Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa na Nguvu za Ujana Milele!

Kuwa na Nguvu za Ujana Milele!

Kuwa na Nguvu za Ujana Milele!

MTU aliyekuwa kando ya Yesu alikuwa anakaribia kufa. Alisihi hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu alimjibu: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:42, 43) Ni kweli kwamba mwanamume huyo ambaye hajatajwa jina hakuwa anakufa kwa sababu ya ugonjwa unaotokea uzeeni; alikuwa akiuawa kwa sababu ya uhalifu. Hata hivyo, wazee wanaweza kutiwa moyo sana na hali yake yenye kusikitisha.

Tunachochewa na imani isiyo ya kawaida ya mwanamume huyo! Hata ingawa Yesu ambaye alikuwa kando yake alikuwa akifa kwenye mti wa mateso, mwanamume huyo alikuwa na uhakika kwamba kwa kweli Yesu angetawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Pia, alijiambia kwamba Yesu angemkumbuka siku moja. Hebu wazia, mwanamume huyo aliyehukumiwa ataamka kutoka katika kifo na kuishi katika paradiso nzuri Yesu akiwa Mfalme!

Wanadamu wako katika hali sawa na ile ya mkosaji huyo aliyekuwa anakaribia kufa. Jinsi gani? Haidhuru tuna umri gani, sote hupatwa na matokeo ya dhambi na tunahitaji wokovu. (Waroma 5:12) Kama mhalifu huyo, tunaweza kuweka tumaini letu kwa Kristo Yesu, na hata tutumaini kwamba atatuondolea matatizo ambayo hutupata tunapozeeka! Ili sisi tuwe na uhakika, Yesu aliwatolea wanadamu tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani wakiwa na afya kamilifu ya mwili na akili.—Yohana 3:16, 36.

Vitu Vyote Vipya kwa Wazee na Vijana

Chini ya Ufalme wa Kristo, wakaaji wa dunia “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Hakuna atakayesema: “Mimi ni mgonjwa.” (Isaya 33:24) Ulemavu wowote ambao huenda tumekuwa nao, utaondolewa kwani “kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.” (Isaya 35:6) Wazee watapata tena nguvu zao za ujana, nyama yao itakuwa “laini kuliko wakati wa ujana.”—Ayubu 33:25.

Hata hivyo, je, ni jambo linalopatana na akili kutazamia mambo hayo? Mfikirie Yule aliyempa mwanamume huyo aliyekuwa akifa tumaini la Paradiso. Pindi nyingi umati ulimletea Yesu watu waliokuwa viwete, vilema, vipofu, na viziwi. Aliponya “kila namna ya magonjwa na kila namna ya udhaifu.” (Mathayo 9:35, 36; 15:30, 31; Marko 1:40-42) Alionyesha wazi mambo ambayo Ufalme wake utatimiza. Yesu hata aliwafufua watu kadhaa waliokuwa wamekufa. (Luka 7:11-17; Yohana 11:38-44) Kwa kufanya hivyo, alitilia mkazo ahadi yake kwamba “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Hebu wazia kuamka katika Paradiso ukiwa na mwili mpya, macho yanayoona vizuri, masikio yanayosikia sauti za ndege na sauti zenye shangwe, mikono na miguu isiyo na uchungu, na akili iliyo chonjo kabisa. Hakutakuwako tena “siku zenye msiba” za uzeeni. (Mhubiri 12:1-7; Isaya 35:5, 6) Hata kifo ‘kitaangamizwa,’ naam, ‘kitamezwa milele.’—1 Wakorintho 15:26, 54.

Yanapolinganishwa na unabii wa Biblia, matukio ya sasa ulimwenguni yanaonyesha kwamba wakati wa kuondolewa kwa uzee unakaribia haraka. (Mathayo 24:7, 12, 14; Luka 21:11; 2 Timotheo 3:1-5) Hivi karibuni, wazee ambao wamemwamini Mungu na kumtumikia watafurahia tena nguvu za ujana milele!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Zoeza Ubongo Wako!

Kama vile tu mazoezi ya mwili huimarisha misuli, ndivyo mazoezi ya akili huboresha ubongo. Ili kuchochea ubongo, tunahitaji kufanya mambo mapya. Mambo yafuatayo yanaonyesha njia za kusitawisha na kuimarisha mawasiliano ya chembe za ubongo.

▪ Tafuta mambo mapya ya kufanya kama vile sanaa, kuchonga vinyago, mchezo wa kutafuta maneno na kuyaunganisha, na fumbo la kuunganisha vipande vya kufanyiza picha; jifunze lugha nyingine.

▪ Shirikiana na watu mbalimbali; zungumza nao ili usifanye mambo yaleyale na uboreshe akili.

▪ Kuwa mtu wa kiroho. “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” —Wafilipi 4:6, 7.

▪ Soma vichapo vinavyofaa; mweleze mtu fulani jambo ulilosoma.

▪ Kumbuka habari ulizosikia kwenye redio au televisheni na uwaeleze wengine ili kuzoeza kumbukumbu lako.

▪ Tumia mkono ambao hautumii kwa ukawaida (mkono wa kushoto ikiwa wewe hutumia mkono wa kulia) kufinya kibonyezo cha televisheni, kupiga simu, au kupiga mswaki.

▪ Tumia hisi zako zote kadiri uwezavyo siku nzima.

▪ Jifunze na utembelee sehemu mbalimbali zilizo karibu au mbali.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yesu anaahidi kwamba uzee uliojaa maumivu utakwisha karibuni, nao watu watakuwa na nguvu za ujana milele