Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Yesu Alikuwa Mwana wa Mungu?

Je, Kweli Yesu Alikuwa Mwana wa Mungu?

Maoni ya Biblia

Je, Kweli Yesu Alikuwa Mwana wa Mungu?

KWA imani kubwa mtume Petro alimwambia Yesu hivi: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16) Hili ni andiko moja tu kati ya maandiko mengi ya Biblia yanayomtaja Yesu kuwa Mwana wa Mungu. Usemi huo, Mwana wa Mungu, umechochea hisia mbalimbali miongoni mwa watu wa dini.

Wengi wanaoamini kwamba Yesu Kristo ni Mungu hushindwa kueleza sababu inayofanya aitwe Mwana wa Mungu. Mtu anayetumia akili atakubali kwamba Yesu hawezi kuwa Mungu na wakati huohuo awe Mwana wa Mungu. Wengine humwona Yesu kuwa tu mtu mashuhuri katika historia, mtu mwenye hekima, au hata nabii wa kweli wa Mungu. Lakini Biblia inafundisha nini hasa? Je, ni muhimu kuzingatia yale unayoamini?

Mzaliwa wa Kwanza wa Mungu

Biblia inaonyesha kwamba kuna wakati ambapo Mungu alikuwa peke yake. Kwa kuwa yeye ni mwenye upendo, aliamua kumpa mtu mwingine zawadi ya uhai na hivyo akawa baba, lakini si baba wa kibinadamu. Hivyo, kwa kutumia uwezo wake mkuu wa kuumba Yehova alifanya mtu wa roho mwenye akili, yaani, Yesu Kristo, ambaye ndiye “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14; Methali 8:22) Kwa kuwa Mungu alimuumba Yesu moja kwa moja, naye alikuwa peke yake alipomuumba, kwa kufaa Yesu anaitwa “mwana mzaliwa-pekee” na “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.”—Yohana 1:14; Wakolosai 1:15.

Hivyo basi, kwa kuwa Yesu ndiye kiumbe wa kwanza wa Mungu, yeye hawezi kuitwa Muumba, “Mungu pekee.” (1 Timotheo 1:17) Kwa upande mwingine, Mungu alimpa Mwana wake mapendeleo mengi. Kwa mfano, kupitia Yesu, Mungu aliumba “vitu vingine vyote” kutia ndani hata malaika. Malaika hao wanaitwa “wana wa Mungu” kwa kuwa Yehova ndiye aliyewapa uhai.—Wakolosai 1:16; Ayubu 1:6; 38:7.

Yaonekana Mungu alikuwa akizungumza na Mwana wake mzaliwa wa kwanza aliposema hivi baada ya kuitayarisha dunia ili ikaliwe na wanadamu: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” (Mwanzo 1:26; Methali 8:22-31) Hivyo, Yehova alimuumba pia Adamu, mwana wa kwanza wa kibinadamu wa Mungu, kupitia kiumbe wa roho ambaye angekuwa Yesu.—Luka 3:38.

Yesu Awa Mwana wa Kibinadamu wa Mungu

Mtume Yohana anafunua kwamba katika wakati uliowekwa, Mwana wa roho wa Mungu “akawa mwili, akakaa katikati yetu.” (Yohana 1:14) Ili kuubadili mwili wa roho wa Yesu uwe wa kibinadamu, Mungu aliuhamisha kimuujiza uhai wa Yesu kutoka mbinguni na kuuingiza katika tumbo la uzazi la Maria, msichana Myahudi aliyekuwa bikira. Kwa njia hiyo, Yesu aliendelea kuwa Mwana wa Mungu ingawa alikuwa binadamu. Isitoshe, kwa kuwa Mungu ndiye aliyempa Yesu uhai, bali si binadamu, Yesu alizaliwa akiwa mkamilifu, bila dhambi. Malaika Gabrieli alimwambia Maria hivi: “Kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”—Luka 1:35; Waebrania 7:26.

Yesu alipokuwa binadamu, Baba mwenyewe alithibitisha kwamba Yesu alikuwa Mwana wake. Wakati wa ubatizo wa Yesu, Yohana Mbatizaji aliona mbingu zikifunguka na akasikia sauti kutoka huko ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:16, 17) Haishangazi kwamba Yohana aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimeona, na nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.”—Yohana 1:34.

Wakati wa huduma yake duniani, Yesu hakutangaza hadharani kwamba yeye ndiye Masihi, Mwana wa Mungu. (Marko 8:29, 30) Mara nyingi aliwaacha watu waamue wenyewe kwa kusikiliza mafundisho yake, kwa kutazama maisha yake, na kwa kushuhudia miujiza mingi ambayo aliifanya hadharani. Kwa mfano, aliwaponya “wote waliokuwa na hali mbaya, waliokuwa wakitaabishwa na magonjwa na kuteswa kwa namna mbalimbali.” (Mathayo 4:24, 25; 7:28, 29; 12:15) Wote waliokuwa vipofu, viziwi, vilema, na wagonjwa walimwendea Yesu nao wakaponywa. Hata aliwafufua wafu! (Mathayo 11:4-6) Wanafunzi wa Yesu walishuhudia alipotembea kimuujiza juu ya maji na kutuliza pepo na mawimbi wakati wa dhoruba kali. Mambo hayo yaliyoonyesha uwezo wake yaliwachochea wanafunzi kusema: “Wewe kwa kweli ni Mwana wa Mungu.”—Mathayo 14:24-33.

Jinsi Mwana wa Mungu Anavyoweza Kukunufaisha

Kwa nini Mungu alimhamisha Mwana wake mzaliwa-pekee kutoka mbinguni hadi duniani, kisha akauawa kikatili? “Ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Naam, ni kupitia kifo tu Yesu angeweza “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Katika historia yote, hakuna mtu yeyote ambaye ameonyesha upendo mwingi kwa wanadamu kuliko Yehova na Mwana wake mzaliwa wa kwanza.—Waroma 8:32.

Baada ya kifo chake, Yesu “alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu” kwa njia ya pekee na yenye nguvu, yaani, kurudishwa hai kupitia “ufufuo kutoka kwa wafu” na hivyo kuwa tena Mwana wa roho wa Mungu. (Waroma 1:4; 1 Petro 3:18) Kisha, baada ya kungoja kwa subira akiwa kando ya Baba yake kwa miaka ipatayo 1,900, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ni serikali ya mbinguni ambayo hivi karibuni itatawala dunia yote. —Zaburi 2:7, 8; Danieli 7:13, 14.

Je, ungependa kupata kibali cha Mwana huyo wa Mungu mwenye nguvu? Ikiwa ndivyo, tunakutia moyo uchunguze mafundisho yake na kuyafuata maishani. Yesu mwenyewe alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Naam, yale ambayo mtu anaamini kumhusu Mwana wa Mungu ni muhimu!—Yohana 3:18; 14:6; 1 Timotheo 6:19.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Yesu ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu katika njia gani?—Yohana 1:3, 14; Ufunuo 3:14.

▪ Kwa nini unaweza kuamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?—Mathayo 3:16, 17.

▪ Unaweza kunufaikaje kwa kuamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?—Yohana 3:16; 14:6; 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Mafundisho ya Yesu yenye hekima na miujiza yake yenye nguvu ilithibitisha kwamba yeye hakuwa mwanadamu wa kawaida