Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kupata Upendo wa Kweli

Jinsi Unavyoweza Kupata Upendo wa Kweli

Jinsi Unavyoweza Kupata Upendo wa Kweli

Unaweza kufanya nini ili upate upendo na upendwe zaidi, na si kwa njia ya kimahaba tu? Je, unahitaji kuwa tajiri? Au unahitaji kuboresha sura yako?

WANAUME na wanawake hufikiri hilo ndilo suluhisho kwa kuwa wameathiriwa na matangazo ya biashara na vyombo vya habari. Bila shaka, ni jambo la kawaida na linalofaa kujali sura yetu, lakini urembo haudumu, na huo au utajiri hauwezi kuweka msingi wa kuwa na kifungo cha kudumu. Lakini kuwa na upendo usio na ubinafsi kunaweza kusaidia watu wapate upendo wa kweli. Yesu alifundisha hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:38) Kwa ufupi, ukitaka kupendwa, waonyeshe wengine upendo.

Tunaweza kuonyeshaje upendo? Akiandika chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, mtume Paulo alijibu swali hilo. Alifunua kwamba upendo una nguvu, nao huonyeshwa si kwa hisia, bali kupitia yale ambayo mtu huwatendea wengine na yale anayojizuia kutenda. Ona maneno haya ya Paulo: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4-7.

Wewe huhisije mtu anapokuonyesha fadhili au anapokuvumilia licha ya kwamba wewe husema au kufanya mambo madogomadogo yanayoudhi? Je, huvutiwi na mtu anayekujali kikweli, hakasiriki upesi, husamehe na husema kweli hata ingawa si rahisi kusamehe au kuwa mnyoofu?

Basi watendee wengine vivyo hivyo. Yesu alisema: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Si rahisi sikuzote kuonyesha upendo, lakini kuna manufaa ya kujitahidi kufanya hivyo. Kwanza, utapendwa na familia yako, marafiki, mwenzi wako wa ndoa, au yule atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa. Pia, utakuwa na furaha kwa kuwa unafanya jambo lililo sawa na unajitoa kwa ajili ya wengine. Naam, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Jifunze Upendo Kutoka kwa Mwenye Mamlaka Kuu Zaidi

Yehova ni Mungu wa upendo, naye ndiye mtaalamu bora zaidi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo wake humchochea kuwafundisha wote wanaotaka kujifunza sifa hiyo. Fikiria kanuni kadhaa za Biblia ambazo zinaweza kutusaidia kupendwa na kuwaonyesha wengine upendo.

‘Iweni wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Uchunguzi uliofanyiwa wenzi wa ndoa zaidi ya 20,000 ulionyesha kwamba watu waliokuwa na furaha zaidi ni wale ambao wenzi wao waliwasikiliza kwa makini. Mawasiliano mazuri ni muhimu katika uhusiano. Profesa mmoja wa masuala ya kijamii aliandika hivi: “Utajihisi mpweke ikiwa mwenzi wako hajui mambo unayokabiliana nayo. Au hali yako inaweza kuwa mbaya hata zaidi ikiwa mwenzi wako anajua yale unayokabili lakini haelewi sababu inayofanya mambo hayo yakuhangaishe sana.” Profesa huyo anaongeza kusema kwamba hata kama watu wawili wanatofautiana sana, “ikiwa mwenzi mmoja anajali maoni ya mwenzake na yale yanayompata maishani, basi tofauti hizo si kitu.”

“Mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo wenu mwororo. . . . Panukeni.” (2 Wakorintho 6:12, 13) Sisi hunufaika tunapopanua upendo wetu kwa wengine. Kichapo kimoja cha Chuo cha Kitiba cha Harvard kinasema: “Uchunguzi mwingi umeonyesha kwamba watu walio na utegemezo wa jamii, yaani, watu walio na uhusiano mzuri na familia, marafiki, na jamii, huwa na furaha zaidi, huwa na matatizo machache zaidi ya afya, nao huishi muda mrefu zaidi.”

“Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Waebrania 10:24, 25) Sisi huathiriwa na marafiki wetu. Unaposhirikiana na wale wanaoonyesha upendo wa kweli wa Kikristo, utaonyeshwa sifa hiyo nawe utajifunza jinsi ya kuwaonyesha wengine sifa hiyo. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuonyeshana upendo huo, wakijua kwamba sifa hiyo huwatambulisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu. (Yohana 13:35) Unakaribishwa uhudhurie mikutano yao ya Kikristo.

Ukihisi kwamba hupendwi, usivunjike moyo wala usijilaumu sana. Kumbuka kwamba Yehova anaona hali yako. Je, unamkumbuka Lea aliyetajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu? Yehova aliona hali yake, naye akapata wana sita na binti mmoja, na hiyo ilikuwa baraka kwelikweli katika kizazi ambacho kilithamini sana watoto! Isitoshe, baadaye wana wote wa Lea walikuwa babu wa makabila ya Israeli. (Mwanzo 29:30-35; 30:16-21) Lazima Lea awe alifarijika sana kuona jinsi ambavyo Mungu alimjali kwa upendo.

Katika ulimwengu mpya unaoahidiwa katika Biblia, hakuna mtu atakayehisi kuwa hapendwi. Badala yake, wanadamu wote wataonyeshana upendo wa kweli. (Isaya 11:9; 1 Yohana 4:7-12) Basi na tuonyeshe sasa kwamba tunataka kuishi katika ulimwengu huo kwa kusitawisha upendo unaofundishwa katika Biblia na ambao umeonyeshwa na Mtungaji wake. Naam, shangwe ya kweli haitokani tu na kupendwa, bali inatokana na kuwaonyesha wengine upendo usio na ubinafsi.—Mathayo 5:46-48; 1 Petro 1:22.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ukitaka kuonyeshwa upendo, waonyeshe wengine upendo