Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa nini mimi hujiumiza?

Kwa nini mimi hujiumiza?

Vijana Huuliza . . .

Kwa nini mimi hujiumiza?

“Nilikata viwiko vyangu vibaya sana hivi kwamba nilihitaji kushonwa. Wakati huo, nilimwambia daktari kwamba nimekatwa na balbu ya stima, jambo ambalo lilikuwa kweli, ni kwamba tu sikumtajia kuwa nilifanya hivyo kimakusudi.”—Sasha, 23.

“Wazazi wangu wameona majeraha yangu, lakini wameona tu yale ambayo si mabaya sana na ambayo yanaonekana kama mikwaruzo tu. . . . Nyakati nyingine wanaweza kuona jeraha fulani ambalo hawakuwa wameona, kwa hiyo mimi hutoa udhuru. . . . Sitaki wajue.”—Ariel, 13.

“Nilikuwa nikijiumiza tangu nilipokuwa na umri wa miaka 11. Nilijua Mungu anathamini sana mwili wa binadamu, lakini hilo halikunizuia nisijiumize.”—Jennifer, 20.

HUENDA ikawa unamjua mtu anayejiumiza kama Sasha, Ariel, au Jennifer. * Labda ni mwanafunzi mwenzako. Pengine ni ndugu au dada yako. Huenda ikawa ni wewe. Inakadiriwa kwamba nchini Marekani pekee, mamilioni ya watu, wengi wao wakiwa vijana, hujiumiza kimakusudi kwa njia mbalimbali kama vile kujikata-kata, kujichoma, kujichubua, au kukwaruza ngozi yao. *

Je, kweli watu hujiumiza kimakusudi? Zamani, watu wengi wangehusianisha zoea hilo na mtindo wa kiajabu-ajabu au na madhehebu fulani. Hata hivyo, hivi karibuni zoea hilo la kujiumiza au kujikata-kata limeanza kujulikana na watu wengi. Pia inaonekana kwamba wale walio na tatizo hilo wanazidi kujitokeza. Michael Hollander, mkurugenzi wa kituo cha matibabu huko Marekani anasema, “kila daktari anasema kwamba tatizo hilo linaongezeka.”

Si rahisi mtu afe kwa kujikata-kata, lakini ni hatari. Kwa mfano, mfikirie Beth. Anasema: “Ninapojiumiza, mimi hutumia wembe. Nimelazwa hospitalini mara mbili. Pindi moja, ilibidi nipelekwe haraka hospitalini ili kupata matibabu ya dharura kwa sababu ya kujikata sana.” Sawa na watu wengi walio na tatizo hilo, Beth aliendelea kujikata-kata hadi alipokuwa mtu mzima. Anasema: “Nimekuwa nikijikata-kata tangu nilipokuwa na umri wa miaka 15, na sasa nina umri wa miaka 30.”

Je, wewe, au mtu fulani unayemjua ana tatizo hilo? Ikiwa ndivyo, usivunjike moyo. Unaweza kupata msaada. Katika toleo litakalofuata la Amkeni! tutazungumzia jinsi watu walio na tatizo hilo wanavyoweza kusaidiwa. * Hata hivyo, inafaa tuzungumzie watu walio na tatizo hilo na mambo ambayo huchangia tatizo hilo.

Watu Ambao Hujiumiza Ni wa Malezi Mbalimbali

Ni vigumu kusema kwamba watu ambao hujiumiza au kujikata-kata ni wa malezi fulani hususa au wana tabia fulani hususa. Wengine hutoka katika familia zenye matatizo; wengine hutoka katika familia zilizo imara na zenye furaha. Wengi hawafanyi vizuri shuleni, lakini wengine ni wanafunzi bora. Mara nyingi, watu ambao hujiumiza hawaonyeshi kwamba wana tatizo hilo, kwa sababu huwezi kujua mtu ana tatizo hilo kwa kumwangalia tu. Biblia inasema: “Hata katika kicheko moyo unaweza kuwa na maumivu.”—Methali 14:13.

Pia, watu hawajiumizi kwa kiwango kilekile. Kwa mfano, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba watu fulani hujikata-kata mara moja tu kwa mwaka, ilhali wengine hufanya hivyo mara mbili hivi kwa siku. Kwa kushangaza, idadi ya wanaume wanaojikata-kata inaongezeka kuliko ilivyodhaniwa. Hata hivyo, wasichana wanaobalehe ndio wenye tatizo hilo hasa.

Ingawa watu ambao hujiumiza wanatoka katika malezi mbalimbali, wengine wao wana tabia zinazofanana. Ensaiklopedia moja ya vijana inasema hivi: “Mara nyingi vijana ambao hujiumiza hujihisi kuwa hoi, huona ni vigumu kuwaeleza wengine hisia zao, huhisi upweke au kuwa hawapendwi, huwa na woga, na hawajiheshimu.”

Bila shaka, huenda watu fulani wakasema kwamba mambo hayo humpata kijana yeyote ambaye anakabili woga na wasiwasi wa kukua. Hata hivyo, mtu ambaye hujiumiza hukabiliana na pambano kali sana. Ikiwa mtu hawezi kumweleza rafiki anayemtumaini mambo yanayomsumbua, hilo linaweza kumfanya alemewe na mikazo ya shuleni, kazini, au mizozo inayotokea nyumbani. Mtu huyo huona kuwa hakuna suluhisho naye huhisi kwamba hana mtu wa kuzungumza naye. Yeye huhisi kwamba hawezi kukabiliana na mkazo huo. Mwishowe, anatambua jambo hili: Kwa kujiumiza, anaona ni kana kwamba anapata kitulizo cha aina fulani kutokana na mfadhaiko wa kihisia, na anahisi kwamba anaweza kuendelea na maisha yake, angalau kwa wakati huo.

Kwa nini mtu anayejikata-kata hujiumiza ili kupunguza mfadhaiko wa kihisia? Fikiria kinachotokea wakati unapokuwa kwenye chumba cha daktari ukisubiri kudungwa sindano. Anapojitayarisha kukudunga sindano, je, umewahi kujikuta ukijichuna ili tu kukengeusha fikira zako usihisi uchungu utakapodungwa sindano? Mtu anayejiumiza hufanya jambo kama hilo lakini kwa njia iliyo hatari zaidi. Mtu anayejiumiza huona kujikata kuwa njia ya kukengeusha fikira na ya kutuliza mfadhaiko wa kihisia. Mfadhaiko huo huwa mwingi sana hivi kwamba mtu huona ni afadhali kujiumiza. Labda hiyo ndiyo sababu iliyofanya mtu fulani aliye na zoea la kujiumiza aseme kwamba kujikata ni “dawa ya woga wangu.”

“Mbinu ya Kukabiliana na Mfadhaiko”

Huenda watu wasiofahamu tatizo hilo wakaona kujiumiza kuwa jaribio la kujiua. Lakini kwa kawaida hivyo sivyo ilivyo. “Kwa kawaida, watu hao wanajaribu tu kumaliza maumivu yao, si kujiua,” anaandika Sabrina Solin Weill, mhariri mkuu wa gazeti la matineja. Kwa hiyo, kitabu kimoja kinataja kujiumiza kuwa “‘njia ya kuokoa uhai’ badala ya njia ya kukatiza uhai.” Pia kinaita zoea hilo “mbinu ya kukabiliana na mfadhaiko.” Mfadhaiko wa aina gani?

Imeonekana kwamba watu wengi ambao hujiumiza wamepatwa na jambo fulani lenye kuhuzunisha, kama vile kutendewa vibaya walipokuwa wadogo au kupuuzwa. Wengine waliathiriwa na migogoro katika familia au uraibu wa kileo wa mzazi mmoja. Wengine wana matatizo ya kiakili.

Huenda kukawa na matatizo mengine pia. Kwa mfano, Sara alijitesa sana kwa sababu alitaka kufanya mambo kikamilifu lakini hakuweza. Ingawa alikuwa amefanya makosa mazito na kusaidiwa na wazee Wakristo, alihisi kuwa na hatia kubwa kwa sababu ya kupungukiwa kwake kila siku. “Nilihisi kwamba sipaswi kujibembeleza,” anasema Sara. “Niliona kujiumiza kuwa njia ya kujitia nidhamu. Njia yangu ya ‘kujitia nidhamu’ ilitia ndani kung’oa nywele zangu, kukata-kata viwiko na mikono yangu, kujipiga na kujikwaruza sana, kujiadhibu kwa kuweka mikono yangu ndani ya maji moto sana, kuketi nje bila koti wakati wa baridi kali sana, au kushinda njaa siku nzima.”

Sara aliona kujiumiza kuwa ishara ya kujichukia kabisa. Anasema: “Nyakati nyingine nilihisi kwamba Yehova amenisamehe makosa yangu, lakini sikutaka anisamehe. Nilitaka niteseke kwa kuwa nilijichukia sana. Ingawa nilijua kwamba Yehova hajawahi kufikiria kutengeneza mahali pa kuwatesa watu kama vile moto wa mateso unaofundishwa na Jumuiya ya Wakristo, nilitaka atengeneze mahali kama hapo kwa ajili yangu tu.”

“Nyakati za Hatari”

Huenda watu fulani wakashangaa kwa nini zoea hilo lenye kuhuzunisha limejulikana katika miaka ya karibuni tu. Hata hivyo, wanafunzi wa Biblia wanajua kwamba hizi ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hivyo, hawashangai kujua kwamba watu, kutia ndani vijana, wana tabia ambazo si rahisi kuzielewa.

Biblia inakiri kwamba “uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu.” (Mhubiri 7:7) Nyakati nyingine, magumu ya ujana pamoja na kupatwa na mambo yenye kuhuzunisha maishani yanaweza kumfanya mtu awe na zoea la kujiumiza. Huenda kijana anayehisi upweke na kuamini kwamba hana mtu wa kuzungumza naye akaamua kujikata ili kupata kitulizo. Lakini kitulizo chochote kinachotokana na kujiumiza ni cha muda mfupi. Punde si punde, matatizo hurudi, na mtu huanza kujiumiza.

Kwa kawaida, wale ambao hujiumiza hutaka kuacha zoea hilo lakini wanaona ni vigumu sana kuliacha. Wengine wamefauluje kuacha zoea la kujiumiza? Habari hiyo itazungumziwa katika makala “Vijana Huuliza . . .  Nitaachaje Kujiumiza?” katika toleo la Amkeni! la Februari 2006.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini vijana fulani huamua kujiumiza?

▪ Baada ya kusoma makala hii, je, unaweza kufikiria njia bora za kukabiliana na mfadhaiko?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Majina fulani katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 6 Kujiumiza si sawa na kujitoboa mwilini au kujichanja. Kwa kawaida, watu hufanya hivyo kama mtindo lakini si kwa sababu ya kuchochewa na hamu ya kufanya hivyo. Ona gazeti Amkeni! la Agosti 8, 2000, ukurasa wa 18-19.

^ fu. 9 Andiko la Mambo ya Walawi 19:28 linasema: “Msijikatekate mwili wenu kwa ajili ya nafsi iliyokufa.” Zoea hilo la kipagani ambalo yaonekana lilikusudiwa kuwatuliza miungu iliyodhaniwa kuwa inawasimamia wafu ni tofauti na zoea la kujiumiza linalozungumziwa hapa.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Hata katika kicheko moyo unaweza kuwa na maumivu.”—Methali 14:13

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Kwa kawaida, watu hao wanajaribu tu kumaliza maumivu yao, si kujiua”

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—2 Timotheo 3:1