Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kukataa Ngono Shuleni?

Nawezaje Kukataa Ngono Shuleni?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kukataa Ngono Shuleni?

“Kila siku, vijana huzungumza kuhusu ngono. Wasichana huwashawishi wavulana, nao hufanya ngono shuleni.”—Eileen, 16.

“Shuleni kwetu, walawiti hufanya mambo yasiyo ya adili mbele ya vijana wengine bila kujali.”—Michael, 15. *

JE, WANADARASA wenzako huzungumza daima kuhusu ngono? Je, wengine hata hufanya ngono? Ikiwa ndivyo, basi huenda ukahisi kama msichana mmoja ambaye alilinganisha shule yao na “kufanya kazi mahali sinema chafu ya watu wazima inaigizwa.” Kwa kweli, vijana wengi shuleni hupata nafasi tele kuzungumza kuhusu ngono au hata kuifanya.

Huenda ukawasikia wanadarasa wenzako wakizungumza kuhusu kufanya mapenzi, maneno yanayomaanisha kufanya ngono bila kuwajibika kokote. Katika visa fulani vijana hufanya mapenzi na watu wasiowajua vizuri. Katika visa vingine wao hufanya ngono na watu wasiowajua kabisa ambao wamekutana nao kwenye Intaneti. Katika hali nyingine lengo la kufanya mapenzi si kusitawisha uhusiano wa kimapenzi. “Watu hufanya mapenzi kwa sababu tu walishindwa kuzuia hisia zao,” anasema Danielle mwenye umri wa miaka 19.

Si ajabu kwamba katika shule nyingi watu hupenda sana kuzungumza kuhusu kufanya mapenzi. “Baada ya kila mwisho-juma, wanafunzi huzungumza sana kuhusu kufanya mapenzi, nao husimuliana waziwazi mambo waliyofanya,” akaandika msichana mmoja mwenye umri wa miaka 17 katika gazeti la shule yake.

Ikiwa unajaribu kuishi kulingana na viwango vya Biblia, huenda ukahisi kuwa umetengwa kama unazungukwa na watu ambao huzungumza tu kuhusu ngono. Ikiwa hujiungi nao, unaweza kudhihakiwa kwa urahisi. Kwa kiwango fulani hilo ni jambo linalotazamiwa, kwani Biblia husema kwamba iwapo wengine hawaelewi msimamo wako, wanaweza ‘kukutukana.’ (1 Petro 4:3, 4) Hata hivyo, hakuna anayependa kudhihakiwa. Kwa hiyo, unawezaje kukataa ngono shuleni na kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu msimamo wako? Kwanza, ni muhimu kuelewa sababu inayofanya watu watamani ngono sana.

Jichunguze

Unapobalehe, unapitia mabadiliko mengi, kimwili na kihisia. Unapopitia kipindi hicho, unakuwa na tamaa ya ngono yenye nguvu sana. Uwe na hakika kwamba hilo ni jambo la kawaida kabisa. Kwa hiyo, ukihisi kwamba unavutiwa na watu wa jinsia tofauti, usikate kauli kwamba wewe ni mbaya au huwezi kudumisha usafi wa maadili. Unaweza kuwa safi kiadili ukitaka!

Mbali na kupambana na hisia na mabadiliko ya kubalehe, kuna jambo jingine unalohitaji kutambua. Wanadamu wote wana mwelekeo wa kufanya mabaya kwa kuwa wao si wakamilifu. Hata mtume Paulo alikiri hivi: “Mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.” Paulo alisema kwamba kutokamilika kwake kulimfanya ajihurumie. (Waroma 7:23, 24) Lakini alishinda vita hivyo, nawe pia unaweza!

Waelewe Wanadarasa Wenzako

Kama ilivyotajwa awali, wanadarasa wenzako wanaweza kuzungumza kuhusu ngono wakati wote au wajivune kuhusu jinsi walivyofanya ngono. Unapaswa kujihadhari na uvutano wao usiofaa. (1 Wakorintho 15:33) Lakini huhitaji kuwaona wanadarasa wenzako kuwa maadui. Kwa nini?

Wanadarasa wenzako wana tamaa zilezile kama wewe. Wao pia wana mwelekeo wa kufanya mabaya. Lakini tofauti na wewe, huenda wengine wao ‘wanapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ Au huenda wakawa wanatoka katika familia zisizo na “upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1-4) Huenda baadhi ya wanadarasa wenzako hawakufunzwa nidhamu na maadili na wazazi wenye upendo.—Waefeso 6:4.

Kwa kuwa hawaongozwi na hekima inayotoka chanzo kikuu, yaani, Neno la Mungu, Biblia, huenda wanadarasa wenzako wasitambue madhara yanayoweza kutokea wanapojiruhusu waongozwe na tamaa zao. (Waroma 1:26, 27) Ni kana kwamba wazazi wao wamewanunulia gari lenye nguvu na kuwaruhusu waliendeshe kwenye barabara kuu yenye magari mengi, lakini hawakuwafundisha jinsi ya kuliendesha. Huenda wakasisimuliwa kwa muda mfupi, lakini msiba hauna budi kutokea. Kwa hiyo, unaweza kufanya nini wanadarasa wenzako wanapoanza kuzungumza kuhusu ngono au watakapojaribu kukushawishi ufanye ngono?

Kataa Mazungumzo Yasiyo ya Adili

Wanadarasa wenzako wakianza kuzungumza kuhusu ngono, huenda ukashawishiwa kusikiliza au hata kujiunga nao, ili tu usionekane kuwa tofauti. Lakini fikiria watakuwa na maoni gani kukuhusu. Kupendezwa na mazungumzo yao kutaonyesha wewe ni mtu wa aina gani au unataka kuwa mtu wa aina gani.

Kwa hiyo, unapaswa kufanya nini wakianza kuzungumza kuhusu ngono? Je, unapaswa tu kuamka na kuondoka? Bila shaka! (Waefeso 5:3, 4) Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Kwa hiyo, kuondoka, si kukosa heshima, bali ni tendo la hekima.

Kwa kweli, hupaswi kuhisi vibaya unapoondoka mahali ambapo kuna mazungumzo kuhusu ngono. Bila shaka, kuna mazungumzo mengine ambayo yangefanya uondoke bila kuona haya, hasa ikiwa hupendezwi na mambo yanayosemwa au ikiwa hutaki kujihusisha nayo. Kwa mfano, tuseme baadhi ya wanadarasa wenzako wanaanza kuzungumza kuhusu kuiba kwa kutumia nguvu. Je, ungeendelea kukaa hapo usikilize njama yao? Ikiwa ungekaa, ungeonekana kuwa mshiriki wao. Kwa hiyo, kwa hekima ungeondoka. Fanya hivyohivyo wanapoanza kuzungumza kuhusu ngono. Mara nyingi unaweza kuondoka bila kujifanya kuwa mtakatifu na hivyo kufanya wakudhihaki.

Ni kweli, huenda isiwe rahisi nyakati zote kujiondoa katika hali kama hiyo. Kwa mfano, vijana waliopangwa kuketi karibu nawe darasani wanaweza kujaribu kukuhusisha katika mazungumzo kuhusu ngono. Wanapofanya hivyo, unaweza kuwaambia kwa upole lakini ukiwa imara waache kukukengeusha. Ikiwa hilo halifaulu, unaweza kufanya kama Brenda. Anasema hivi: “Nilimwomba mwalimu kwa busara anihamishe.”

Uwe na Utambuzi

Baada ya muda, baadhi ya wanadarasa wenzako watauliza sababu inayofanya usipendezwe na mazungumzo yao machafu. Wakiuliza kuhusu maadili yako, uwe na utambuzi unapojibu. Ni kweli, huenda wengine wakakuuliza ili tu wakudhihaki badala ya kuelewa maoni yako. Lakini ikiwa anayeuliza kwa kweli angependa kujua, zungumza kwa kujivunia imani yako. Vijana wengi wametumia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi ili kuwasaidia wanadarasa wenzao waelewe manufaa ya kuishi kulingana na viwango vya Biblia. *

Azimia

Unapaswa kufanya nini ikiwa mwanafunzi mwenzako ni mwenye ujasiri kiasi cha kujaribu kukugusa au kukubusu? Ukimruhusu afanye hivyo, unaweza kumpa ujasiri wa kuendelea kufanya jambo hilo baya. Biblia inazungumza kuhusu kijana aliyemruhusu mwanamke mwenye maadili mapotovu amshike na kumbusu. Alimwacha amtongoze. Matokeo yalikuwaje? “Ghafula kijana huyo akamfuata, kama ng’ombe-dume anayeenda machinjoni.”—Methali 7:13-23.

Kwa kutofautisha, fikiria jinsi Yosefu alivyoshughulikia hali kama hiyo. Mke wa bwana wake aliendelea kujaribu kumtongoza, lakini alikataa katakata. Mwishowe alipojaribu kumkamata, Yosefu alichukua hatua mara moja na kukimbia.—Mwanzo 39:7-12.

Kama Yosefu, huenda ukahitaji kuchukua hatua madhubuti mwanadarasa mwenzako au mtu mwingine anapojaribu kukugusa kwa njia isiyofaa. “Kijana anapojaribu kunigusa mimi humwambia aache,” anasema Eileen. “Ikiwa haachi, mimi humwambia kwa sauti ya juu aniache.” Eileen anaongeza kusema hivi kuhusu wavulana katika shule yake: “Hawawezi kukuheshimu usipowalazimisha.

Wewe pia unaweza kuheshimiwa na wanadarasa wenzako iwapo utakataa kusikiliza wanapozungumza mambo machafu. Inapofaa, waeleze kwa heshima msimamo wako wa maadili, na ukatae kabisa wanapokutendea kwa njia isiyo ya adili. Kwa kufanya hivyo, utajiheshimu na jambo la maana hata zaidi, utapata kibali cha Yehova!—Methali 27:11.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unaweza kusema nini ili uondoke mahali penye mazungumzo machafu?

▪ Utasema na kufanya nini iwapo mwanadarasa anakutendea kwa njia isiyo ya adili?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 22 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mazungumzo yanapohusu ngono haramu, ondoka

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kataa katakata unapotendewa kwa njia isiyo ya adili