Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Utegemee Mwongozo wa Biblia?

Kwa Nini Utegemee Mwongozo wa Biblia?

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Utegemee Mwongozo wa Biblia?

“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

WEWE hutafuta wapi mwongozo? Leo kuna mashauri chungu nzima kuhusu karibu kila jambo. Hata hivyo, watu wengi hutegemea mwongozo wa kitabu cha zamani, Biblia.

Hata hivyo, wengi huiona Biblia kuwa yenye thamani ndogo, hasa wakati huu ambapo watu wanaweza kupata habari nyingi kwa kutumia kompyuta na teknolojia ya kisasa. Walimu na wanasayansi fulani mashuhuri wanaunga mkono wazo la kwamba Biblia haifai tena. Je, maoni yao ni sahihi? Kwa kuwa leo kuna vyanzo vingi sana vya mwongozo, kwa nini mtu aitegemee Biblia?

Kitabu cha Kweli

Pindi moja Yesu Kristo alipokuwa akipumzika karibu na kisima alizungumza na mwanamke Msamaria. Alimwambia hivi: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Maneno hayo yanaonyesha kwamba kuna ibada fulani inayokubalika na Mungu. Ili tuweze kumwabudu Mungu kwa kweli, lazima ibada yetu ipatane na mambo ambayo Mungu amefunua juu yake katika Biblia. Neno la Mungu lina kweli.—Yohana 17:17.

Hata hivyo, kuna dini nyingi zinazodai kuwa zinaamini Biblia, na inaonekana kwamba kila moja hufunza mambo yaliyo tofauti. Kwa sababu hiyo, kuna mvurugo mwingi kuhusu yale ambayo Biblia inafundisha hasa. Je, Yesu ni Mungu, au yeye ni Mwana wa Mungu? Je, kweli kuna maisha baada ya kifo au la? Je, kweli kuna mahali penye moto wa mateso ambapo watu huteswa baada ya kufa? Je, Shetani ni mtu halisi? Kuwa Mkristo kunahusisha nini? Je, Mungu huona matendo na mawazo yetu kuwa muhimu? Je, mtu anapaswa kufanya ngono kabla ya ndoa ili kuthibitisha upendo wa kweli? Je, ni kosa kunywa vileo? * Dini kadhaa hudai kuwa zinafundisha ukweli kuhusu mambo hayo. Lakini mara nyingi imani hizo za kidini hupingana. Yote hayawezi kuwa ya kweli.—Mathayo 7:21-23.

Basi unawezaje kujua kweli kumhusu Mungu na namna ya ibada inayompendeza? Tuseme umegundua kwamba unahitaji kufanyiwa upasuaji ili kutibu ugonjwa fulani mbaya. Ungefanya nini? Labda ungechagua kwa makini daktari anayejulikana kuwa bora zaidi kufanya upasuaji huo. Ungefikiria sifa zake za ustahili, umwone, na kuzungumza naye. Mwishowe, baada ya kusadiki kwamba yeye ndiye daktari bora zaidi kwa sababu ya habari ulizopata, unamtumaini na kukubali akufanyie upasuaji. Huenda wengine wakawa na maoni tofauti. Lakini wewe una sababu nzuri za kumwamini kabisa daktari huyo.

Kwa njia hiyo, ukichunguza kwa unyoofu uthibitisho uliopo, unaweza kumwamini Mungu na Biblia. (Methali 2:1-4) Una uhuru wa kutafuta majibu kuhusu ibada inayokubalika na Mungu. Unaweza kutegemea mafundisho na mawazo ya wanadamu yasiyopatana, au unaweza kuchunguza maoni ya Biblia.

Ni Sahihi na Inafaa

Ukichunguza Biblia kwa makini utaona kwamba kuna uthibitisho wa kutosha kuwa “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” * (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa mfano, Biblia ina unabii wenye habari nyingi. Historia inathibitisha kwamba unabii mwingi ulitimizwa. (Isaya 13:19, 20; Danieli 8:3-8, 20-22; Mika 5:2) Ingawa Biblia si kitabu cha sayansi, ni sahihi kisayansi. Ina habari kuhusu mambo ya asili na afya ambayo yaliandikwa maelfu ya miaka kabla wanasayansi kuyagundua.—Mambo ya Walawi 11:27, 28, 32, 33; Isaya 40:22.

Isitoshe, Biblia hutusaidia kufanya maamuzi ya hekima. Ina mashauri mengi mazuri kuhusu maisha ya familia, afya ya kimwili na ya kihisia, biashara, na shughuli nyingine za kila siku. Methali 2:6, 7 inasema: “Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi. Naye atawawekea wanyoofu hazina ya hekima inayotumika.” Kwa kutegemea mwongozo wa Biblia, unaweza kuzoeza nguvu zako za ufahamu “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.”—Waebrania 5:14.

Pia Neno la Mungu hutusaidia kuelewa kusudi la maisha. (Yohana 17:3; Matendo 17:26, 27) Linaeleza kuhusu hali za ulimwengu. (Mathayo 24:3, 7, 8, 14; 2 Timotheo 3:1-5) Biblia hutuonyesha jinsi Mungu atakavyoondoa uovu duniani na kuwawezesha wanadamu wapate afya nzuri na uzima wa milele.—Isaya 33:24; Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4.

Mamilioni ya watu wameshuhudia moja kwa moja kwamba kwa kweli Biblia ina mashauri ya hekima yanayotegemeka na kutumainika. Wachapishaji wa Amkeni! wanakualika uchunguze mfululizo wa makala zenye kichwa “Maoni ya Biblia,” ambazo zitakuwa zikichapishwa katika kila toleo la gazeti hili. Kwa kufanya hivyo, huenda ukapata uthibitisho zaidi kwamba Biblia ndiyo hutoa mwongozo bora zaidi kwa maisha yako.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Mungu hukubali ibada ya aina gani?—Yohana 4:24.

▪ Unapaswa kufanya nini ili unufaishwe na hekima ya Mungu?—Methali 2:1-4.

▪ Biblia hutoa mwongozo unaotumika katika njia gani?—Waebrania 5:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Maswali hayo na mengine mengi yatazungumziwa katika matoleo yajayo ya gazeti Amkeni! katika makala “Maoni ya Biblia” yanayochapishwa kwa ukawaida.

^ fu. 12 Ili kupata uthibitisho kwamba Biblia iliandikwa chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.