Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ni Vigumu Kupata Upendo wa Kweli?

Kwa Nini Ni Vigumu Kupata Upendo wa Kweli?

Kwa Nini Ni Vigumu Kupata Upendo wa Kweli?

Kuna mashauri chungu nzima kuhusu upendo wa kimahaba. Madaktari na washauri hutoa mwongozo. Mara nyingi kunakuwa na mijadala kuhusu habari hiyo kwenye televisheni au redio.

VITUO vingi vya Intaneti hudai kwamba vinatoa maagizo kuhusu jinsi ya kupata upendo. Huenda ukaambiwa kwamba utagundua “siri zenye kustaajabisha” na utajifunza kutoka kwa “wataalamu wa kutafutia watu wachumba,” “wataalamu wa mahusiano,” “madaktari wa upendo,” na vilevile kutoka kwa wataalamu wa akili, wanasaikolojia, na wanajimu.

Watu hununua sana vitabu na magazeti ambayo huzungumzia upendo, na baadhi yake hutoa ahadi zilizotiwa chumvi. Kwa mfano, kitabu kimoja kinadai kuwa kinaweza kukuonyesha “jinsi ya kumfanya mtu yeyote akupende.” Kitabu kingine husema kinaweza kukuonyesha jinsi ya kupata “mwenzi bora zaidi katika mwezi mmoja tu.” Kwa wale wanaohisi kuwa mwezi mmoja ni muda mrefu sana, kuna kitabu kinachofunua jinsi ambavyo katika muda “usiozidi dakika 90,” unaweza kumfanya mtu akupende milele.

Mashauri mengi hugharimu. Nao watu wengi hulipa katika njia mbili. Wao hutoa pesa kupata mashauri. Kisha, mwongozo huo unapokuwa na kasoro, na mara nyingi huwa nayo, watu hao huumia kihisia.

Hata hivyo, kuna chanzo kimoja cha mashauri ambacho mashauri yake hufaulu yanapofuatwa. Isitoshe, kinazungumzia habari hiyo kwa unyoofu bila kutoa madai yenye kusisimua yasiyo na msingi na ahadi zisizoweza kutimizwa. Ingawa kiliandikwa zamani sana, mashauri yake hayajapitwa na wakati. Mtungaji wake ana hekima na upendo usio na kifani. Huenda tayari una zawadi hii ya pekee, yaani, Biblia Takatifu. Haidhuru hali au malezi yetu, Biblia hutufundisha yale tunayohitaji kujua kuhusu upendo. Na mashauri yake hayatozwi.

Je, Biblia inaweza kutusaidia tuwe na uhusiano mzuri na kila mtu? La. Watu fulani hawawezi kuwa rafiki zetu hata tujitahidi kadiri gani. Nao upendo wa kweli hauwezi kulazimishwa. (Wimbo wa Sulemani 8:4) Hata hivyo, tukifuata mwongozo wa Biblia, itakuwa rahisi zaidi kusitawisha mahusiano yenye upendo, ingawa huenda hilo likahitaji wakati na jitihada nyingi. Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata. Lakini kwanza fikiria sababu inayofanya iwe vigumu zaidi kupata upendo wa kweli siku hizi.

Upendo “Utapoa”

Katika unabii wake wenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitabiri kwa usahihi kuhusu hali na maelekeo ya watu katika siku zetu. Alisema kwamba kungekuwa na uasi-sheria na vita, mambo yaliyo kinyume cha upendo! Alisema pia kwamba ‘watu wengi . . . watasalitiana na kuchukiana’ na kwamba “upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:3-12) Je, hukubali kwamba upendo wa wengi umepoa, na kwamba upendo wa kweli unakosekana hata katika familia?

Kuongezea maneno ya Yesu, mtume Paulo alifafanua kwa njia ya wazi zaidi tabia za watu katika “siku za mwisho.” Aliandika kwamba watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Katika nchi nyingi tabia hizo zimekuwa za kawaida.

Fikiria maswali haya: Je, wewe huvutiwa na watu wenye kiburi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, ambao wanaweza kukuchongea au kukusaliti? Je, wewe huvutiwa na watu wanaojipenda wenyewe, wanaopenda pesa, au wanaopenda raha? Kwa kuwa watu wenye ubinafsi huruhusu pupa na mapendezi yao wenyewe yaongoze mahusiano yao, huenda wakapendezwa na watu wengine kwa sababu za kibinafsi. Kwa hekima, Maandiko hushauri hivi: “Geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:5.

Pia ona kwamba Paulo anasema kuwa katika siku za mwisho watu watakuwa “wasio na upendo wa asili,” au kama tafsiri nyingine inavyosema, “hawatakuwa na upendo wa kawaida kwa familia zao.” Kwa kuhuzunisha, watoto wengi wanakua katika familia kama hizo. Mara nyingi, watoto hao hujifunza kuhusu upendo kutoka kwenye vyombo vya habari. Lakini je, vyombo vya habari huwafundisha mambo sahihi kuhusu upendo ambao utawasaidia kuwa na mahusiano mazuri zaidi?

Je, Ni Upendo wa Kuwaziwa au Ni Upendo Halisi?

Kwa kiwango fulani, sisi sote tunaathiriwa na vyombo vya habari. Mtafiti mmoja aliandika hivi: “Tangu utotoni, sisi hupata habari chungu nzima kuhusu hadithi za kuwaziwa na maoni yaliyokita mizizi kuhusu ngono, upendo, na mahusiano ya kimahaba katika sinema na televisheni, vitabu na magazeti, redio na muziki, matangazo ya kibiashara, na hata kwenye habari.” Pia alieleza hivi: “Mambo ambayo vyombo vingi vya habari huonyesha kuhusu ngono, upendo, na mahusiano ya kimahaba hufanya tuwe na matarajio yasiyoweza kutimia ambayo huwa vigumu kuyaondoa akilini kabisa. Mambo hayo hufanya tusitosheke na wenzi wetu wala tusiridhike na jinsi tulivyo.”

Mara nyingi vitabu, sinema, na nyimbo hazielezi upendo kwa usahihi kwani lengo la vyombo vya habari si kuelimisha bali ni kutumbuiza. Kwa hiyo, waandikaji hutunga hali za kuwaziwa na hadithi za mahaba ambazo zitawaletea pesa nyingi. Hata hivyo, kwa kusikitisha, si rahisi kutofautisha kati ya mambo halisi na yale ya kuwaziwa. Kwa hiyo, mara nyingi watu hutamauka mahusiano yao yasipokuwa kama yale ya watu wanaosimuliwa katika hadithi za kuwaziwa. Hivyo, tunawezaje kutofautisha kati ya hadithi za kuwaziwa na mambo halisi, kati ya upendo wa kimahaba unaoonyeshwa katika vyombo vya habari na upendo wa kweli? Fikiria tofauti zifuatazo.

Tofauti Kati ya Upendo wa Kuwaziwa na Upendo wa Kweli

Iwe ni katika vitabu, sinema, au michezo ya kuigiza, hadithi za mahaba zinaweza kutofautiana, lakini mambo ya msingi hayatofautiani. Gazeti Writer linasema hivi: “Hadithi nyingi za mahaba hazitofautiani. Na kuna sababu nzuri. Hadithi ifuatayo hupendwa sana na watu: Mvulana fulani akutana na msichana, kisha mvulana anampoteza msichana huyo halafu mvulana anampata tena msichana huyo. Hadithi hiyo huwavutia watu haidhuru imesimuliwa lini, wapi na mara ngapi.” Na tuchunguze kwa uangalifu hadithi hiyo inayopendwa sana.

Mvulana fulani akutana na msichana: Mwana wa mfalme mwenye kuvutia anakutana na mwanamke mrembo, nao wanapendana. Mwandishi mmoja mwenye mafanikio anawashauri hivi wale wanaotaka kuwa waandishi wa riwaya za mahaba: “Lazima msomaji wako aone kwamba watu hao wawili walipendana mara tu walipokutana kwa mara ya kwanza.”

Wazo la kwamba watu wanaweza kupendana wanapokutana tu mara ya kwanza huwafanya watu wafikiri kwamba upendo wa kweli ni hisia tu, hisia yenye nguvu sana ambayo hukulemea unapokutana na mtu wa pekee, na kwamba upendo wa aina hiyo hutukia ghafula pasipo jitihada yoyote na hata huhitaji kumjua sana yule mtu mwingine. Hata hivyo, upendo wa kweli si hisia tu. Ni kweli kwamba hisia zinahusika, lakini upendo ni kifungo chenye nguvu kinachotia ndani kanuni fulani. Upendo huendelea kuimarika unapokuzwa na kudumishwa.—Wakolosai 3:14.

Isitoshe, unahitaji muda kumjua mtu mwingine. Kufikiri kwamba umempata mwenzi anayekufaa mnapokutana tu kwa mara ya kwanza ni kama hadithi ya kuwaziwa na mara nyingi hukatisha tamaa. Kwa kuongezea, ukikata kauli haraka kwamba umepata mtu unayempenda kikweli, huenda ukapuuza mambo yanayoonyesha kwamba huo si upendo wa kweli. Kuchagua mwenzi anayekufaa kunahitaji mengi zaidi kuliko kuwa na hisia zenye nguvu zinazochochewa na kupumbazwa ghafula na upendo bandia. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba kuchagua mwenzi asiyekufaa kunaweza kuathiri kazi yako, afya yako ya akili na mwili, na hata kufupisha maisha yako.

Mvulana anampoteza msichana: Mwanamume fulani mwenye cheo anamteka nyara mwanamke huyo mrembo kutoka kwenye kasri. Mwana wa mfalme anafunga safari hatari ili kumtafuta mrembo huyo. Msemaji wa Shirika la Waandishi wa Riwaya za Mahaba la Marekani anasema hivi: “Hadithi hiyo inapaswa kuzungumzia watu wawili wanaopendana na wanaofanya juu chini ili uhusiano wao ufanikiwe.” Katika riwaya nyingi, wasomaji hujua kwamba uhusiano huo utafaulu. Vikwazo vyovyote vile hushindwa.

Katika mahusiano halisi, matatizo husababishwa ama na watu walio katika uhusiano huo au na watu wengine. Huenda yakasababishwa na pesa, kazi, watu wa ukoo, na marafiki. Matatizo hutokea pia wakati mmoja wao hatimizi matarajio ya mwingine. Katika hadithi za kuwaziwa, kasoro za wahusika huwa ndogo tu, lakini sivyo ilivyo katika mahusiano halisi. Isitoshe, kwa kuwa watu wanapendana kikweli hiyo haimaanishi kwamba mambo yatakuwa shwari licha ya majaribu au licha ya kwamba watu hao wana maoni, malezi, tamaa, na nyutu tofauti. Upendo unahusisha ushirikiano, unyenyekevu, upole, subira, na ustahimilivu. Hizo ni sifa ambazo lazima mtu akuze.—1 Wakorintho 13:4-7.

Mvulana anampata msichana tena. Mwana wa mfalme anamwokoa mwanamke mrembo na kumfukuza yule mwanamume mwenye cheo. Wenzi hao wanaoana na kuishi raha mustarehe. Mhariri mmoja wa riwaya za mahaba aliwashauri hivi wanaotaka kuwa waandishi: “Umalizio wako unapaswa kuonyesha kwamba wenzi hao waliishi raha mustarehe. . . . Msomaji anapaswa kuridhika kwamba wenzi hao wanaishi pamoja na wana furaha.” Mara chache sana riwaya za mahaba huzungumza kuhusu maisha ya wenzi hao miaka kadhaa baada ya ndoa. Katika kipindi hicho huenda kutoelewana, magumu na matatizo mengine yakawa yamejaribu uhusiano wao. Kama takwimu za talaka zinavyoonyesha, baada ya muda ndoa nyingi hushindwa kustahimili majaribu na hivyo huvunjika.

Naam, upendo wa riwaya hauhitaji jitihada; upendo halisi si mchezo. Kuelewa tofauti kati ya aina hizo mbili za upendo kutakulinda dhidi ya kutarajia mambo yasiyowezekana. Pia kutakusaidia usitoe ahadi harakaharaka ambazo utajutia baadaye. Makala inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kusitawisha upendo wa kweli usio na ubinafsi na jinsi unavyoweza kuwa mtu anayependeka kwa urahisi.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Watu ambao hawawapendi wengine sana hawapendwi sana

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Upendo wa riwaya hauhitaji jitihada; upendo halisi si mchezo

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Mashujaa wa Mahaba—wa Kiume na wa Kike

Nchini Marekani, waandishi wa riwaya za mahaba hupata mabilioni ya dola kila mwaka. Karibu riwaya zote zinazouzwa nchini humo ni za mahaba. Kulingana na takwimu zilizochapishwa na Shirika la Waandishi wa Riwaya za Mahaba la Marekani, mambo matatu ambayo wasomaji, ambao asilimia 90 kati yao ni wanawake hutafuta katika mashujaa wa kiume ni misuli, sura yenye kuvutia, na akili. Mambo matatu yanayopendwa katika mashujaa wa kike ni akili, utu wenye nguvu, na urembo.

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Ni mara chache sana vyombo vya habari hufundisha mambo sahihi kuhusu upendo