Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ni Lazima Nisome?

Kwa Nini Ni Lazima Nisome?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Ni Lazima Nisome?

“Sipendi kusoma. Afadhali nitazame televisheni.” —Margarita, 13, Urusi.

“Nikiambiwa nichague kati ya kusoma kitabu na kucheza mpira wa vikapu, afadhali kucheza.” —Oscar, 19, Marekani.

IKIWA umesoma sentensi hii, basi huenda unatambua kwamba ni muhimu kujifunza kusoma. Hata hivyo, huenda ukaona kwamba wazo la kusoma kitabu au hata makala katika gazeti ni kama kumeza dawa: Unajua kwamba itakufaidi, lakini ungependa kuiepuka.

Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji vijana kutoka nchi 11 ili kuchunguza maoni yao kuhusu magumu na manufaa ya kusoma. Walisema yafuatayo.

Kwa nini ni vigumu kwako kusoma?

“Ni vigumu kwangu kupata wakati wa kusoma.”—Semsihan, 19, Ujerumani.

“Kusoma si kazi rahisi. Ninafikiri mimi ni mvivu kidogo.”—Ezekiel, 19, Filipino.

“Sipendi kulazimishwa kusoma habari zenye kuchosha.”—Christian, 15, Uingereza.

“Ikiwa kitabu ni chembamba, ninaweza kukisoma. Lakini iwapo ni kinene, hicho huniogopesha.”—Eriko, 18, Japani.

“Mimi hukengeushwa kwa urahisi. Siwezi kukaza uangalifu.” —Francisco, 13, Afrika Kusini.

Vijana Wakristo hutiwa moyo wasome Biblia. (Zaburi 1:1-3) Je, ni vigumu kwako kufanya hivyo? Ikiwa ndivyo, kwa nini?

“Biblia ni kitabu kikubwa sana! Mimi huona kwamba sitaweza kukimaliza maishani mwangu!”—Anna, 13, Urusi.

“Sehemu fulani za Biblia ni ngumu kueleweka na hazifurahishi sana.”—Jezreel, 11, India.

“Ni vigumu kwangu kusoma Biblia kwa ukawaida kwani ratiba yangu imevurugika sana.”—Elsa, 19, Uingereza.

“Ni vigumu kwangu kwa sababu wakati wangu mwingi huishia katika kazi za nyumbani na za shuleni.”—Zurisadai, 14, Mexico.

“Ni vigumu kwangu kusoma Biblia kwa sababu nimeshindwa kupunguza wakati ninaotumia kufanya mambo ninayopenda.”—Sho, 14, Japani.

Ni wazi kwamba inaweza kuwa vigumu kusoma. Lakini je, kujitahidi kufanya hivyo kuna faida yoyote? Umefaidikaje kwa kusoma?

“Kusoma kumepanua ujuzi wangu, na hilo limefanya niwe na uhakika zaidi ninapozungumza na watu.”—Monisha, 14, India.

“Kusoma hunistarehesha na kunifanya nisahau matatizo yangu.”—Alison, 17, Australia.

“Kusoma hunifanya nisafiri hadi maeneo ambayo singeweza kutembelea.”—Duane, 19, Afrika Kusini.

“Kusoma hunisaidia nijichunguzie mambo badala ya kutegemea mambo ambayo wengine huniambia.”—Abihú, 16, Mexico.

Ni nini ambacho kimekusaidia ufurahie kusoma?

“Tangu nilipokuwa mtoto mchanga, wazazi wangu wamenitia moyo nisome kwa sauti.”—Tanya, 18, India.

“Wazazi wangu walinitia moyo nitumie uwezo wangu wa kufikiri ninaposoma, nipige picha akilini mambo yanayoendelea.” —Daniel, 18, Uingereza.

“Baba alipendekeza kwamba nianze kwa kusoma vitabu vya Biblia ambavyo vinanivutia zaidi, kama vile Zaburi na Methali. Sasa mimi hufurahia kusoma Biblia badala ya kuiona kuwa mzigo.”—Charene, 16, Afrika Kusini.

“Nilipokuwa na umri wa miaka minne, tayari wazazi wangu walikuwa wamenipa meza na rafu iliyokuwa na vitabu vyote ambavyo walikuwa wamenikusanyia tangu nilipozaliwa.”—Airi, 14, Japani.

Kwa nini unafikiri ni muhimu kusoma Biblia?

“Watu huamini mambo mengi yasiyo ya kweli kuhusu Biblia. Ni afadhali kujichunguzia mambo hayo.” (Matendo 17:11)—Matthew, 15, Marekani.

“Unahitaji kuwa na akili unapotumia Biblia. Lakini kuisoma kumenisaidia kuzungumza kwa uhakika na waziwazi ninapowaeleza wengine imani yangu.” (1 Timotheo 4:13)—Jane, 19, Uingereza.

“Ninaposoma Biblia, mimi huhisi kana kwamba Yehova anazungumza nami moja kwa moja. Nyakati nyingine inagusa hisia zangu.” (Waebrania 4:12)—Obadiah, 15, India.

“Ninajifunza kufurahia kusoma Biblia kwa sababu hiyo hunieleza yale ambayo Yehova anafikiria kunihusu nayo hunipa mashauri mazuri.” (Isaya 48:17, 18)—Viktoriya, 14, Urusi.

Wewe hupataje wakati wa kusoma Biblia na vichapo vya Biblia?

“Nina ratiba. Mimi husoma sura moja ya Biblia kila asubuhi mara tu ninapoamka.”—Lais, 17, Brazili.

“Mimi husoma Biblia na vichapo vingine vya Kikristo ndani ya gari la moshi ninaposafiri kuelekea na kutoka shuleni. Nimefaulu kudumisha ratiba hiyo kwa miaka minne sasa.”—Taichi, 19, Japani.

“Mimi husoma sehemu ndogo ya Biblia kila usiku kabla ya kulala.” —Maria, 15, Urusi.

“Mimi husoma kurasa nne za ‘Mnara wa Mlinzi’ au ‘Amkeni!’ kila siku. Mimi hufaulu kumaliza gazeti lote kabla ya lile linalofuata kufika.”—Eriko, 18, Japani.

“Mimi husoma Biblia kila asubuhi kabla ya kwenda shuleni.”—James, 17, Uingereza.

Kama maelezo hayo yanavyoonyesha, kusoma kunaweza kukupa uhakika, na kupanua ujuzi wako. Kusoma Biblia na vichapo vya Biblia, kutia ndani gazeti hili, pia kutakusaidia ‘umkaribie Mungu.’ (Yakobo 4:8) Hivyo, hata ukiona kwamba ni vigumu kusoma, usikate tamaa!

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini ni muhimu kwako kusoma Neno la Mungu?

▪ Unawezaje ‘kujinunulia wakati’ wa kusoma Biblia na vichapo vya Biblia?—Waefeso 5:15, 16.

[Sanduku katika ukurasa wa 16]

HUSIANISHA MAMBO UNAYOSOMA NA YALE UNAYOJUA

Husianisha mambo unayosoma na yale ambayo unajua kujihusu na kuhusu mazingira yako. Jiulize maswali yafuatayo:

Inahusianaje na Habari Uliyosoma Je, mambo na matatizo yanayofafanuliwa hapa, yanafanana na hadithi au mambo mengine ambayo nimesoma katika vitabu au magazeti? Je, wahusika wana tabia zinazofanana na za watu wengine ambao nimejifunza kuwahusu?

Inakuhusuje Habari hii inahusianaje na hali zangu, utamaduni wangu, na matatizo yangu? Je, ninaweza kutumia habari hii kukabiliana na matatizo au kuboresha maisha yangu?

Inahusianaje na Mazingira Yako Habari hii inanifundisha nini kuhusu mambo ya asili, mazingira, utamaduni mbalimbali, au matatizo katika jamii? Habari hii inanifundisha nini kuhusu Muumba?