Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Wasomaji Wetu

Kwa Wasomaji Wetu

Kwa Wasomaji Wetu

KUANZIA toleo hili, gazeti Amkeni! litakuwa na mabadiliko fulani. Ingawa mambo fulani yatabadilishwa, sehemu kubwa itabaki vile ilivyokuwa.

Bado Amkeni! lina lengo lilelile ambalo limekuwa nalo kwa miaka mingi. Kama inavyoelezwa katika ukurasa wa 4, “gazeti hili huchapishwa ili kuelimisha familia nzima.” Kwa kuchunguza matukio ya ulimwengu, kuzungumzia kuhusu utamaduni mbalimbali, kueleza maajabu ya uumbaji, kuzungumzia mambo ya afya, au kueleza mambo ya sayansi kwa wale wasio na ujuzi wa sayansi, Amkeni! litaendelea kuwaelimisha wasomaji wetu, likiwafahamisha kuhusu matukio ya ulimwengu.

Katika toleo lake la Agosti 22, 1946, Amkeni! liliahidi hivi: “Gazeti hili litaazimia kushikamana kwa uthabiti na ukweli.” Kulingana na azimio hilo, sikuzote Amkeni! limejitahidi kuchapisha habari sahihi. Ili kufanya hivyo, makala hufanyiwa utafiti sana na kuchunguzwa kwa makini ili kuhakikisha kwamba ni sahihi. Lakini jarida hili ‘hushikamana kwa uthabiti na ukweli’ katika njia nyingine muhimu zaidi.

Sikuzote Amkeni! limewaelekeza wasomaji kwenye Biblia. Hata hivyo, kuanzia toleo hili, Amkeni! litakuwa na makala nyingi zaidi zinazotegemea Biblia kuliko ilivyokuwa zamani. (Yohana 17:17) Amkeni! pia litaendelea kuchapisha makala zinazoonyesha jinsi shauri la Biblia linavyoweza kutusaidia kufanikiwa na kuwa na kusudi maishani leo. Kwa mfano, mwongozo wa Biblia hutolewa kupitia makala “Vijana Huuliza . . . ” na “Maoni ya Biblia.” Makala hizo bado zitaendelea kuchapishwa kwa ukawaida katika gazeti hili. Pia Amkeni! litaendelea kuwaelekeza wasomaji kwenye ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya wenye amani ambao hivi karibuni utachukua mahali pa mfumo wa mambo wa sasa usiotii sheria.—Ufunuo 21:3, 4.

Ni jambo gani jingine litakalokuwa tofauti? Kuanzia toleo hili, Amkeni! litakuwa likichapishwa mara moja kwa mwezi katika nyingi za lugha 82 ambazo hilo huchapishwa (zamani lilikuwa likichapishwa mara mbili kwa mwezi katika lugha nyingi). * Makala “Kuutazama Ulimwengu” ambayo imekuwa ikichapishwa kwa ukawaida tangu 1946, itaendelea kuchapishwa katika kila toleo lakini sasa itapunguzwa kutoka kurasa mbili hadi moja. Kwenye ukurasa wa 31 tutaanza kuchapisha kwa ukawaida makala mpya yenye kichwa “Ungejibuje?” Itakuwa na mambo gani, na unaweza kuitumiaje?

Hebu tazama ukurasa wa 31 kwenye toleo hili. Sehemu fulani za ukurasa huu zitawavutia wasomaji wachanga; nyingine zitachangamsha akili za watu wenye ujuzi zaidi wa Biblia. Sehemu, “Ilitukia Lini?” itakusaidia uwe na chati ya tarehe inayoonyesha kipindi cha wakati ambacho watu wanaotajwa katika Biblia waliishi na mambo muhimu yaliyotukia wakati huo. Ingawa majibu ya sehemu “Kutoka Katika Toleo Hili” yatapatikana katika gazeti lote, majibu ya mengi ya maswali yatachapishwa yakiwa juu-chini katika ukurasa fulani. Mbona usifanye utafiti fulani kabla ya kusoma majibu hayo kisha uwaeleze wengine yale ambayo umejifunza? Unaweza pia kuzungumzia sehemu hii mpya, “Ungejibuje?” ukiwa na familia yako au na kikundi chochote unachoshirikiana nacho.

Miaka 60 hivi iliyopita, Amkeni! liliahidi hivi: “Gazeti hili litajitahidi kuandika habari kutoka sehemu zote za ulimwengu. Litavutia watu wanyoofu kutoka nchi zote. . . . Habari zilizomo kwenye gazeti hili . . . zitakuwa zenye kuarifu, kuelimisha, na kupendeza watu wengi, wachanga kwa wazee.” Wasomaji wa gazeti hili kutoka sehemu mbalimbali za dunia wanakubali kwamba Amkeni! limetimiza ahadi yake. Tunawahakikishia kwamba litaendelea kufanya hivyo.

Wachapishaji

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Amkeni! huchapishwa mara moja baada ya kila miezi mitatu katika lugha fulani na huenda makala zilizotajwa katika barua hii zisiwepo katika matoleo hayo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Liliitwa “The Golden Age” mwaka wa 1919, kisha jina hilo likabadilishwa kuwa “Consolation” mnamo 1937, na kuwa “Awake!” mnamo 1946

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kwa muda mrefu, gazeti “Amkeni!” limewaelekeza wasomaji wake kwenye Biblia

[Hisani]

Guns: U.S. National Archives photo; starving child: WHO photo by W. Cutting