidia tubaki tukiwa waaminifu kwake katika majaribu yetu!

Kadiri ambavyo miaka yangu imesonga, afya mbaya na kuzeeka kumenizuia nisifanye mengi katika huduma. Lakini bado mimi hujitahidi kufanya yote niwezayo. Nimejifunza kwamba hata tukabili majaribu gani maishani, Yehova yuko tayari kutupa nguvu na kitia moyo tunachohitaji. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 42 Efrem Platon alikufa Julai 28, 2005, makala hii ilipokuwa ikitayarishwa ili ichapishwe.

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Mashahidi wa Yehova katika kambi ya kazi ngumu ya Vorkuta

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Olga mnamo 2002