Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutembelea Kituo cha Viungo Bandia

Kutembelea Kituo cha Viungo Bandia

Kutembelea Kituo cha Viungo Bandia

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI NEW ZEALAND

SABABU mbili zilifanya nipange kutembelea Kituo cha Viungo Bandia huko Wellington, New Zealand. Kwanza, mguu wangu bandia ulihitaji kurekebishwa. Pili, nilitaka kutembea ndani ya kituo hicho ili nijifunze kuhusu kazi inayohusika katika kutengeneza viungo bandia.

Mtaalamu mmoja wa kuunganisha viungo bandia alikubali kunitembeza huko. Kutembelea kituo hicho kulininufaisha na kuongeza uelewaji na uthamini wangu kwa ustadi na bidii ya wale wanaohusika katika kazi hiyo.

Mguu Bandia Hutengenezwaje?

Wagonjwa wengi ambao hutembelea kituo hicho hutaka mguu bandia. Hatua ya kwanza katika kuunda mguu ni kutia kifuniko kwenye gutu, yaani, sehemu ya iliyobaki ya kiungo kilichokatwa. Kisha plasta humwagwa kwenye kifuniko hicho ili kufanyiza mfano wa gutu la kiungo hicho. Kisha plasta hiyo hutumiwa kutengeneza soketi ambayo mguu huo mpya utaingizwa. Hivyo hatua za kutengeneza mguu unaofanya kazi kabisa huanza. Njia mpya, inayofaa zaidi ni kutumia programu ya kompyuta (CAD/CAM) kupima gutu. Kisha mashini huchonga mfano kamili wa sehemu ya mguu wa mtu uliosalia.

Baada ya kutazama maonyesho ya utaalamu uliotumiwa katika kituo hicho, nilionyeshwa baadhi ya viungo bandia vilivyoletwa kutoka nchi nyingine. Mojawapo ya viungo vyenye kuvutia zaidi ni kiunganishi cha goti cha haidroli kilichounganishwa kwenye soketi fulani ya plastiki inayoweza kubadilishwa umbo kwa moto ili imtoshee mgonjwa. Broshua zenye picha nyingi kuhusu vifaa kama hivyo zinapatikana mahali mbalimbali ulimwenguni.

Katika hatua za mwisho za kutengeneza mguu, mabadiliko madogomadogo hufanywa ili kupatanisha shimo la goti, goti, ngozi, na mguu ili mtu aweze kutembea bila matatizo. Mwishowe, kifuniko cha sponji hutayarishwa. Kifuniko hicho huficha “mifupa” ya mguu bandia. Kifuniko hicho hutengenezwa kwa njia ambayo kitafanana kabisa na sehemu iliyobaki ya mguu.

Mgonjwa anapoweza kutembea kwa uhakika wa kutosha, mipango hufanywa amwone mpasuaji wa mifupa ambaye hutembelea kituo hicho cha viungo. Hivyo, mtaalamu huyo huchunguza kwa mara ya mwisho ikiwa kiungo hicho bandia kinafaa kabisa.

Watoto na Wanamichezo

Nilipokuwa nikitembezwa, nilimwona msichana mdogo. Hakuona haya kutuonyesha gutu lake na kiungo bandia kilichokuwa kimeunganishwa. Baadaye nilimwona akirukaruka, bila wasiwasi wowote.

Nilimuuliza mtaalamu wa kuunganisha viungo bandia kuhusu watoto ambao hupoteza viungo. Alinionyesha mkono mdogo na kunieleza kwamba viungo bandia kama hivyo huunganishwa kwenye gutu la watoto wachanga wenye miezi sita hivi. Kwa nini? Ili kumzoeza jinsi atakavyotumia mkono bandia wakati ujao. Mtaalamu huyo alisema kwamba bila mazoezi hayo, mtoto huyo atakua akitumia mkono mmoja na hivyo itakuwa vigumu kuanza kutumia mikono miwili baadaye.

Nilielezwa kwamba hivi majuzi kampuni moja ya Ulaya ilituma kontena ya vifaa vya viungo bandia kwa ajili ya wanamichezo huko Sydney, Australia, ili wavitumie wakati wa Olimpiki za Walemavu. Wanamichezo walipewa vifaa hivyo bila malipo, na wataalamu wa kuviunganisha, kutia ndani wachache kutoka New Zealand, walikuwapo kuwasaidia wakati wa michezo.

Viungo fulani vilikuwa hasa vimeundwa kwa ajili ya wanamichezo. Nilionyeshwa mfano mmoja. Kilikuwa kifaa cha mguu na kifundo cha mguu kilichotengenezwa kwa vifaa vya pekee ambavyo hunyumbulika tu kama mguu wa mwanadamu.

Maendeleo ya Kisasa

Tunaweza kutazamia nini katika ufundi wa viungo bandia? Mtaalamu aliyekuwa akinitembeza aliniambia kuhusu mguu bandia ambao huelekezwa kwa kompyuta ambao sasa unavaliwa na angalau mgonjwa mmoja huko New Zealand. Inaonekana kwamba kiungo hicho hutenda wakati mkazo unapowekwa kwenye vibonyezo fulani. Hilo hufanya mtu atembee kwa njia ya kawaida.

Katika nchi fulani, mbinu ya kuunganisha kiungo bandia kwenye mfupa inajaribiwa na wapasuaji stadi wa viungo. Pini fulani ya pekee huingizwa kwenye gutu ili kuliunganisha na kiungo bandia. Mbinu hiyo huondoa uhitaji wa kufungwa plasta na kutengeneza soketi.

Utafiti pia unafanywa ili kutia vitu vya kuhisi katika nyuzi za neva, ambazo zitamfanya mtu adhibiti kiungo bandia kwa kutumia akili pekee. Nchini Marekani na nchi nyinginezo, watu fulani wamepandikizwa mikono ya watu wengine, lakini mbinu hiyo imetokeza ubishi kwani mgonjwa hulazimika kutumia dawa maisha yake yote ili kiungo hicho kisikataliwe na mwili wake.

Sasa mfumo wa kielektroniki pia unatumiwa kwa ajili ya kuunganisha mikono bandia. Mikazo kutoka kwenye misuli ya mkono, ambayo bado huwapo katika sehemu ya mkono iliyobaki, hutendesha elektroni. Mikazo hiyo midogo huvumishwa na kutumiwa kuongoza mifumo ya elektroniki katika kiungo hicho bandia. Teknolojia ya kisasa ya mikono bandia hutumia kompyuta kuwezesha mkono bandia wa mgonjwa ufanye kazi vizuri.

Kwa kuwa nilishangazwa na maendeleo ya teknolojia ya viungo, nilimwuliza mtaalamu huyo wa kuunganisha viungo bandia angelinganishaje utendaji wa viungo hivyo na wa viungo halisi. Alisema kwamba viungo halisi havina kifani. Hilo lilifanya nifikiri kuhusu maneno ya mtunga-zaburi ambaye alisali hivi kwa Muumba wake: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”Zaburi 139:14.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

[Picha]

Mikono inayoelekezwa na elektroni hutumia ishara za misuli kuongoza mwendo na uwezo wa kushika vitu

[Hisani]

Hands: © Otto Bock HealthCare

[Picha]

Ndani ya goti hili, kifaa fulani cha kompyuta husaidia kufanya goti lipatane na kutembea kwa mgonjwa

[Hisani]

Knee: Photos courtesy of Ossur

[Picha]

Picha hii ya mguu inaonyesha kifuniko cha sponji na kifundo cha mguu

[Hisani]

© Otto Bock HealthCare

[Hisani]

© 1997 Visual Language

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kurekebisha mguu bandia

[Picha katika ukurasa wa 22]

Daktari akimvisha mgonjwa kiungo bandia

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mkono mdogo bandia unaotumiwa kuzoeza watoto wachanga waliokatwa viungo

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mnamo 2004 mshindi wa mbio za meta 100 katika Olimpiki za Walemavu alishinda kwa muda wa sekunde 10.97 akiwa amevalia mguu bandia uliotengenezwa kwa nyuzi za kioo na kaboni

[Hisani]

Photo courtesy of Ossur/Photographer: David Biene

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

© Otto Bock Healthcare