Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Jinsi ya Kupata Kazi na Kuidumisha (Julai 8, 2005) Nilishukuru kwa pendekezo lenu kwamba nichunguze kila nafasi ya kazi inayotokea hata kama inaonekana kuwa kazi ya hali ya chini. Hivi majuzi nilitaka kuacha kazi yangu ya wakati wote na kufanya kazi ya muda ili nitumie wakati mwingi zaidi katika huduma ya Kikristo. Lakini nilikuwa nikichagua sana kazi. Kisha nilipewa kazi nyingine, ambayo nilikubali. Ni kazi ya hali ya chini, lakini ninajitahidi kuridhika nayo. Angalau hainichoshi akili ninaporudi nyumbani, kwa hiyo ninaweza kukaza fikira zangu ninapojifunza Biblia.

M. I., Japani

Mei Mosi—Ina Maana Gani Kwako? (Aprili 22, 2005) Niko karibu kumaliza shule ya sekondari na sikukuu ya Mei Mosi huadhimishwa shuleni mwetu kila mwaka. Wanafunzi hufanya mazoezi ya mwisho ya mchezo wa kuigiza kabla hawajauigiza rasmi, na wanafunzi wote wa sekondari na wale wa darasa la saba na la nane huombwa wahudhurie mazoezi hayo. Niliwahi kuhudhuria mazoezi hayo hapo awali, lakini jambo hilo lilisumbua dhamiri ya dada yangu. Makala hii ilinisaidia kutambua kwamba haikufaa Mkristo kuhudhuria mazoezi hayo! Asanteni sana. Makala hiyo ilifika kwa wakati barabara!

C. C., Marekani

Kukabili Ugonjwa kwa Ucheshi (Aprili 22, 2005) Nimekuwa na kansa ya mfuko wa mayai kwa muda wa miaka sita sasa, na nimefanyiwa upasuaji mara kadhaa na kupewa matibabu ya kemikali. Sawa na Conchi, ninajaribu kuunga mkono kutaniko langu na kuhudhuria mikutano yote na makusanyiko kadiri niwezavyo. Ni vigumu kuishi na kansa, kwa hiyo ninashukuru kwa maelezo ya Conchi kuhusu jinsi ambavyo wagonjwa wa kansa kama sisi tunaweza kukabiliana na habari mbaya ambazo sisi hupata mara kwa mara kutoka kwa madaktari. Nilitiwa moyo kwelikweli na simulizi la Conchi!

B. F., Marekani

Nina ugonjwa wa lupus, na pindi moja nilipoteza kumbukumbu kwa muda fulani. Nilipokuwa nikipata nafuu, nilijaribu kudumisha ucheshi. Hivi majuzi, nilipolazwa hospitalini kwa sababu ya kidonda cha tumbo, nilijitahidi kufanya hivyohivyo. Ninakubaliana na maneno ya Conchi aliyesema kwamba, “Ugonjwa si jambo la kuchekesha, lakini unapaswa kujitahidi kudumisha ucheshi wako.”

M. A., Venezuela

Kuutazama Ulimwengu (Julai 8, 2005) Ningependa kusema kwamba wataalamu wengi wa lishe hawaungi mkono maoni yaliyonukuliwa ya Dakt. Sullivan katika sehemu iliyokuwa na kichwa, “Madawa ya Vitamini na Kansa.” Ripoti za vichapo vingi vya sayansi na uchunguzi mwingi unaonyesha kwamba dawa mlizotaja zimesaidia sana kuzuia na hata kutibu aina fulani za kansa. Ninahisi kwamba kuchapisha habari kama hiyo ambayo inaunga mkono upande mmoja kunaweza kuhatarisha msimamo wa Amkeni! wa kutounga mkono upande wowote.

A. B., Uholanzi

“Amkeni!” lajibu: Yaonekana kwamba kama msomaji huyu anavyosema, uchunguzi umeonyesha kuwa dawa zilizotajwa katika makala yetu nyakati fulani zimewasaidia wagonjwa wa kansa. Tunaomba radhi ikiwa tulichapisha habari zisizoeleweka. “Amkeni!” haliungi mkono upande wowote kuhusiana na matibabu. Hata ingawa tunawachapishia wasomaji wetu makala zinazohusu matibabu, hiyo haimaanishi kwamba tunaunga mkono habari hizo. Vivyo hivyo, tunaponukuu kichapo au mtaalamu wa nyanja fulani, tunajua kwamba—kama ambavyo imetukia mara nyingi—huenda vichapo vingine na wataalamu wengine wakawa na maoni tofauti. Tunataka wasomaji wetu wajiamulie wenyewe mambo yanayohusu afya yao.