Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?

Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?

Maoni ya Biblia

Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?

JIBU la swali hilo ni muhimu kwetu. Kwa nini? Kwa sababu Adamu na Hawa walipokosa kumtii Mungu, hilo liliathiri wanadamu wote hadi wakati wetu. Biblia inasema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Lakini kwa nini tendo rahisi la kuchukua na kula tunda kutoka kwenye mti liwe na matokeo mabaya hivyo?

Mungu alipowaumba Adamu na Hawa, aliwaweka kwenye bustani nzuri iliyokuwa na mimea na miti mingi ya matunda ambayo wangeweza kula. Walikatazwa tu mti mmoja, yaani, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Kwa kuwa walikuwa na uhuru wa kuchagua, Adamu na Hawa wangeweza kuchagua kumtii Mungu au kutomtii. Hata hivyo, Adamu alikuwa ameonywa hivi: “Siku utakapokula [kutokana na mti wa ujuzi], utakufa hakika.”—Mwanzo 1:29; 2:17.

Kizuizi Kinachofaa

Kizuizi hicho kimoja hakikutokeza ugumu wowote; Adamu na Hawa wangeweza kula matunda ya miti mingine yote ya bustani. (Mwanzo 2:16) Isitoshe, katazo hilo halikudokeza kwamba wanadamu hao walikuwa na maelekeo ya kutenda mabaya, wala halikuwapokonya adhama yao. Ikiwa Mungu angekuwa amewakataza mambo maovu kama vile kufanya ngono na wanyama au kuua, wengine wangeweza kudai kwamba wanadamu wakamilifu walikuwa na maelekeo fulani mabaya ambayo wangepaswa kuyazuia. Hata hivyo, kula kulikuwa jambo la kawaida na linalofaa.

Je, tunda lililokatazwa lilikuwa ngono kama watu fulani wanavyoamini? Biblia haiungi mkono maoni hayo. Jambo moja linalopaswa kuzingatiwa ni kwamba Mungu alipoweka katazo hilo, Adamu alikuwa peke yake na yaonekana aliendelea kuwa peke yake kwa muda fulani. (Mwanzo 2:23) Pili, Mungu aliwaambia Adamu na Hawa ‘wazae, wawe wengi na kuijaza dunia.’ (Mwanzo 1:28) Bila shaka, hangewaamuru wavunje amri yake kisha awahukumu kifo kwa kufanya hivyo! (1 Yohana 4:8) Tatu, Hawa alikula tunda hilo kabla ya Adamu kisha baadaye akampa mumewe. (Mwanzo 3:6) Ni wazi kwamba tunda hilo halikuwa ngono.

Wajaribu Kujiamulia Mema na Mabaya

Mti wa ujuzi ulikuwa mti halisi. Hata hivyo, uliwakilisha haki ya Mungu akiwa Mtawala ya kuamulia wanadamu mema na mabaya. Kwa hiyo, kula matunda ya mti huo hakukuwa tu wizi, yaani, kuchukua kitu kilichokuwa mali ya Mungu, bali pia kulikuwa jitihada ya kujiamulia mema na mabaya. Ona kwamba baada ya kumdanganya Hawa kwamba iwapo yeye na mume wake wangekula tunda hilo, ‘hawangekufa hakika,’ Shetani alisisitiza hivi: “Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:4, 5.

Hata hivyo, Adamu na Hawa walipokula tunda hilo hawakupata ufahamu kama wa Mungu kuhusu mema na mabaya. Kwa kweli, Hawa alimwambia Mungu: “Yule nyoka—alinidanganya.” (Mwanzo 3:13) Hata hivyo, alijua amri ya Mungu, hata alimtajia tena nyoka, aliyetumiwa na Shetani. (Ufunuo 12:9) Kwa hiyo, tendo lake lilikuwa kutotii kimakusudi. (Mwanzo 3:1-3) Hata hivyo, Adamu, hakudanganywa. (1 Timotheo 2:14) Badala ya kuwa mshikamanifu kwa Muumba wake na kumtii, alimsikiliza mke wake na kufuata mwenendo wake wa kujitegemea.—Mwanzo 3:6, 17.

Kwa kutangaza msimamo wao wa kujitegemea, Adamu na Hawa waliharibu uhusiano wao pamoja na Yehova kwa njia isiyoweza kurekebika na wakapatwa na madhara ya kudumu ya dhambi, kufikia kiwango cha kuathiri chembe zao za mwili. Ni kweli kwamba waliishi kwa mamia ya miaka, lakini walianza kufa “siku” ambayo walitenda dhambi, sawa na vile tawi huanza kufa linapokatwa kutoka kwenye mti. (Mwanzo 5:5) Isitoshe, kwa mara ya kwanza, walihisi hawana amani ya akili. Walitambua kwamba walikuwa uchi na wakajaribu kujificha Mungu asiwaone. (Mwanzo 3:7, 8) Pia walihisi kuwa wana hatia, wakakosa usalama, na wakaona aibu. Dhambi yao ilisababisha mvurugo, na dhamiri zao zikaanza kuwashutumu kuwa wametenda mabaya.

Ili kutekeleza neno lake na kushikamana na viwango vyake vitakatifu, kwa haki Mungu aliwahukumu kifo Adamu na Hawa na kuwafukuza kutoka kwenye shamba la Edeni. (Mwanzo 3:19, 23, 24) Hivyo, Paradiso, furaha, na uzima wa milele vikapotea, kisha kukatokea dhambi, kuteseka, na kifo. Hilo lilikuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini kwa jamii ya kibinadamu! Hata hivyo, mara tu baada ya kuwahukumu Adamu na Hawa, Mungu aliahidi kuondoa madhara yote yanayotokana na dhambi yao bila kukiuka viwango vyake vya uadilifu.

Yehova alikusudia kufanya iwezekane kwa wazao wa Adamu na Hawa wakombolewe kutokana na dhambi na kifo. Alitimiza hilo kupitia Yesu Kristo. (Mwanzo 3:15; Mathayo 20:28; Wagalatia 3:16) Kupitia Yesu, Mungu ataondoa dhambi na madhara yake yote na kufanya dunia yote iwe paradiso kama alivyokusudia hapo mwanzo.—Luka 23:43; Yohana 3:16.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Tunajuaje kwamba tunda lililokatazwa halikuwa ngono?—Mwanzo 1:28.

▪ Kula tunda lililokatazwa kuliwakilisha nini?—Mwanzo 3:4, 5.

▪ Mungu amefanya mipango gani ili kuondoa madhara ya dhambi?—Mathayo 20:28.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Tunda lililokatazwa halikuwa ngono

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Hawa alitaka kuwa kama Mungu, ajiamulie mema na mabaya