Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Mungu Mmoja Tu wa Kweli?

Je, Kuna Mungu Mmoja Tu wa Kweli?

Maoni ya Biblia

Je, Kuna Mungu Mmoja Tu wa Kweli?

MOLEKI, Ashtorethi, Baali, Dagoni, Merodaki, Zeu, Herme, na Artemi ni baadhi ya majina ya miungu ya kiume na ya kike yanayotajwa katika Biblia. (Mambo ya Walawi 18:21; Waamuzi 2:13; 16:23; Yeremia 50:2; Matendo 14:12; 19:24) Hata hivyo, ni Yehova peke yake anayetajwa katika Maandiko kuwa Mungu Mweza-Yote. Alipowaongoza watu wake katika wimbo wa ushindi, Musa aliimba hivi: “Ni nani kati ya miungu aliye kama wewe, Ee Yehova?”—Kutoka 15:11.

Ni wazi kwamba Biblia inamkweza Yehova juu ya miungu mingine yote. Lakini miungu hiyo midogo huwa na jukumu gani? Je, miungu hiyo pamoja na mingine mingi ambayo imeabudiwa kwa miaka mingi, ni miungu halisi iliyo na mamlaka ndogo zaidi ya Mungu Mweza-Yote, Yehova?

Miungu ya Kuwaziwa Tu

Biblia inamtaja Yehova kuwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli. (Zaburi 83:18; Yohana 17:3) Nabii Isaya aliandika maneno ya Mungu mwenyewe aliposema: “Kabla yangu hakuna Mungu yeyote aliyefanyizwa, na baada yangu hapakuendelea kuwapo yeyote. Mimi—mimi ni Yehova, na zaidi ya mimi hakuna mwokozi.”—Isaya 43:10, 11.

Si kwamba tu miungu mingine yote ni duni ikilinganishwa na Yehova. Mingi yao imewaziwa tu na wanadamu. Biblia hufafanua miungu hiyo kuwa “kazi ya mikono ya mwanadamu . . . , ambayo haiwezi kuona wala kusikia wala kula wala kunusa.” (Kumbukumbu la Torati 4:28) Biblia inafundisha waziwazi kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli.

Haishangazi kwamba Maandiko huonya vikali dhidi ya kuabudu mungu mwingine yeyote isipokuwa Yehova. Kwa mfano, katika amri ya kwanza ya zile Amri Kumi alizopewa Musa, taifa la kale la Israeli liliambiwa lisiabudu mungu mwingine yeyote. (Kutoka 20:3) Kwa nini?

Kwanza, kumwabudu mungu ambaye hata hayupo ni suto kubwa kwa Muumba. Biblia inasema kwamba waabudu wa miungu hiyo ya uwongo ‘wamebadili kweli ya Mungu kwa ajili ya uwongo nao wakauheshimu mno uumbaji na kuutolea utumishi mtakatifu badala ya kumtolea Yeye aliyeumba.’ (Waroma 1:25) Mara nyingi miungu hiyo ya kuwaziwa huwakilishwa na sanamu ambazo zimetengenezwa kwa vitu vya asili kama chuma au mbao. Miungu mingi huhusianishwa na vitu vya asili kama vile radi, bahari, na upepo. Basi kwa kweli, kuabudu miungu hiyo bandia ni kumkosea heshima kabisa Mungu Mweza-Yote.

Muumba huchukizwa sana na miungu ya uwongo na sanamu zao. Lakini maneno ya Mungu yanayoonyesha kwamba amechukizwa huelekezwa hasa kwa watu ambao wamefanyiza miungu hiyo ya uwongo. Maoni yake yanaelezwa waziwazi na maneno haya: “Sanamu za mataifa ni fedha na dhahabu, kazi ya mikono ya mtu wa udongo. Zina kinywa, lakini haziwezi kusema lolote; zina macho, lakini haziwezi kuona chochote; zina masikio, lakini haziwezi kusikia lolote. Pia hazina roho yoyote katika vinywa vyao. Wale wanaozifanya watakuwa tu kama hizo, kila mtu anayezitegemea.”—Zaburi 135:15-18.

Kuna sababu nyingine inayofanya Biblia ionye vikali dhidi ya kuabudu mtu yeyote au kitu chochote isipokuwa Yehova Mungu. Kufanya hivyo kungekuwa kupoteza wakati na jitihada nyingi. Nabii Isaya alisema hivi kwa kufaa: “Ni nani ambaye amefanya mungu au kutengeneza sanamu ya kuyeyushwa? Imekuwa isiyo na faida yoyote.” (Isaya 44:10) Biblia pia husema kwamba “miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani.” (Zaburi 96:5) Miungu ya uwongo si kitu na mtu hapati faida yoyote kwa kuiabudu.

Yesu, Malaika, na Ibilisi

Nyakati nyingine, Biblia hutaja watu halisi kuwa miungu. Hata hivyo, kuchunguza mambo kwa makini hufunua wazi kwamba Biblia inapowaita hivyo, neno “mungu” halikusudiwi kuwafanya watu hao waabudiwe. Badala yake, katika lugha ya awali ya Biblia, neno “mungu” lilitumiwa pia kumfafanua mtu mwenye nguvu au mtu aliye na mwili wa kiroho kama Mungu au aliyeshirikiana kwa ukaribu na Mungu Mweza-Yote.

Kwa mfano, maandiko fulani ya Biblia humtaja Yesu Kristo kuwa mungu. (Isaya 9:6, 7; Yohana 1:1, 18) Je, hilo linamaanisha kwamba Yesu anapaswa kuabudiwa? Yesu mwenyewe alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Ni wazi kwamba ingawa Yesu ana nguvu nyingi na ni kama Mungu, Biblia haionyeshi kwamba anapaswa kuabudiwa.

Malaika pia wanatajwa kuwa “kama Mungu.” (Zaburi 8:5; Waebrania 2:7) Hata hivyo, hakuna andiko lolote linalowatia moyo wanadamu waabudu malaika. Kwa kweli, pindi moja, mtume Yohana aliyezeeka alipigwa na butwaa alipomwona malaika hivi kwamba aliinama chini ili kumwabudu. Hata hivyo, malaika huyo alimwambia: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Mwabudu Mungu.”—Ufunuo 19:10.

Mtume Paulo alimtaja Ibilisi kuwa “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Akiwa “mtawala wa ulimwengu huu,” amejaribu kuwafanya watu waabudu miungu mingi ya uwongo. (Yohana 12:31) Kwa hiyo, kuabudu miungu iliyofanywa na wanadamu ni kumwabudu Shetani. Lakini Shetani si mungu anayestahili ibada yetu. Alijiweka mwenyewe kuwa mtawala, alinyakua utawala. Hatimaye, yeye, na ibada zote za uwongo zitaondolewa. Wakati huo, wanadamu wote, naam, uumbaji wote, utakiri kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli aliye hai.—Yeremia 10:10.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Biblia hufundisha nini kuhusu kuabudu sanamu?—Zaburi 135:15-18.

▪ Je, Yesu na malaika wanapaswa kuabudiwa kama miungu?—Luka 4:8.

▪ Mungu wa pekee wa kweli ni nani?—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Sanamu kutoka kushoto hadi kulia: Maria, Italia; mungu wa mahindi wa Wamaya, Mexico na Amerika ya Kati; Ashtorethi, Kanaani; sanamu, Sierra Leone; Buddha, Japani; Chicomecóatl, Aztec, Mexico; Kipanga anayemwakilisha Horus, Misri; Zeu, Ugiriki

[Hisani]

Maize god, Horus falcon, and Zeus: Photograph taken by courtesy of the British Museum