Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Yesu Alikufa Msalabani?

Je, Kweli Yesu Alikufa Msalabani?

Maoni ya Biblia

Je, Kweli Yesu Alikufa Msalabani?

MSALABA ni mojawapo ya mifano ya kidini inayojulikana sana. Mamilioni wameuabudu, wakiuona kuwa kifaa kitakatifu ambacho Yesu aliuawa juu yake. Mwandikaji Mkatoliki ambaye pia ni mchunguzi wa vitu vya kale, Adolphe-Napoleon Didron, alisema hivi: “Msalaba umepewa ibada inayokaribia, au kama ile anayopewa Kristo; kipande hiki kitakatifu cha mbao kimepewa heshima inayokaribia ile ambayo Mungu Mwenyewe hupewa.”

Watu fulani husema kwamba msalaba huwafanya wamkaribie Mungu zaidi wanaposali. Wengine huutumia kama hirizi, wakidhani kwamba utawalinda na maovu. Lakini, je, Wakristo wanapaswa kuabudu msalaba? Je, kweli Yesu alikufa msalabani? Biblia inafundisha nini kuhusu jambo hilo?

Msalaba Hufananisha Nini?

Muda mrefu kabla ya Ukristo, Wababiloni wa kale walitumia misalaba katika ibada kama mifano ya mungu wa uzazi aliyeitwa Tamuzi. Matumizi ya msalaba yalienea hadi Misri, India, Siria, na China. Kisha, karne nyingi baadaye, Waisraeli walichanganya ibada yao kwa Yehova na ibada ya mungu wa uwongo Tamuzi. Biblia inasema kwamba ibada ya aina hiyo ni ‘chukizo.’—Ezekieli 8:13, 14.

Masimulizi ya Injili ya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana yanatumia neno la Kigiriki stau·rosʹ yanaporejelea kifaa ambacho Yesu aliuawa juu yake. (Mathayo 27:40; Marko 15:30; Luka 23:26) Neno stau·rosʹ linarejelea nguzo iliyonyooka au mti. Kitabu The Non-Christian Cross cha J. D. Parsons, kinaeleza hivi: “Hakuna hata sentensi moja katika yale maandishi mengi yanayofanyiza Agano Jipya katika Kigiriki cha kwanza, inayotoa hata uthibitisho usio wa moja kwa moja unaoonyesha kwamba mti uliotumiwa katika kisa cha Yesu ulikuwa tofauti na miti ya kawaida; hakuna uthibitisho kwamba mti huo haukuwa kipande kimoja cha mti bali vipande viwili vilivyopigiliwa misumari pamoja kama vile msalaba.”

Kama inavyoonyeshwa kwenye Matendo 5:30, mtume Petro alitumia neno xyʹlon, linalomaanisha “mti,” kama kisawe cha stau·rosʹ, kumaanisha kipande cha kawaida cha mti au mbao iliyo wima bali si msalaba wenye vipande viwili vya mbao. Miaka 300 hivi baada ya kifo cha Yesu watu fulani waliodai kuwa Wakristo walianzisha wazo la kwamba Yesu aliuawa juu ya msalaba wenye vipande viwili vya mbao. Hata hivyo, wazo hilo lilitegemea mapokeo na kutumiwa vibaya kwa neno la Kigiriki stau·rosʹ. Inapaswa kuzingatiwa kwamba michoro fulani ya kale ilionyesha kwamba Waroma waliwaua watu juu ya nguzo ya mbao au mti.

“Jilindeni na Sanamu”

Suala muhimu zaidi kwa Wakristo wa kweli linapaswa kuwa kama inafaa kuabudu kifaa kilichotumiwa kumuua Yesu. Iwe aliuawa kwenye mti wa mateso, msalaba, kwa mshale, au kisu, je, inafaa kutumia kifaa hicho katika ibada?

Tuseme mpendwa wako aliuawa kikatili na silaha iliyotumiwa ikatolewa kortini kama ushahidi. Je, ungejaribu kuchukua silaha hiyo, uipige picha, na kutokeza nakala nyingi za picha hiyo na kuwapa watu? Je, ungetengeneza mifano mbalimbali ya silaha hiyo? Je, ungetengeneza vito kutokana na silaha hiyo? Au je, ungekubali vito hivyo vitengenezwe kiwandani na kuuziwa marafiki na watu wa ukoo ili waviabudu? Huenda ikawa ungechukizwa na wazo hilo! Lakini, hivyo ndivyo watu wamefanya kuhusiana na msalaba!

Isitoshe, kutumia msalaba katika ibada ni sawa na kutumia sanamu, jambo linaloshutumiwa katika Biblia. (Kutoka 20:2-5; Kumbukumbu la Torati 4:25, 26) Mtume Yohana alionyesha kwa usahihi mafundisho ya Ukristo wa kweli alipowaonya Wakristo wenzake hivi: “Jilindeni na sanamu.” (1 Yohana 5:21) Na Wakristo hao walifanya hivyo hata walipokabili kifo katika viwanja vya michezo vya Roma.

Hata hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza waliheshimu sana kifo cha kidhabihu cha Kristo. Vivyo hivyo leo, ingawa kifaa kilichotumiwa kumtesa na kumwua Yesu hakipaswi kuabudiwa, Wakristo wa kweli hukumbuka kifo cha Yesu ambacho kupitia hicho Mungu ameandaa wokovu kwa wanadamu wasio wakamilifu. (Mathayo 20:28) Wonyesho huo mkuu wa upendo wa Mungu utawaletea watu wanaopenda kweli baraka nyingi, kutia ndani tarajio la kuishi milele.—Yohana 17:3; Ufunuo 21:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Michoro fulani ya zamani inaonyesha kwamba Waroma waliwaua watu juu ya nguzo moja ya mbao

[Hisani]

Rare Books Division, The New York Public Library, Astor, Lenox and Tilden Foundations