Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yangu Yaniimarisha—Kuishi na Ugonjwa wa ALS

Imani Yangu Yaniimarisha—Kuishi na Ugonjwa wa ALS

Imani Yangu Yaniimarisha—Kuishi na Ugonjwa wa ALS

SIMULIZI LA JASON STUART

“Pole sana, Bw. Stuart. Una ugonjwa wa ‘amyotrophic lateral sclerosis,’ au ALS, unaoitwa pia ugonjwa wa Lou Gehrig.” * Kisha daktari akanielezea kwamba: Karibuni sitaweza kutembea au kuzungumza, na ugonjwa huo utaniua. “Nina muda gani wa kuishi?” nikamuuliza. “Labda miaka mitatu au mitano,” akajibu. Nilikuwa tu na umri wa miaka 20. Hata hivyo, licha ya habari hizo zenye kusikitisha, bado nilijihisi nimebarikiwa katika njia nyingi. Hebu nieleze.

NILIZALIWA Machi 2, 1978, huko Redwood City, California, Marekani. Nilikuwa mtoto wa tatu katika familia ya watoto wanne. Wazazi wangu, Jim na Kathy Stuart, walimpenda Mungu sana, nao walikazia maadili ya kiroho ndani yetu sote, mimi, Matthew, Jenifer, na Johnathan.

Kadiri ninavyoweza kukumbuka, ilikuwa kawaida kwa familia yetu kuhubiri nyumba kwa nyumba, kujifunza Biblia, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mazoezi hayo ya kiroho yalinisaidia kujenga imani yenye nguvu katika Yehova Mungu. Sikutambua kwamba imani yangu ingejaribiwa.

Tamaa Yangu Nikiwa Mvulana Yatimia

Mnamo 1985, baba alitupeleka kutembelea Betheli ya Brooklyn, huko New York, ambayo ndiyo makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka saba tu, nilihisi kwamba Betheli palikuwa pahali pa pekee. Wote walifurahia kazi waliyofanya. Nilijiambia hivi, ‘Nitakapokuwa mkubwa nitakuja Betheli nisaidie kumtengenezea Yehova Biblia.’

Oktoba 18, 1992, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Miaka michache baadaye, nilipokuwa na umri wa miaka 17, baba alinipeleka Betheli tena. Kwa kuwa sasa nilikuwa na umri mkubwa zaidi, ningeweza kuelewa zaidi umuhimu wa kazi iliyofanywa huko. Nilirudi nyumbani nikiwa nimeazimia kabisa kufikia mradi wangu wa kwenda Betheli.

Mnamo Septemba 1996, nilianza kutumika nikiwa painia wa kawaida, au mweneza injili wa wakati wote. Ili nisikengeuke kutoka kwenye mradi wangu, nilijihusisha kabisa na mambo ya kiroho. Niliongeza muda wa kusoma Biblia na wa funzo la kibinafsi. Usiku nilisikiliza hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Baadhi ya hotuba hizo zilitaja mambo yaliyoonwa ya Wakristo ambao walikuwa wamekabili kifo wakiwa na imani thabiti katika ufufuo na Paradiso inayokuja. (Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Baada ya muda ningeweza kukumbuka hotuba zote. Sikujua kwamba habari hizo zingenifaidi sana katika siku za usoni.

Julai 11, 1998, nilipata barua kutoka Brooklyn. Naam, nilikuwa nimekaribishwa Betheli. Mwezi mmoja baadaye nilikuwa katika chumba changu cha Betheli. Nilipewa mgawo katika idara ya kujalidi vitabu, ambapo tulitengeneza vitabu vilivyosafirishwa kwa makutaniko mengi. Tamaa yangu ya utotoni ilikuwa imetimia. Nilikuwa Betheli, ‘nikitengeneza Biblia kwa ajili ya Yehova’!

Napatwa na Ugonjwa

Hata hivyo, mwezi mmoja kabla ya kwenda Betheli, niligundua kwamba singeweza kunyoosha kabisa kidole changu cha shahada. Karibu na wakati huo, nilichoka haraka nilipofanya kazi yangu ya kusafisha vidimbwi vya kuogelea. Nilijiambia kwamba sikuwa nikijitahidi sana. Isitoshe, kabla ya hapo nilikuwa nimefanya kazi ngumu zaidi bila shida yoyote.

Baada ya kukaa majuma machache Betheli, dalili zilizidi kuwa mbaya. Singeweza kukimbizana na vijana wengine walipopanda na kuteremka ngazi. Kazi yangu katika idara ya kujalidi vitabu ilitia ndani kuinua mabunda ya vitabu. Nilichoka haraka na vilevile mkono wangu wa kulia ulianza kujipinda. Pia, msuli wa kidole changu cha gumba ulianza kudhoofika na baada ya muda singeweza kusogeza kidole hicho hata kidogo.

Katikati ya Oktoba, miezi miwili baada ya kufika Betheli, daktari aliniambia kwamba nilikuwa na ugonjwa wa ALS. Nilipotoka kwenye ofisi ya daktari, mara moja nilianza kukumbuka hotuba za Biblia ambazo nilikuwa nimeweka akilini. Lazima roho ya Yehova ilikuwa pamoja nami kwani sikuogopeshwa na wazo la kufa. Nilienda tu nje na kungoja gari la kunirudisha Betheli. Nilisali kwamba Yehova aimarishe familia yangu wakati ambapo ningewaeleza habari hizo.

Kama nilivyotaja mwanzoni, nilijihisi kuwa nimebarikiwa. Ndoto yangu tangu utotoni ya kwenda Betheli ilikuwa imetimia. Jioni hiyo nilitembea kwenye Daraja la Brooklyn, nami nilimshukuru Yehova kwa kuniruhusu nitimize mradi wangu. Nilimwomba pia anisaidie kukabiliana na jambo hilo lenye kuogofya.

Marafiki wengi walipiga simu ili kunitegemeza na kunitia moyo. Nilijaribu kuwa mchangamfu na kuzungumzia mambo yanayofaa. Hata hivyo, juma moja baada ya kuambiwa mambo hayo na daktari, nilipokuwa nikizungumza na mama kwenye simu, aliniambia kwamba ninafanya vizuri kujikaza lakini pia aliniambia kuwa hakuna ubaya kulia. Kabla hajamaliza kusema hivyo nilianza kulia. Ghafula nilitambua kwamba ningepoteza kila kitu nilichokuwa nimetamani tangu utotoni.

Mama na Baba walitaka sana niende nyumbani, hivyo ghafula asubuhi moja mwishoni mwa Oktoba walikuwa mlangoni. Siku chache zilizofuata niliwatembeza Betheli na kuwajulisha kwa marafiki wangu kutia ndani washiriki wa Betheli wenye umri mkubwa waliokuwa wametumika huko kwa muda mrefu. Siku hizo ambazo nilikaa Betheli pamoja na wazazi wangu ni kati ya siku ninazokumbuka kwa furaha zaidi.

Kuhesabu Baraka Zangu

Tangu wakati huo, Yehova amenibariki kwa njia nyingi. Mnamo Septemba 1999, nilitoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote. Nilitoa hotuba nyingine kadhaa katika makutaniko mbalimbali, lakini baada ya muda ilikuwa vigumu sana kuongea vizuri hivi kwamba nililazimika kuacha kutoa hotuba za watu wote.

Baraka nyingine imekuwa upendo na utegemezo usiokoma ambao nimepata kutoka kwa familia yangu na pia ndugu na dada zangu wa kiroho. Miguu yangu ilipoanza kuwa dhaifu, marafiki walinishika mkono na kunisaidia kutembea kwenda kwenye utumishi. Wengine hata walikuja nyumbani na kusaidia kunitunza.

Kati ya baraka kubwa zaidi ambazo nimepata ni mke wangu, Amanda. Tulianza kuwa marafiki niliporudi nyumbani kutoka Betheli, nami nilivutiwa na ukomavu wake wa kiroho. Nilimwambia kila kitu kuhusu ugonjwa wangu wa ALS na mambo ambayo daktari alikuwa amesema. Mara nyingi tulienda pamoja katika utumishi kabla ya kuanza uchumba. Tulifunga ndoa Agosti 5, 2000.

Amanda anaeleza hivi: “Nilivutiwa na Jason kwa sababu ya upendo wake kwa Mungu na bidii yake kwa ajili ya mambo ya kiroho. Watu walivutiwa naye kwa urahisi, vijana kwa wazee. Mimi ni mnyamavu, naye ni mchangamfu sana, na hata haogopi watu. Sisi sote hupenda kufanya ucheshi, kwa hiyo tulicheka mara nyingi pamoja. Sikuwa na wasiwasi wowote nilipokuwa naye, ni kana kwamba tumefahamiana kwa muda mrefu. Jason alihakikisha kwamba nilielewa kabisa ugonjwa wake na mambo ambayo yangempata. Lakini nilijiambia kwamba tungefurahia kipindi ambacho sote tungekuwa hai. Isitoshe, huwezi kujua mambo yatakuwaje katika mfumo huu wa mambo. ‘Wakati na tukio lisilotazamiwa’ huwapata hata wale wenye afya nzuri.”—Mhubiri 9:11.

Kutafuta Njia za Kuwasiliana

Usemi wangu ulipoacha kueleweka, Amanda alianza kutafsiri mambo niliyokuwa nikisema. Nilipopoteza kabisa uwezo wa kusema, tulibuni njia ya pekee ya kuwasiliana. Amanda husema herufi za alfabeti, na anaposema herufi ninayotaka, mimi hupepesa macho yangu. Yeye hukumbuka herufi hiyo na tunaendelea na herufi inayofuata. Kwa njia hiyo mimi huunda sentensi nzima. Mimi na Amanda tumezoea sana kuwasiliana kwa njia hiyo.

Kwa sababu ya teknolojia ya kisasa, nina kompyuta ambayo hunisaidia kuwasiliana. Mimi huchapa ninachotaka kusema, na sauti ya kompyuta husema nilichochapa. Kwa kuwa siwezi kutumia mikono yangu, nuru fulani ya infrared imeelekezwa kwenye shavu langu nayo huhisi wakati wowote ninapolisogeza. Sanduku iliyo na alfabeti hutokea kwenye kona ya kompyuta. Kwa kusogeza shavu ninaweza kuchapa herufi yoyote na hivyo kuchapa maneno.

Kwa kutumia kompyuta hiyo, ninaweza kuwaandikia barua watu wanaopendezwa na Biblia ambao mke wangu hukutana nao katika utumishi. Kwa kutumia sauti yangu ya kompyuta, ninaweza kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kutumia njia hizo nimefaulu kuendelea kutumika kama painia wa kawaida. Hivi karibuni nimeweza tena kutoa hotuba na migawo mingine ya kufundisha katika kutaniko, ambako ninatumika kama mtumishi wa huduma.

Kuendelea Kuwa Mcheshi

Tumepatwa na mambo fulani yenye kuhuzunisha. Kadiri miguu yangu inavyozidi kuwa minyonge ndivyo ninavyoanguka mara kwa mara. Nimeanguka na kuumia kichwa zaidi ya mara moja. Misuli yangu huacha kunyumbulika, kwa hiyo nyakati nyingine mimi huanguka kama mti. Hilo hufanya watu washtuke na kukimbia ili wanisaidie. Lakini mara nyingi mimi hutoa ucheshi ili kuwatuliza. Sikuzote nimejaribu kuwa mcheshi. Hakuna kitu kingine cha kufanya. Kungekuwa na faida gani ikiwa ningekasirika kwa sababu ya jinsi maisha yanavyozidi kuwa magumu?

Usiku mmoja mimi na Amanda tulipokuwa tumeenda matembezi pamoja na marafiki wawili, nilianguka ghafula kwa nyuma na kugonga kichwa chini. Nakumbuka nyuso tatu zenye wasiwasi zikinitazama nikiwa chini na mmoja wa rafiki zetu akiuliza ikiwa nilikuwa sawa.

Nilijibu, “Ndiyo, lakini ninaona nyota.”

“Kweli?” akauliza.

“Kweli, tazama,” nikajibu nikimwonyesha angani. “Ni maridadi.” Kila mtu aliangua kicheko.

Kukabiliana na Magumu ya Kila Siku

Misuli yangu ilipozidi kudhoofika, nilianza kukabili magumu mengi zaidi. Ilianza kuwa vigumu kufanya mambo rahisi ya kila siku, kama vile, kula, kuoga, kwenda haja, au kufungua vifungo vya nguo zangu. Sasa hali yangu imedhoofika sana hivi kwamba siwezi kusonga, kuzungumza, kula, au kupumua bila msaada. Nina mrija unaoingia tumboni ambao hutumiwa kunilisha chakula cha umajimaji. Kuna mrija mwingine ulioingizwa ndani ya koo langu ambao huniwezesha kupumua.

Ingawa niliazimia kujitegemea kadiri niwezavyo, Amanda alikuwa tayari nyakati zote kunisaidia. Hajawahi kunifanya nijihisi kuwa bure ingawa nimelazimika kuwategemea wengine. Nyakati zote amenifanya nijiheshimu. Yeye hufanya kazi nyingi kunitunza, nami najua kwamba si rahisi kufanya hivyo.

Amanda anaeleza jinsi anavyohisi: “Ugonjwa wa Jason umemdhoofisha hatua kwa hatua, hivyo nimejifunza jinsi ya kumtunza hatua kwa hatua. Kwa kuwa anahitaji msaada kupumua, lazima atunzwe kila dakika. Kikohozi na mate hujikusanya kwa wingi ndani ya mapafu yake, nayo lazima yavutwe kwa kifaa fulani. Kwa hiyo, ni vigumu kwetu kupata usingizi mzuri usiku. Nyakati nyingine mimi hujihisi mpweke nami huvunjika moyo. Ingawa sisi huwa pamoja nyakati zote, ni vigumu kuwasiliana. Alikuwa mtu mchangamfu, lakini sasa ni macho tu yaliyo machangamfu. Bado yeye ni mcheshi sana, na akili yake iko chonjo. Lakini mimi hutamani sana kusikia sauti yake, kukumbatiwa na kushikwa mkono naye.

“Nyakati nyingine watu huniuliza jinsi mimi huvumilia hali hiyo. Hali hiyo imenifundisha kwamba ninahitaji kumtegemea Yehova kabisa. Ninapojitegemea, mimi huhisi kana kwamba nimekazwa sana hata siwezi kupumua. Sala husaidia, kwani Yehova tu ndiye anayenielewa kikweli naye anaelewa mambo ninayokabiliana nayo. Wazazi wa Jason wametusaidia sana. Wao huwapo wakati wowote ninapohitaji kupumzika au ninapotaka kwenda utumishi wa shambani. Mimi huthamini msaada na utegemezo ambao tumepokea kutoka kwa ndugu na dada wa kutaniko letu. Jambo jingine ambalo hunisaidia ni kukumbuka kwamba kuteseka kokote katika mfumo huu ni kwa ‘dakika na ni kwepesi.’ (2 Wakorintho 4:17) Mimi hujaribu kukazia macho ulimwengu mpya unaokuja, ambapo Yehova atasuluhisha kila jambo. Huenda nitacheka na kulia wakati uleule wakati mkazo huu wote utakapopotelea mbali na Jason atakuwa Jason tena.”

Kupigana na Kushuka Moyo

Nyakati nyingine inavunja moyo nikiwa mwanamume kuketi katika gari hili la magurudumu na huku sijiwezi. Ninakumbuka wakati mmoja tulikuwa kwenye nyumba ya dadangu kwenye kikusanyiko cha familia. Sikuwa nimekula hivyo nilihisi njaa. Kila mtu alikuwa akila nyama zilizokaangwa na kutiwa katikati ya mikate pamoja na mahindi. Nilipowatazama wakila na kucheza na watoto, nilishuka moyo sana. Nilianza kufikiri: ‘Ole wangu! Kwa nini ni lazima nikose mambo haya?’ Sikutaka kuwaharibia wengine jioni hiyo nzuri, hivyo nilimsihi Yehova anisaidie nisitoe machozi.

Nilijikumbusha kwamba kwa kuendelea kuwa mwaminifu ninaweza kumpa Yehova nafasi ya ‘kumjibu Shetani anayemdhihaki.’ (Methali 27:11) Hilo lilinipa nguvu, kwani nilitambua kwamba kuna mambo mengi muhimu zaidi kuliko kula mahindi au kucheza na watoto.

Ninafahamu kabisa jinsi ilivyo rahisi kwa mgonjwa kama mimi kuhangaikia matatizo yake kupita kiasi. Lakini nimepata msaada kwa sababu ya kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Kwa sababu ya kujishughulisha na utumishi, sina wakati wa kuhangaikia matatizo yangu. Kuwasaidia wengine wasitawishe imani katika Yehova kumenisaidia nipate furaha.

Kuna jambo jingine ambalo limenisaidia kukabiliana na kushuka moyo. Mimi hufikiria mambo yaliyoonwa ya akina ndugu waaminifu ambao walifungwa gerezani, wengine katika kifungo cha upweke, kwa sababu walikataa kuacha kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Mimi huwazia kwamba chumba changu ni jela na kwamba nimefungwa kwa sababu ya imani yangu. Mimi hufikiria mambo ninayoweza kufanya na ambayo baadhi ya ndugu hao hawawezi. Ninaweza kupata vichapo vya Biblia. Ninaweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kusikiliza mikutano hiyo kupitia simu. Niko huru kuendelea na utumishi wangu. Mke wangu mpendwa hufanya nisihisi upweke. Kutafakari mambo hayo hufanya nithamini jinsi nilivyobarikiwa.

Maneno haya ya mtume Paulo hunigusa moyo sana: “Kwa hiyo hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku.” Bila shaka ninaendelea kuchakaa kwa nje. Lakini nimeazimia kutokufa moyo. Kinachonipa nguvu ni kuendelea kukaza macho yangu juu ya “vitu visivyoonekana,” kutia ndani baraka za ulimwengu mpya unaokuja, ambako ninajua kwamba Yehova atanifanya niwe kamili tena.—2 Wakorintho 4:16, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ili kuelewa ugonjwa huu, inapendekezwa usome sanduku, “Habari Kuhusu ALS,” kwenye ukurasa wa 27.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Habari Kuhusu ALS

ALS ni nini? ALS (amyotrophic lateral sclerosis) ni ugonjwa ambao huenea haraka na kuvamia chembe za neva katika uti wa mgongo na sehemu ya chini ya ubongo. Chembe hizo za neva hutumika kusambaza habari kutoka kwenye ubongo hadi kwenye misuli mbalimbali mwilini. ALS hufanya chembe za mwili ziharibike au zife, na hilo humfanya mtu apooze polepole. *

Kwa nini ALS huitwa pia ugonjwa wa Lou Gehrig? Lou Gehrig alikuwa mchezaji maarufu wa besiboli wa Marekani ambaye alipatikana na ugonjwa wa ALS mnamo 1939 na akafa mwaka wa 1941 akiwa na umri wa miaka 38. Katika nchi fulani ALS huitwa ugonjwa wa mfumo wa neva. Lakini kuna magonjwa mengi ya mfumo wa neva na ALS ni moja kati ya hayo. Nyakati nyingine, ALS huitwa ugonjwa wa Charcot, jina la Mfaransa Jean-Martin Charcot, mtaalamu wa chembe za neva ambaye alifafanua ugonjwa huo kwa mara ya kwanza mnamo 1869.

Ni nini husababisha ALS? Haijulikani kinachosababisha ALS. Kulingana na watafiti, huenda ugonjwa huo husababishwa na virusi, upungufu wa protini, kasoro za chembe za urithi (hasa katika familial ALS), madini mazito mwilini, sumu zinazodhuru mfumo wa neva, (hasa katika Guamanian ALS), kasoro za mfumo wa kinga, na kasoro za vimeng’enya.

Matumaini ya kupona. Kadiri ugonjwa unavyoenea, ndivyo misuli mbalimbali mwilini huanza kudhoofika na kuharibika. Katika hatua zake za mwisho ugonjwa huo hudhoofisha misuli ya mfumo wa kupumua, na mwishowe lazima wagonjwa watumie kifaa cha kuwasaidia kupumua. Kwa kuwa ugonjwa huo huathiri tu chembe za neva, haudhuru akili, utu, uwezo wa kufikiri, au kumbukumbu ya mgonjwa. Wala hauathiri hisi za wagonjwa kwani wanaweza kuona, kunusa, kuonja, kusikia, na kuhisi wanapoguswa. Mara nyingi watu wanaougua ALS hufa miaka mitatu hadi mitano baada ya kuonyesha dalili za kwanza, lakini huenda asilimia 10 hivi ya wagonjwa wakaendelea kuishi kwa miaka kumi au zaidi.

Kutibu ugonjwa huo. Hakuna tiba ya ALS. Huenda daktari akapendekeza dawa za kupunguza maumivu. Ikitegemea dalili na hatua za ugonjwa, mgonjwa anaweza kufanyiwa mazoezi fulani, kutia ndani mazoezi ya viungo, kukandwa, kumzoeza kufanya utendaji wa kila siku, mazoezi ya kusema, na kupewa vifaa maalumu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 48 Kuna aina tatu za kawaida za ALS: sporadic, yaani, hutukia tu bila sababu yoyote (ya kawaida zaidi), familial, yaani, hupitishwa kwa kurithi (asilimia 5 hadi 10 hivi hutokea kwa sababu ya kuambukizwa kwa chembe za urithi), na Guamanian (visa vingi vimetokea huko Guam na katika maeneo ya Pasifiki yaliyo chini ya Umoja wa Mataifa).

[Hisani]

Lou Gehrig: Photo by Hulton Archive/Getty Images

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kutembelea Betheli mnamo 1985

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Mimi na Amanda siku yetu ya arusi

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kompyuta fulani ya pekee hunisaidia kuwasiliana

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Mimi hufurahia kutoa hotuba katika kutaniko letu