Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuwa Mwenye Kufanya Amani?

Je, Inawezekana Kuwa Mwenye Kufanya Amani?

Maoni ya Biblia

Je, Inawezekana Kuwa Mwenye Kufanya Amani?

KATIKA mahubiri yake maarufu zaidi, Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” Pia alisema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5, 9) Kuwa mwenye kufanya amani kunahusisha mengi zaidi ya kuwa mtulivu tu. Mtu mwenye kufanya amani huchukua hatua ya kuendeleza amani.

Je, leo watu wanaweza kutii maneno ya Yesu yaliyonukuliwa hapa juu? Watu fulani hufikiri kwamba ili kufanikiwa katika ulimwengu wa leo, lazima mtu awe mwenye kuogepesha, mchokozi, na hata mjeuri. Je, ni jambo la hekima kulipiza kisasi unapochokozwa? Au inawezekana kuwa mwenye kufanya amani? Na tuchunguze sababu tatu ambazo hufanya tufikirie maneno haya ya Yesu: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.”

▪ UTULIVU WA MOYO “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama,” yasema Methali 14:30. Ripoti nyingi za kitiba zinaonyesha kwamba hasira na uhasama zinaweza kusababisha kiharusi na ugonjwa wa moyo. Hivi majuzi, lilipokuwa likizungumza kuhusu watu wenye ugonjwa wa moyo, jarida moja la kitiba lililinganisha mlipuko wa hasira na sumu. Pia jarida hilo lilisema kwamba “kukasirika sana kunaweza kumfanya mtu awe mgonjwa sana.” Hata hivyo, wale wanaofuatia amani, wanaweza kusitawisha “moyo mtulivu” na kunufaika.

Tuna mfano wa Jim, mwenye umri wa miaka 61 ambaye sasa huwafundisha Biblia watu wanaozungumza Kivietnamu. Anasema: “Baada ya kufanya kazi jeshini kwa miaka sita na kupigana mara tatu huko Vietnam, nilielewa vizuri jeuri, hasira, na kufadhaika. Mambo niliyofanya zamani yalinisononesha na kunikosesha usingizi. Punde si punde, nilipatwa na ugonjwa wa tumbo na tatizo la mfumo wa neva.” Ni nini kilichomtuliza? Anajibu: “Kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kuliokoa maisha yangu. Nimekuwa na moyo mtulivu kwa kujifunza kusudi la Mungu la kuleta dunia mpya yenye amani na pia kujifunza jinsi ninavyoweza kujivika ‘utu mpya.’ Afya yangu imeboreka sana kwa sababu ya mambo hayo.” (Waefeso 4:22-24; Isaya 65:17; Mika 4:1-4) Kwa sababu ya mambo ambayo wamepitia maishani, watu fulani wamekata kauli kwamba kuwa mwenye kufanya amani kunaweza kuboresha afya ya kihisia, kimwili, na kiroho.—Methali 15:13.

▪ MAHUSIANO YENYE KUFURAHISHA ZAIDI Tutakuwa na mahusiano mazuri na wengine tukiwa watu wenye kufanya amani. Biblia inasema kwamba “hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano” yanapaswa ‘kuondolewa mbali . . . , pamoja na ubaya wote.’ (Waefeso 4:31) Mara nyingi watu wenye kutisha hufanya wengine wasitake kuwa na uhusiano wa karibu nao, na hivyo hukosa marafiki wenye kutegemeka. Methali 15:18 inasema: “Mtu mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, lakini yule ambaye hakasiriki upesi hutuliza mabishano.”

Andy, mzee Mkristo mwenye umri wa miaka 42 anayeishi New York City, alikulia katika mazingira yenye uhasama. Anasema: “Niliingia ulingoni na kuzoezwa kupigana ndondi nikiwa na umri wa miaka minane. Sikuona wapinzani wangu kuwa watu. Badala yake, nilijiambia hivi ‘wapige au upigwe.’ Muda si muda, nilijiunga na genge fulani. Tulijihusisha na mapigano mengi sana ya mtaani. Watu wamewahi kunielekezea bunduki kichwani na kunitisha kwa visu. Nilikuwa na woga na wasiwasi kuelekea rafiki zangu.”

Ni nini kilichomfanya Andy afuatie amani? Anasema: “Siku moja nilihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, na mara moja niliona jinsi watu hao wanavyopendana. Tangu wakati huo, kushirikiana na watu hao wanaopenda amani kumenisaidia kusitawisha moyo mtulivu, na hatimaye kulinisaidia niondolee mbali mawazo yangu ya zamani. Nimepata marafiki wengi wa kudumu.”

▪ TUMAINI LA WAKATI UJAO Sababu muhimu zaidi ya kuwa mwenye kufanya amani ni hii: Inaonyesha kwamba tunaheshimu mapenzi ya Muumba wetu ambayo ametufunulia. Neno la Mungu, Biblia, linatuhimiza: “Utafute amani, na kuifuatia.” (Zaburi 34:14) Mtu anaweza kuwa na urafiki wa karibu na Yehova Mungu akikiri kwamba Mungu yuko kisha ajifunze na kutii mafundisho yake yenye kutoa uhai. Tukiwa na uhusiano huo wa karibu pamoja naye, tutapata “amani ya Mungu.” Hiyo ndiyo amani bora zaidi hata kuwe na magumu gani maishani.—Wafilipi 4:6, 7.

Isitoshe, tukiwa watu wenye kufanya amani, tunamwonyesha Yehova tunataka kuwa watu wa aina gani. Tunaweza kumthibitishia Mungu sasa kwamba tutajipatanisha na viwango vyake ili kuishi katika ulimwengu wake mpya wenye amani ambao ameahidi. Mungu atakapoondoa waovu na kuwawezesha walio na tabia-pole ‘wairithi nchi’ kama alivyosema Yesu, tutaweza kujionea jambo hilo. Hiyo itakuwa baraka iliyoje!—Zaburi 37:10, 11; Methali 2:20-22.

Naam, ni wazi kwamba kuna faida ya kutii maneno ya Yesu kwamba “wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” Tunaweza kuwa na moyo mtulivu, mahusiano mazuri, na tumaini thabiti la wakati ujao. Tunaweza kupata baraka hizo tukifanya yote tuwezayo ‘kuwa wenye kufanya amani na watu wote.’—Waroma 12:18.

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Afya yangu imeboreka sana.”—Jim

[Picha katika ukurasa wa 29]

“Nimepata marafiki wengi wa kudumu.”—Andy