Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

“Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.”—AYUBU 33:25.

MBWA anapokufa akiwa na miaka 10 au 20, huenda ikawa amefanya mambo mengi ambayo kwa kawaida mbwa hufanya. Huenda akawa amelea watoto, akafukuza paka, akazika mifupa, na kumlinda bwana wake. Lakini mwanadamu anapokufa akiwa na umri wa miaka 70 au 80, huwa ametimiza mambo machache sana kati ya mambo ambayo angeweza kufanya. Ikiwa alipenda michezo, labda alikuwa mahiri katika mchezo mmoja au miwili tu. Ikiwa alipenda muziki, huenda ikawa alijua kucheza vizuri ala moja au mbili tu. Ikiwa alipenda kuzungumza na watu katika lugha yao, pengine alizungumza kwa ufasaha lugha mbili au tatu tu. Angeweza kufurahia mambo mengi zaidi kama vile kukutana na watu, kugundua vitu vipya, na kumkaribia Mungu zaidi iwapo tu angeweza kuishi muda mrefu zaidi.

Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu amuumbe mwanadamu akiwa na akili yenye uwezo wa kufurahia mambo mengi hivyo, kisha amkatishe tamaa kwa kutomwezesha aishi muda mrefu vya kutosha kufurahia mambo hayo?’ Maisha mafupi ya mwanadamu hayapatani na ubuni ulio na kusudi ambao unaonekana wazi katika uumbaji. Pia huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu amuumbe mwanadamu akiwa na sifa za pekee kama vile haki na huruma na wakati huohuo ampe mwelekeo wa kutenda mabaya?’

Ukiona gari zuri likiwa limebonyea, je, utakata kauli kwamba liliundwa hivyo? La hasha! Bila shaka utakata kauli kwamba gari hilo halikupaswa kuwa hivyo. Lazima iwe lilitengenezwa vizuri, lakini baadaye mtu fulani akaliharibu. Vivyo hivyo, tunapofikiria jinsi ambavyo mwanadamu ameumbwa kwa njia ya ajabu, tunaweza kukata kauli kwamba maisha ya mwanadamu hayakukusudiwa yawe jinsi yalivyo leo. Maisha yetu mafupi na mwelekeo wa kutenda mabaya ni kama mibonyeo mibaya. Ni wazi kwamba mtu fulani aliharibu vibaya sana uhai mkamilifu wa wanadamu. Ni nani aliyefanya hivyo? Biblia inaonyesha waziwazi mtu huyo ni nani.

Ikiwa hapo mwanzo wanadamu waliumbwa waishi milele, ni nani ambaye baadaye angeweza kuharibu uhai mkamilifu wa wanadamu? Inaweza kuwa tu babu ya wanadamu wote. Mwanadamu mwingine yeyote angeweza tu kuharibu chembe za urithi za wanadamu wachache, yaani, wazao wake. Kwa hiyo, Neno la Mungu, Biblia, linapatana na ukweli huo wa mambo, linaposema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu, mwanadamu wa kwanza] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote.” (Waroma 5:12) Kwa hiyo, Biblia inasema kwamba Adamu ndiye wa kulaumiwa kwa kuharibu uhai wetu mkamilifu. Maisha ya mwanadamu yalikusudiwa yaweje tangu mwanzo?

Kuelewa Kusudi la Kuumbwa kwa Wanadamu

Biblia inaposema kwamba kifo ‘kiliingia katika ulimwengu,’ inaonyesha kwamba mwanzoni wanadamu hawakukusudiwa wafe. Wanadamu wanazeeka na kufa kwa sababu mwanadamu wa kwanza alimwasi Mungu. Kwa upande mwingine, wanyama hawakukusudiwa waishi milele.—Mwanzo 3:21; 4:4; 9:3, 4.

Watu waliumbwa kwa njia tofauti na wanyama. Uhai wetu ni wa hali ya juu zaidi kuliko wa wanyama, kama vile uhai wa malaika ulivyo wa hali ya juu kuliko wa wanadamu. (Waebrania 2:7) Tofauti na wanyama, mwanadamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:27) Pia, tofauti na wanyama, Biblia inamtaja Adamu kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Kwa hiyo, tuna sababu nzuri ya kuamini kwamba mwanadamu hakukusudiwa azeeke na kufa. Mungu hafi, wala hakuwaumba watoto wake wafe.—Habakuki 1:12; Waroma 8:20, 21.

Tunaelewa zaidi kusudi la Mungu la kuumba wanadamu, tunapochunguza rekodi za kihistoria kuhusu vizazi vya kwanza vya wanadamu. Wakati huo, watu waliishi mamia ya miaka kabla ya kuzeeka. Adamu aliishi miaka 930. Vizazi vichache baadaye, Shemu, mwana wa Noa, aliishi miaka 600 tu, naye Arpakshadi, mjukuu wa Noa akaishi miaka 438. * (Mwanzo 5:5; 11:10-13) Baadaye, Abrahamu aliishi miaka 175. (Mwanzo 25:7) Inaonekana kwamba hatua kwa hatua dhambi imeathiri muda ambao wanadamu wanaishi, na hivyo kupunguza muda huo kadiri miaka ilivyopita tangu wanadamu wapoteze ukamilifu. Lakini mwanzoni mwanadamu aliumbwa aishi milele. Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kujiuliza, ‘Je, bado Mungu anataka watu wafurahie kuishi milele duniani?’

Kukombolewa Kutokana na Kuzeeka

Kwa kuwa Yehova Mungu alikuwa amesema kwamba mtu yeyote asiyemtii angelipia dhambi yake kwa kufa, ilionekana kwamba wazao wa Adamu walikuwa katika hali isiyokuwa na tumaini. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, Maandiko yaliyoongozwa na roho, yalitoa tumaini la kwamba mtu fulani angelipa ili kuwakomboa watu kutokana na kuzeeka. Tunasoma hivi: “Mwachilie ili asishuke chini kuingia shimoni! Nimepata fidia! Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.” (Ayubu 33:24, 25; Isaya 53:4, 12) Katika andiko hili, Biblia inatoa tumaini zuri kwamba mtu fulani angelipa fidia ili kuwakomboa watu kutokana na kuzeeka!

Ni nani angeweza kulipa fidia hiyo? Bei ya fidia haingeweza kununuliwa kwa pesa. Ikizungumza kuhusu wanadamu wasio wakamilifu, Biblia inasema: “Hakuna hata mmoja wao anayeweza kumkomboa hata ndugu, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake . . . hivi kwamba yeye aendelee kuishi milele.” (Zaburi 49:7-9) Hata hivyo, Yesu Kristo alikuwa na kitu fulani chenye thamani zaidi kuliko pesa. Alipokuwa duniani, alikuwa na uhai mkamilifu wa kibinadamu. Kwa kuwa alikuwa Mwana wa Mungu, alilindwa asirithi dhambi ya Adamu. Yesu alisema kwamba alikuja “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” Pindi nyingine alisema hivi: “Nimekuja ili wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.”—Mathayo 20:28; Yohana 10:10.

Tumaini la kuishi milele ndilo lililokuwa jambo kuu katika mahubiri ya Yesu. Pindi moja, Petro ambaye alikuwa mfuasi wake mwaminifu alimwambia hivi: “Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:68) Biblia humaanisha nini inapotaja uzima wa milele?

Uzima Usiokoma

Mitume wa Yesu walitazamia wakati ambapo wangefurahia kuishi milele mbinguni wakiwa sehemu ya serikali ya Ufalme wa Yesu. (Luka 22:29; Yohana 14:3) Hata hivyo, mara nyingi Yesu alizungumza kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. (Mathayo 5:5; 6:10; Luka 23:43) Hivyo, miujiza na mafundisho ya Yesu kuhusu uzima wa milele yanathibitisha ahadi ambazo Mungu alitoa mapema sana kupitia nabii Isaya ambaye aliandika hivi: “Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Maisha ya wanadamu hayatakuwa tena miaka michache tu ya ujana yakifuatiwa na miaka ya kudhoofika na kuchakaa.

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, wakati ambapo wanadamu waaminifu watakuwa wakamilifu, watafurahia uhuru kutokana na kuzeeka. Biblia inasema: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Wazia! Watu wataendelea kupata hekima na uzoefu. Lakini kadiri miaka itakavyosonga, hawatapoteza kamwe nguvu zao za ujana. Je, utakuwa hai wakati huo?

Utaishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Kulingana na Yesu, kutakuwa na watu wachache sana duniani baada ya siku ya Mungu ya hukumu. (Mathayo 24:21, 22) Yesu alisema: “Barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.

Ili uwe kati ya watu watakaofurahia kuishi milele, unahitaji kutafuta kibali cha Mungu. Hatua ya kwanza ni kumjua Mungu. Yesu alieleza: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Ni kweli kwamba jitihada inahitajiwa ili kumjua Mungu vizuri; lakini, jitihada hiyo ina manufaa. Vivyo hivyo, jitihada inahitajiwa ili kupata pesa za chakula cha kila siku. Akilinganisha ujuzi kumhusu Mungu na chakula, Yesu alihimiza hivi: “Fanyeni kazi, si kwa ajili ya chakula ambacho huharibika, bali kwa ajili ya chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele.” (Yohana 6:27) Bila shaka, inafaa kujitahidi kadiri uwezavyo ili kupata uzima wa milele.—Mathayo 16:26.

Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa hiyo, muda ambao utaishi unategemea jinsi unavyoitikia upendo wa Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Watu fulani wanadai kwamba miaka inayotajwa katika simulizi hilo la Biblia ni miezi. Hata hivyo, andiko hilo linasema kwamba Arpakshadi alimzaa Shela akiwa na umri wa miaka 35. Tukichukua miaka hiyo kuwa miezi 35, basi Arpakshadi alimzaa mwana wake kabla ya kufikia umri wa miaka mitatu. Ni wazi kwamba hilo haliwezekani. Isitoshe, sura za kwanza za Mwanzo zinatofautisha miaka ya jua na miezi.—Mwanzo 1:14-16; 7:11.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Mwanadamu akiwa na umri wa miaka 80, huwa ametimiza mambo machache sana kati ya mambo ambayo angeweza kufanya

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Wanadamu waliumbwa wakiwa na uhai wa hali ya juu zaidi kuliko wanyama

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, gari hili lilitengenezwa likiwa limebonyea?

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Neno la Mungu linasema kwamba wanadamu watarudia ‘siku za nguvu za ujana wao’