Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

ITAKUWAJE miaka 10, 20, au 30 ijayo? Kwa kuwa katika kipindi hiki kuna ugaidi inaweza kuogopesha kufikiria wakati ujao utakuwaje. Kuna maendeleo makubwa ya kiteknolojia. Biashara ya kimataifa imefanya mataifa mengi yategemeane. Je, viongozi wa ulimwengu wataungana na kutokeza wakati ujao mzuri zaidi? Watu wengine wanasema itawezekana, wakitarajia kwamba kufikia mwaka wa 2015, viongozi wataweza kukomesha umaskini na njaa, kuzuia kuenea kwa UKIMWI, na kupunguza kwa asilimia 50 idadi ya watu wasio na maji safi na mfumo wa kuondoa maji machafu na takataka.—Ona sanduku “Tofauti Kati ya Kutarajia Mema na Kuona Mambo Kihalisi.”

Hata hivyo, mara nyingi matumaini ya wanadamu kuhusu wakati ujao yamekuwa ndoto tu. Kwa mfano, miaka mingi iliyopita, mtaalamu mmoja alisema kwamba kufikia mwaka wa 1984, wakulima wangekuwa wakilima sakafu ya bahari kwa kutumia trekta zinazosafiri chini ya maji; mwingine alisema kwamba kufikia mwaka wa 1995, magari yangekuwa na kifaa fulani cha elektroniki cha kuzuia yasigongane; naye mwingine akatabiri kwamba kufikia mwaka wa 2000, watu 50,000 hivi wangekuwa wakiishi na kufanya kazi katika anga za juu. Bila shaka, huenda ikawa wale waliotabiri mambo hayo wanaghairi. Mwandishi mmoja wa habari aliandika hivi: “Kupita kwa wakati hufanya watu wenye akili zaidi ulimwenguni waonekane kuwa wapumbavu wa mwisho.”

“Ramani” ya Kutuongoza

Watu hutabiri daima kuhusu wakati ujao, lakini nyakati nyingine wao huwazia mambo yasiyowezekana. Tunaweza kupata wapi maoni yenye kutegemeka kuhusu wakati ujao?

Fikiria mfano huu. Wazia kwamba unasafiri kwa basi katika nchi usiyoijua. Kwa kuwa uko ugenini, unaanza kuwa na wasiwasi. Huenda ukajiuliza, ‘niko wapi? Je, basi hili linaelekea mahali ninapoenda? Niko mbali kadiri gani kutoka mahali ninapoelekea?’ Kwa kutumia ramani sahihi na kwa kutazama ishara za barabarani, unaweza kupata majibu ya maswali yako.

Hali hiyo ni sawa na ya wengi ambao wana wasiwasi wanapofikiria wakati ujao. Wao hujiuliza, ‘tunaelekea wapi? Je, kweli tuko katika barabara inayoelekeza kwenye amani ya ulimwenguni pote? Ikiwa ndivyo, tutafika tunakoelekea lini?’ Biblia ni kama ramani inayoweza kutusaidia kujibu maswali hayo. Kwa kuisoma kwa makini na kwa kutazama mambo yanayotendeka katika mandhari ya ulimwengu, tunaweza kujifunza mengi kuhusu mahali tulipo na tunapoelekea. Hata hivyo, kwanza tunapaswa kufikiria jinsi matatizo yetu yalivyoanza.

Mwanzo Wenye Kusikitisha

Biblia inatuambia kwamba Mungu alipowaumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, walikuwa wakamilifu na kwamba aliwaweka katika paradiso. Adamu na Hawa waliumbwa waishi milele, si kwa miaka 70 au 80 tu. Mungu aliwaambia hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” Mungu alikusudia Adamu, Hawa, na watoto wao wafanye sehemu zote za dunia ziwe Paradiso.—Mwanzo 1:28; 2:8, 15, 22.

Adamu na Hawa walimwasi Mungu. Kwa sababu hiyo walipoteza makao yao ya kiparadiso. Isitoshe, miili na akili zao zilianza kuzorota polepole. Kila siku, Adamu na Hawa walikaribia kifo. Kwa nini? Kwa sababu kwa kumwasi Muumba wao, walitenda dhambi, na “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.”—Waroma 6:23.

Hatimaye Adamu na Hawa walikufa baada ya kupata wana na mabinti kadhaa. Je, watoto hao wangeweza kutimiza kusudi la Mungu la awali? La, kwa kuwa walikuwa wamerithi kutokamilika kutoka kwa wazazi wao. Kwa kweli, kuanzia kizazi kimoja hadi kingine, wazao wote wa Adamu wamerithi dhambi na kifo. Sisi pia tumerithi dhambi na kifo. Biblia inasema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 3:23; 5:12.

Kutambua Mahali Tulipo Sasa

Uasi wa Adamu na Hawa ulikuwa mwanzo wa safari ndefu na yenye kuhuzunisha ya wanadamu ambayo imeendelea hadi leo. Kama mwandikaji mmoja wa Biblia alivyosema, wanadamu ‘wametiishwa chini ya ubatili.’ (Waroma 8:20) Andiko hilo linafafanua vizuri sana hali ngumu ambayo wanadamu wanakabili. Kati ya wazao wa Adamu, kumekuwa na wanaume na wanawake wenye ujuzi mwingi wa kisayansi, magwiji wa kitiba, na waasisi wa teknolojia. Hata hivyo, hakuna hata mmoja wao ambaye ameweza kuleta amani duniani na kufanya wanadamu wawe na afya bora kabisa kama Mungu alivyokusudia.

Sisi sote tunapatwa na matokeo mabaya ya uasi wa Adamu na Hawa. Kwa mfano, ni nani hajapatwa na uchungu wa ukosefu wa haki, woga wa uhalifu, maumivu ya ugonjwa wa kudumu, au kulemewa na huzuni wakati mpendwa anapokufa? Utulivu wowote katika maisha yetu huvurugwa upesi na msiba. Hata ikiwa nyakati fulani sisi huwa na furaha, maisha yetu huwa kama tu alivyosema mzee wa ukoo Ayubu: “Mwanadamu . . . ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko.”—Ayubu 14:1.

Tunapofikiria historia ya mwanadamu na hali yenye kusikitisha iliyopo leo, huenda tukaona kuwa hakuna matumaini kwa wakati ujao. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu hataruhusu hali hizo ziendelee milele. Atatimiza kusudi lake la awali kwa mwanadamu. (Isaya 55:10, 11) Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba jambo hilo litatendeka hivi karibuni?

Biblia inaonyesha kwamba sasa tunaishi katika kipindi hatari kinachoitwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Maneno hayo hayamaanishi mwisho wa dunia na viumbe vilivyomo. Badala yake, yanamaanisha “umalizio wa mfumo wa mambo” na hivyo mwisho wa mambo yanayotuhuzunisha. (Mathayo 24:3) Biblia inaeleza matukio na tabia ambazo watu wangedhihirisha katika siku za mwisho. Ona baadhi ya mambo hayo kwenye sanduku katika ukurasa wa 8, kisha utazame mandhari ya ulimwengu. Ramani yetu, yaani, Biblia inatusaidia kutambua kwamba sasa tunakaribia sana mwisho wa mfumo huu wa mambo. Lakini ni nini kitakachotendeka baada ya hapo?

Wakati Ujao Utakuwaje?

Mara tu baada ya Adamu na Hawa kuasi, Mungu alianza kufunua kusudi lake la kusimamisha Ufalme “ambao hautaharibiwa kamwe.” (Danieli 2:44) Ufalme huo, ambao wengi wamefundishwa wasali kuuhusu katika ile Sala ya Bwana, utawaletea wanadamu baraka zisizo na kifani.—Mathayo 6:9, 10.

Ufalme wa Mungu si hisia fulani isiyoeleweka iliyomo moyoni. Ni serikali halisi ya kimbingu ambayo italeta mabadiliko makubwa duniani. Ebu fikiria yale ambayo Mungu anaahidi kuwatimizia wanadamu kupitia Ufalme wake. Biblia inasema kwamba kwanza Mungu ‘ataharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Atawafanyia nini wale wanaomtii? Neno lake lililoandikwa linasema kwamba “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Ni mwanadamu yupi angeweza kutimiza mambo hayo? Ni Mungu tu anayeweza kuturudisha katika hali ambayo tangu awali alikusudia wanadamu wawe nayo.

Unaweza kunufaikaje na baraka zitakazoletwa na Ufalme wa Mungu? Andiko la Yohana 17:3 linasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” Mashahidi wa Yehova wanaendesha programu ya elimu ulimwenguni pote inayowasaidia watu wapate ujuzi huo. Wanafanya kazi yao katika nchi 230 hivi, na vichapo vyao vinachapishwa katika lugha zaidi ya 400. Ikiwa ungependa kujifunza mengi zaidi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova wanaoishi karibu nawe au waandikie kwa kutumia anwani ifaayo iliyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 5.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Sikilizeni nyinyi mnaosema: ‘Leo au kesho tutakwenda katika mji fulani na kukaa huko mwaka mzima tukifanya biashara na kupata faida.’ Nyinyi hamjui hata maisha yenu yatakavyokuwa kesho!”—Yakobo 4:13, 14, Biblia Habari Njema

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Biblia inaeleza historia ya wanadamu kuanzia watu wawili wa kwanza. Hivyo, inatuambia tulitoka wapi. Pia inaonyesha tunakoelekea. Lakini ili tuelewe yale ambayo Biblia inatuambia, tunahitaji kuichunguza kwa makini, jinsi ambavyo tungechunguza ramani kwa makini

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Dhambi” inaweza kumaanisha tendo baya au hali ya kuwa na mwelekeo wa kutenda mabaya. Tumezaliwa katika dhambi, ambayo huathiri matendo yetu. “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.”—Mhubiri 7:20

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Ikiwa ungepiga fotokopi karatasi yenye doa, doa hilo lingetokea kwenye nakala zote. Tukiwa wazao wa Adamu, sisi ni kama nakala hizo, sote tuna doa la dhambi. Adamu ndiye aliyekuwa na doa la kwanza

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Biblia inasema: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Andiko hilo linaonyesha kwa nini mwanadamu hajafaulu kuleta amani duniani. Hakuumbwa ‘aongoze hatua zake’ bila kumtegemea Mungu

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Mtunga-zaburi wa Biblia alimwambia Mungu hivi: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” (Zaburi 119:105) Biblia ni kama taa ambayo hutusaidia kuchukua hatua za hekima tunapofanya maamuzi. Kama ‘nuru ya barabara yetu,’ inaangaza njia iliyo mbele yetu ili tutambue wakati ujao wa mwanadamu

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

TOFAUTI KATI YA KUTARAJIA MEMA NA KUONA MAMBO KIHALISI

Mnamo Septemba 2000, nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa ziliweka miradi kadhaa ambayo ingetimizwa kufikia 2015. Miradi hiyo ilitia ndani:

Kupunguza kwa asilimia 50 watu wanaopata mshahara wa chini ya dola moja kwa siku na pia wale wanaokabili njaa.

Kuhakikisha kwamba watoto wote wanapata elimu ya msingi.

Kukomesha ukosefu wa usawa wa kijinsia katika viwango vyote vya elimu.

Kupunguza kwa asilimia 66 idadi ya vifo vya watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.

Kupunguza kwa asilimia 75 idadi ya akina mama wanaokufa wakati wa kujifungua.

Kupunguza na kukomesha kuenea kwa UKIMWI na pia magonjwa mengine makubwa, kama vile malaria.

Kupunguza kwa asilimia 50 idadi ya watu wasio na maji safi ya kunywa.

Je, miradi hiyo inaweza kufikiwa? Baada ya kuchanganua tena hali mwaka wa 2004, kikundi cha maofisa wa afya kutoka ulimwenguni pote kilikata kauli kwamba watu wanapaswa kutarajia mema huku wakitambua kwamba maendeleo yanayotazamiwa hayaonyeshi yale yanayotendeka kikweli. Dibaji ya kitabu State of the World 2005 inasema: “Umaskini unazidi kuzuia maendeleo katika maeneo mengi. Magonjwa kama vile UKIMWI yanaongezeka, na hilo linatokeza hali ambazo zinaweza kuwa tisho kubwa kwa afya katika nchi nyingi. Katika miaka mitano illiyopita, watoto wapatao milioni 20 wamekufa kutokana na magonjwa yanayoambukizwa kupitia maji ambayo yangeweza kuzuiwa, na kila siku mamilioni ya watu wanaendelea kukabiliana na uchafu unaosababishwa na ukosefu wa maji safi ya kunywa na mifumo mizuri ya kuondoa maji machafu na takataka.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

BAADHI YA MATUKIO YA “SIKU ZA MWISHO”

Vita visivyo na kifani.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:4.

Njaa.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:5, 6, 8.

Tauni.—Luka 21:11; Ufunuo 6:8.

Kuongezeka kwa uasi-sheria.—Mathayo 24:12.

Kuharibiwa kwa dunia.—Ufunuo 11:18.

Matetemeko makubwa ya nchi.—Luka 21:11.

Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.—2 Timotheo 3:1.

Kupenda pesa kupita kiasi.—2 Timotheo 3:2.

Kutotii wazazi.—2 Timotheo 3:2.

Kutokuwa na upendo wa asili.—2 Timotheo 3:3.

Kupenda raha badala ya kumpenda Mungu.—2 Timotheo 3:4.

Kutojizuia.—2 Timotheo 3:3.

Kutopenda mema.—2 Timotheo 3:3.

Kutojali hatari inayokaribia.—Mathayo 24:39.

Wadhihaki wanaokataa kwamba hizi ni siku za mwisho.—2 Petro 3:3, 4.

Kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu duniani pote. —Mathayo 24:14.

[Hisani]

© G.M.B. Akash/Panos Pictures

© Paul Lowe/Panos Pictures

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu