Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ninataka Kumtumikia Mungu Kabla Sijafa’

‘Ninataka Kumtumikia Mungu Kabla Sijafa’

‘Ninataka Kumtumikia Mungu Kabla Sijafa’

SIMULIZI LA MAMIE FREE

MNAMO 1990, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka nchini Liberia. Vita vilipozidi kupamba moto, msichana mwenye umri wa miaka 12 anayeitwa Mamie, wa kabila la Krahn pamoja na familia yao, hawangeweza kutoka nyumbani kwao huko Monrovia ambao ndio mji mkuu wa nchi hiyo. Mamie anasema: “Tulisikia mlipuko katika nyumba ya jirani. Bomu lilikuwa limeanguka katika nyumba hiyo na kuiwasha moto. Moto huo ulishika nyumba yetu pia.” Vita vilipokuwa vikiendelea, Mamie, mama yake, na ndugu mdogo wa mama yake walitoroka.

“Kwa ghafula, niligongwa na kitu fulani,” Mamie anakumbuka.

“Kuna nini?” mama yangu akauliza.

“Nimegongwa na kitu fulani! Ninafikiri ni risasi,” nikajibu.

Kwa uchungu Mamie alianguka na kusali hivi: “Tafadhali Mungu nisikilize. Ninafikiri niko karibu kufa, lakini ninataka kukutumikia kabla sijafa.” Kisha akapoteza fahamu.

Wakifikiri alikuwa amekufa, majirani walitaka kumzika Mamie katika ufuo uliokuwa karibu. Hata hivyo, mama yake alisisitiza apelekwe hospitali iliyokuwa karibu. Kwa kusikitisha, hospitali hiyo haikuwa na vifaa vya kutosha kuwatunza wanaume, wanawake, na watoto wengi waliokuwa wamejeruhiwa. Mjomba wa Mamie ambaye pia alikuwa amejeruhiwa, alikufa usiku huo, lakini Mamie aliokoka akiwa amepooza kutoka kiunoni kwenda chini.

Aliendelea kuvuja damu kwa ndani na kuwa na uchungu mwingi. Miezi minne baadaye madaktari walimpiga picha ndani ya mwili ili kutafuta risasi hiyo. Ilikuwa katikati ya moyo na mapafu yake. Ingekuwa hatari sana kumpasua, hivyo mama yake alimpeleka kwa daktari wa kienyeji. Mamie anakumbuka: “Daktari huyo alinikata kwa wembe kisha akatia mdomo wake kwenye kidonda na kujaribu kunyonya risasi hiyo. Daktari huyo alisema hivi, ‘Ndiyo hii’ huku akitoa risasi mdomoni. Tulimlipa na kuondoka.”

Lakini daktari huyo alikuwa amedanganya. Picha zilipopigwa baadaye zilionyesha kwamba risasi hiyo bado ilikuwapo. Kwa hiyo Mamie na mama yake walirudi kwa daktari huyo, naye aliwasadikisha kwamba picha zingeonyesha kwamba risasi imeondolewa baada ya miezi tisa. Walirudi nyumbani na kungoja. Wakati huo, Mamie alitumia dawa mbalimbali kutuliza uchungu. Picha nyingine zilipigwa miezi tisa baadaye na kuonyesha kuwa risasi ilikuwa bado ndani. Daktari huyo alitoroka.

Mamie aliishi na risasi hiyo mwilini kwa miezi 18. Mtu fulani wa ukoo alimpeleka kwa mchawi wa kike. Badala ya kusaidia, alisema kwamba Mamie au mama yake wangekufa siku fulani hususa. Kufikia wakati huu Mamie alikuwa na miaka 13. “Nililia bila kukoma,” anasema Mamie. “Lakini siku iliyokuwa imewekwa ilipofika, hakuna aliyekufa.”

Kisha mjomba mmoja wa Mamie akampeleka kwa kiongozi fulani wa kanisa ambaye alidai kwamba aliona njozi iliyoonyesha kupooza kwa Mamie hakukusababishwa na risasi bali kulitokana na kurogwa. Aliahidi kwamba ikiwa Mamie angefuata desturi fulani za kidini, angetembea baada ya juma moja. Mamie anaeleza: “Nilioga mara nyingi ili kujitakasa kwa maji ya bahari, nikafunga, na kila siku saa sita za usiku nilijibingirisha kwenye sakafu kwa muda wa saa nyingi. Lakini jitihada zote hizo ziliambulia patupu, na hali yangu haikuboreka.”

Hatimaye, hospitali nyingine zilifunguliwa tena, na mwishowe Mamie akafaulu kutolewa risasi hiyo mwilini. Alikuwa amevumilia uchungu usiopungua kwa zaidi ya miaka miwili. Anakumbuka hivi: “Baada ya upasuaji ni kana kwamba uchungu ulipotea nami ningeweza kupumua kwa urahisi zaidi. Ingawa bado nilikuwa nimepooza kwa kiasi fulani, ningeweza kusimama kwa kutumia kifaa fulani cha kunitegemeza.”

Mamie Akutana na Mashahidi wa Yehova

Juma moja baada ya upasuaji, mama ya Mamie alikutana na Mashahidi wawili wa Yehova. Akijua kwamba binti yake alipenda kusoma Biblia aliwakaribisha Mashahidi hao nyumbani. Mara moja Mamie alikubali funzo la Biblia. Hata hivyo, miezi kadhaa baadaye alirudi hospitalini naye hakuweza kuwasiliana na Mashahidi.

Lakini bado Mamie alikuwa na kiu ya kupata ujuzi wa Biblia. Kwa hiyo, kiongozi wa kanisa fulani alipomwambia angemfunza, alikubali mara moja. Wakati wa kipindi kimoja cha shule ya watoto ya Jumapili, mtoto mmoja alimwuliza mwalimu, “Je, Yesu ni sawa na Mungu?”

Mwalimu alimjibu: “Ndiyo, wao ni sawa. Lakini Yesu si sawa kabisa na Mungu.”

Mamie alijiuliza: ‘Eti si sawa kabisa? Jambo hilo halipatani na akili. Kuna kasoro fulani hapa.’ Kwa kuwa hakuridhika kwamba alikuwa akijifunza ukweli wa Biblia, mwishowe Mamie aliacha kushirikiana na kanisa hilo.

Mnamo 1996, vita vilizuka tena Monrovia. Mamie alipoteza tena washiriki wawili wa familia yao, na nyumba yao ikateketezwa mara ya pili. Miezi michache baadaye, Mashahidi wawili walikutana na Mamie walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba. Mamie alianza tena kujifunza Biblia. Alipohudhuria mkutano wake wa kwanza, alishangazwa kuona kwamba kila mtu, kutia ndani wazee wa kutaniko, walisaidia kusafisha Jumba la Ufalme. Baadaye mwaka huohuo, alifurahi kuhudhuria mojawapo ya Makusanyiko ya Wilaya ya “Wajumbe wa Amani ya Kimungu,” na huo ndio uliokuwa mkusanyiko wa kwanza mkubwa wa Mashahidi wa Yehova aliowahi kutembelea.

Mamie anasema hivi: “Nilivutiwa sana. Mashahidi walipendana kikweli ingawa walikuwa wa makabila tofauti. Kila kitu kilipangwa kwa utaratibu kabisa.”

Anatimiza Tamaa Yake ya Kumtumikia Mungu

Mnamo 1998, vita vilitokea tena na kumlazimisha Mamie na mama yake wakimbilie nchi jirani ya Côte d’Ivoire, ambako waliishi katika Kambi ya Wakimbizi ya Peace Town pamoja na Waliberia wengine 6,000 hivi. Mamie aliendelea kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi na kufanya maendeleo haraka. Punde si punde, alitaka kuwaeleza wengine yale aliyokuwa ameamini. Ili aweze kuhubiri hadharani, ndugu na dada zake wa kiroho walimsukuma katika kiti chake cha magurudumu. Katika njia hiyo Mamie alifaulu kuwahubiria wakimbizi wengi kwa njia nzuri.

Hata ingawa hali yake ya kimwili ilifanya iwe vigumu kufika kwenye Jumba la Ufalme, ambalo lilikuwa kilometa sita kutoka mahali alipoishi, Mamie alihudhuria mikutano yote. Mei 14, 2000, alisafiri zaidi ya kilometa 190 ili kuhudhuria kusanyiko la pekee na kuonyesha wakfu wake kwa Mungu kupitia ubatizo wa maji. (Mathayo 28:19, 20) Mamie alibebwa hadi kwenye mto na kuingizwa majini huku watazamaji wengi wakitokwa na machozi. Uso wake uling’aa kwa shangwe alipoinuliwa kutoka majini.

Sasa akiwa katika kambi ya wakimbizi huko Ghana, Mamie ana mradi wa kuwa painia wa kawaida, au mweneza-injili wa wakati wote. Mama yake pia ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na sasa anawaeleza wengine mambo ambayo amejifunza. Wote wawili wanatazamia kwa hamu wakati ulioahidiwa katika Neno la Mungu ambapo “kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.”—Isaya 35:5-7.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Risasi iliyotolewa katika mwili wa Mamie

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mamie akibebwa kupelekwa kwenye mto akabatizwe

[Picha katika ukurasa wa 23]

Akiongoza funzo la Biblia na mama yake, Emma