Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tauni—Wakati Ujao Utakuwaje?

Tauni—Wakati Ujao Utakuwaje?

Tauni—Wakati Ujao Utakuwaje?

WATU fulani ambao wamechunguza tauni ya homa ya 1918-1919 wamekumbushwa kwa njia yenye kutokeza unabii wa Biblia. Kwa mfano, Gina Kolata anasema hivi katika kitabu chake Flu—The Story of the Great Influenza Pandemic of 1918 and the Search for the Virus that Caused It: “Tauni ya mwaka wa 1918 iliitwa homa, lakini ilikuwa tofauti na homa nyingine ambazo zimewahi kutokea. Ilikuwa ni kana kwamba unabii wa Biblia unatimizwa.”

Je, ni kweli kwamba Biblia huzungumzia jambo linalohusiana na msiba huo uliowapata wanadamu? Ndiyo.

Unabii wa Biblia na Tauni

Wanafunzi wa Yesu Kristo walimwomba awape ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Yesu alijibu kwa kuwaambia: “Taifa litasimama kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi, na katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni.” (Luka 21:7, 10, 11) Pia Biblia inatabiri kwamba wakati wa mwisho, kutakuwa na “pigo lenye kufisha.”Ufunuo 6:8.

Homa ya Hispania ilianza karibu na mwisho wa vile Vita Vikuu (1914-1918), ambavyo baadaye viliitwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Unabii wa Biblia kuhusu “siku za mwisho” ulianza kutimia wakati huo. Unabii huo unataja upungufu mkubwa sana wa chakula, matetemeko makubwa ya nchi, kuongezeka kwa uasi-sheria, na kuzorota kwa viwango vya maadili. Bila shaka umejionea hali hizo katika ulimwengu leo.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.

Kutimizwa kwa unabii kuhusu “tauni” na “pigo lenye kufisha” kumetokeza woga na taabu isiyo na kifani, na vifo. Na kulingana na jarida Microbes and Infection, “hakuna sababu ya kufikiri kwamba tauni nyingine haitatokea wakati ujao. Inaonekana kwamba jambo hilo haliwezi kuepukika.”

Bado Kuna Tisho

Jarida Emerging Infectious Diseases la Aprili 2005 linasema: “Wakati fulani watu wenye kutumaini mema walifikiri kwamba kufikia sasa hakungekuwa tena na tisho la magonjwa mabaya ya kuambukiza.” Hata hivyo, gazeti hilo linaongeza kwamba “magonjwa ya kuambukiza bado yako na yanaendelea kuibuka tena na tena.” Gazeti Nature la Julai 8, 2004, linataja matokeo haya: “Inakadiriwa kwamba watu milioni 15 hivi . . . hufa kila mwaka kutokana na magonjwa ya kuambukiza.”

Gazeti Nature linasema kwamba “kutokea kwa UKIMWI kumewakumbusha watu kwamba magonjwa ya kuambukiza hayawezi kuepukika nayo yana madhara.” Shirika la UNAIDS, programu ya UKIMWI inayodhaminiwa na Umoja wa Mataifa na vikundi vingine, linaripoti kwamba “inakadiriwa kuwa kati ya mwaka wa 2000 na 2020, watu milioni 68 katika nchi 45 zilizoathiriwa zaidi watakufa mapema kutokana na UKIMWI.”

Katika miaka 25 iliyopita, UKIMWI umekuwa tauni mbaya ambayo imeua watu zaidi ya milioni 20. Lakini tauni ya homa ya Hispania ilisababisha madhara na vifo vya mamilioni katika muda wa mwaka mmoja hivi. Lakini sasa kulingana na maonyo mengi ambayo yametolewa, ulimwengu unakabili tisho la kutokea kwa homa mbaya ambayo ulimwengu hauko tayari kukabiliana nayo.

Katika Mei 19, 2005, Shirika la Habari la Reuters la Kutahadharisha Watu lilionya kuhusu kuendelea kutokea kwa virusi vipya vya homa, na likaongeza kusema kwamba virusi hivyo “bado ni tisho kubwa la kutokea kwa tauni kubwa.” Gazeti The Wall Street Journal la Mei 18, 2005 lilikuwa limesema: “Virusi vya homa ya ndege ambavyo sasa viko Asia vinaitwa H5N1 na vilionekana mara ya kwanza katika masoko ya kuku huko Hong Kong mnamo 1997. Homa hiyo ni mbaya sana kwani huua asilimia 80 hivi ya wale wanaoambukizwa.” Inasemekana kwamba virusi hivyo huambukizwa watu wanaoishi na wanyama walioambukizwa.

Je, Kuna Tumaini Zuri la Wakati Ujao?

Huenda tusiwe na matarajio mazuri ya wakati ujao. Yesu Kristo alipotaja tauni katika siku za mwisho, bila shaka alionyesha kwamba tuna sababu ya kuhangaika. Hata hivyo, Biblia pia hutupa tumaini. Kwa mfano, Mungu alitoa ahadi kwa Noa na familia yake kabla ya Gharika ya ulimwenguni pote. Kwanza, alimwonya Noa kuhusu uharibifu uliokuwa unakaribia, lakini akamwagiza Noa ajenge safina ambapo yeye na wengine wangelindwa. (Mwanzo 6:13, 14; 7:1) Mtume Petro alisema kwamba ‘subira ya Mungu ilikuwa ikingoja katika siku za Noa, safina ilipokuwa ikijengwa,’ na wakati ujenzi ulipokamilika, waokokaji “walichukuliwa salama kupitia maji.”—1 Petro 3:20.

Yesu Kristo, ambaye alitabiri mambo mengi kuhusu hali za ulimwengu tunazoona leo, alisema kwamba siku zetu zinafanana na zile za Noa. Wale wanaomtumaini Mungu kama Noa wanatazamia kuokoka uharibifu mkubwa. (Luka 17:26, 27) Yohana, mtume wa Yesu aliandika hivi: “Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Kwa hiyo, mfumo wa ulimwengu uliopo utakwisha. Waokokaji wataishi maisha ya aina gani? Mtume Yohana alipewa maono haya kuhusu hali nzuri sana zitakazokuwapo duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu: “[Mungu] atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Unaweza kutarajia mema wakati ujao. Ukijifunza juu ya Mungu na kumtumaini kikamili, utakuwa na tumaini zuri la wakati ujao. Mungu anaahidi kwa uhakika kwamba katika ulimwengu wake mpya, wafu watafufuliwa. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Na tauni zitakwisha kabisa. Biblia inaahidi hivi kuhusu unabii utakaotimizwa katika ulimwengu huo mpya: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia inatoa ahadi kuhusu ulimwengu mpya ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa’”