Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kutumiaje Pesa Zangu Vizuri?

Naweza Kutumiaje Pesa Zangu Vizuri?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kutumiaje Pesa Zangu Vizuri?

“Mara nyingi, mimi hujipata nikipanga kununua kitu nisichohitaji kwa sababu tu kimepunguzwa bei, na huenda hata nisiwe na pesa za kukinunua.”—Anna, * Brazili.

“Nyakati nyingine marafiki wangu hunialika twende tafrija za pesa nyingi. Nataka kuwa pamoja na marafiki wangu, kufurahia pamoja nao. Hakuna mtu anayependa kusema, ‘Siwezi kuja, sina pesa.’”—Joan, Australia.

JE, WEWE huona kwamba huna pesa za kutosha za matumizi? Kama tu ungepewa pesa nyingi kidogo za kutumia, ungeweza kununua mchezo fulani unaotaka. Kama tu ungepewa mshahara mkubwa, ungeweza kununua viatu ambavyo “unahitaji.” Hata hivyo, badala ya kuhangaikia pesa ambazo huna, mbona usijifunze kutumia vizuri pesa ulizo nazo?

Ikiwa wewe ni kijana na unaishi na wazazi wako, huenda ukataka kungoja hadi wakati utakapoishi peke yako ndipo ujifunze kupangia pesa zako. Lakini kufanya hivyo ni sawa na kuruka kutoka kwenye ndege kabla ya kujifunza kwanza jinsi ya kutumia parachuti. Ni kweli kwamba huenda mtu akagundua jinsi ya kutumia parachuti hiyo anapokuwa juu angani. Hata hivyo, ingefaa zaidi kama angejifunza jinsi ya kuitumia kabla ya kuruka!

Vivyo hivyo, wakati mzuri zaidi wa kujifunza jinsi ya kupangia pesa zako ni kabla hujajionea mwenyewe hali ngumu za kiuchumi. “Pesa ni ulinzi,” akaandika Mfalme Sulemani. (Mhubiri 7:12) Lakini pesa zitakulinda ikiwa tu utajifunza jinsi ya kuzitumia vizuri. Kufanya hivyo kutakufanya uwe na uhakika zaidi na kutafanya wazazi wako wakuheshimu hata zaidi.

Jifunze Mambo ya Msingi

Je, umewahi kuwauliza wazazi wako wakueleze mambo yanayohusika katika kuitunza familia? Kwa mfano, je, unajua wao hulipa pesa ngapi kila mwezi kwa ajili ya umeme na maji, na unajua inagharimu pesa ngapi kudumisha gari, kununua chakula, na kulipa kodi ya nyumba? Huenda usipendezwe na mambo hayo. Hata hivyo, kumbuka kwamba unachangia gharama hizo. Isitoshe, utakapoondoka nyumbani, itakubidi uanze kulipia vitu hivyo. Hivyo unapaswa kujua huduma hizo hugharimu pesa ngapi. Waulize wazazi wako wakuonyeshe hati ya madai ya huduma hizo, na usikilize kwa makini wanapokueleza jinsi ambavyo wao hupanga kuzilipa.

“Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi, naye mtu mwenye uelewaji ndiye anayepata mwongozo stadi,” inasema methali moja ya Biblia. (Methali 1:5) Anna, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii anasema, “Baba yangu alinifundisha jinsi ya kupangia matumizi ya pesa, naye akanionyesha umuhimu wa kutumia pesa za familia vizuri.” Pia, mama ya Anna alimfundisha mambo mengine muhimu. Anna anasema: “Alinionyesha umuhimu wa kulinganisha bei ya kitu katika maduka mbalimbali kabla ya kukinunua.” Anaendelea kusema, “Mama angeweza kutimiza mambo mengi akiwa na pesa kidogo tu.” Anna amenufaikaje? Anasema: “Sasa naweza kutumia pesa zangu vizuri. Mimi hutumia pesa zangu kwa uangalifu, kwa hiyo niko huru na nina amani ya akili kwa kuwa sina madeni yasiyo ya lazima.”

Tambua Vizuizi

Ni kweli kwamba ni rahisi kuzungumza kuhusu kutumia pesa vizuri lakini ni vigumu kufanya hivyo hasa ikiwa unaishi na wazazi wako nawe hupewa pesa za matumizi au wewe hupata mshahara. Kwa nini? Kwa sababu huenda ikawa wazazi wako ndio wanaolipa gharama za mahitaji. Hivyo huenda ukabaki na kiasi kikubwa cha pesa ambacho unaweza kutumia utakavyo. Na inafurahisha kutumia pesa utakavyo. “Mimi hutumia pesa kwa urahisi, nami hufurahia jambo hilo,” anasema Paresh, kijana kutoka India. Sarah, kutoka Australia, ana maoni hayohayo. Anasema: “Mimi husisimuka ninaponunua vitu.”

Kwa kuongezea, marafiki wako wanaweza kukukaza utumie pesa nyingi kuliko ulivyopanga. Ellena, msichana mwenye umri wa miaka 21, anasema: “Marafiki wangu huona kununua vitu kuwa aina fulani ya tafrija. Nikiwa pamoja nao ni kana kwamba tumefanya mapatano kwamba lazima mtu anunue vitu ili ajifurahishe.”

Ni jambo la kawaida kutaka ukubaliwe na marafiki wako. Lakini jiulize, ‘Je, ninatumia pesa nyingi nikiwa na marafiki wangu kwa sababu nina pesa hizo au kwa sababu ninalazimika kufanya hivyo?’ Watu wengi hutumia pesa ili waheshimiwe na marafiki wao na watu wengine. Hilo linaweza kusababisha matatizo makubwa ya kifedha, hasa ikiwa una kadi ya mkopo. Mshauri wa mambo ya kifedha, Suze Orman, anaonya hivi: “Ikiwa unataka kuwavutia wengine kwa vitu ulivyo navyo badala ya sifa zako nzuri, umo katika hatari ya kuingia katika madeni kwa sababu ya kutumia kadi ya mkopo vibaya.”

Badala ya kutumia kadi yako ya mkopo hadi ufikie kiwango cha juu zaidi cha pesa unachoruhusiwa au kutumia mshahara wako wote siku moja, kwa nini usifuate mapendekezo ya Ellena? Anasema hivi: “Ninapoenda tafrija na marafiki wangu, mimi hupanga mapema kiasi cha pesa nitakachotumia. Mshahara wangu hutumwa moja kwa moja kwenye akaunti yangu ya benki, nami hutoa tu pesa ninazohitaji kwa wakati huo. Mimi huona kuwa ni jambo la hekima kwenda kununua vitu na marafiki ambao hutumia pesa zao kwa uangalifu na wale ambao watanitia moyo kwanza nilinganishe bei ya kitu katika maduka mbalimbali badala ya kukinunua katika duka la kwanza.”—Methali 13:20.

Jifunze Kutoka kwa Wazazi Wako

Hata kama hufanyi kazi ya kuajiriwa au kupewa pesa za matumizi, bado unaweza kujifunza mambo muhimu kuhusu pesa ukiwa bado unaishi na wazazi wako. Kwa mfano, unapowaomba wazazi wako pesa au kuwauliza wakununulie kitu fulani, huenda wakakataa. Kwa nini? Huenda sababu moja ikawa kwamba wazazi wako hawana pesa za ziada za kukununulia kitu hicho. Kwa kukataa, ingawa wangependa kukununulia kitu hicho, wazazi wako wanakuwekea mfano mzuri wa sifa ya kujizuia. Sifa hiyo ni muhimu unaposhughulika na pesa.

Tuseme kwamba wazazi wako wanaweza kukupa pesa au kukununulia kitu hicho. Huenda bado wakakataa kufanya hivyo. Huenda ukadhani kwamba wao ni wachoyo tu. Lakini fikiria jambo hili: Pengine wanajaribu kufundisha jambo muhimu, kwamba si lazima upate chochote unachotaka ili uwe na furaha. Biblia inasema hivi kuhusu jambo hilo: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.

Ukweli wa maneno hayo unaungwa mkono na mambo ambayo yamewapata vijana wengi ambao wazazi wao huwanunulia kila kitu wanachotaka. Punde si punde, vijana hao hugundua kwamba hawaridhiki. Hata wawe na vitu vingi kadiri gani, bado wao hutaka kuwa na vitu zaidi. Baada ya muda, huenda vijana ambao wamezoea kupata kila kitu wanachotaka wakakua na kuwa watu wazima wasio na shukrani. Sulemani alionya hivi: “Mtu akimbembeleza mtumishi [au mwana] wake tangu ujanani, katika maisha yake ya baadaye hata atakuwa mtu asiye na shukrani.”—Methali 29:21.

Pesa Ni Wakati

Tamaduni fulani huwa na msemo, Wakati ni pesa. Hilo linakazia kwamba lazima watu watumie wakati kuchuma pesa kwani kupoteza wakati ni kupoteza pesa. Msemo ulio kinyume cha huo ni kweli pia, yaani, pesa ni wakati. Ukitumia pesa vibaya, unaharibu wakati uliotumia kuchuma pesa hizo. Ukijifunza kutumia pesa zako vizuri utakuwa unajifunza kutumia wakati wako vizuri. Jinsi gani?

Fikiria maneno ya Ellena. Anasema hivi: “Ninapotumia pesa vizuri, ninaamua kiasi cha pesa nitakazochuma. Ninapopangia matumizi ya pesa na kufuata ratiba hiyo, silazimiki kufanya kazi kwa saa nyingi ili kulipia madeni makubwa. Sasa ninatumia maisha na wakati wangu vizuri.” Je, wewe pia ungependa kutumia maisha yako vizuri?

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Je, wewe huona ni vigumu kutumia pesa zako vizuri? Kwa nini?

▪ Kwa nini unapaswa kuepuka kupenda pesa?1 Timotheo 6:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

JE, KUWA NA PESA NYINGI ZAIDI NDILO SULUHISHO?

Je, kuwa na pesa nyingi kutakusaidia usitumie pesa vibaya? “Sote hufikiri kwamba mshahara mnono ndilo suluhisho kwa matatizo yetu ya kifedha, lakini mara nyingi haiwi hivyo,” anasema Suze Orman, mshauri wa mambo ya kifedha.

Fikiria mfano huu: Ikiwa unaendesha gari na ushindwe kulidhibiti au una zoea la kuliendesha ukiwa umefunga macho, je, kuongeza petroli kwenye gari lako kutafanya uhisi kuwa salama zaidi? Je, utafika mahali unakoenda salama? Vivyo hivyo, usipojifunza kutumia pesa vizuri, kuchuma pesa nyingi zaidi hakutaboresha hali.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

CHUKUA HATUA

Ulitumia pesa ngapi mwezi uliopita? Ulizitumiaje? Hujui? Zifuatazo ni hatua ambazo unaweza kuchukua ili kutumia pesa zako vizuri.

Weka rekodi. Kwa angalau mwezi mmoja, weka rekodi ya pesa ambazo umepokea na tarehe ambayo ulizipokea. Andika kila kitu unachonunua na bei yake. Mwishoni mwa mwezi, jumlisha kiasi ulichopokea na kiasi ulichotumia.

Pangia matumizi ya pesa. Chora safu tatu kwenye karatasi. Katika safu ya kwanza, andika pesa zote ambazo unatazamia kupokea mwezi huo. Katika safu ya pili, andika jinsi unavyopanga kutumia pesa hizo; tumia mambo uliyoandika kwenye rekodi yako kama mwongozo. Siku zinapopita, andika kwenye safu ya tatu kiasi unachotumia kwa vitu ulivyopanga kununua. Pia, andika kitu chochote ulichonunua ambacho hukuwa umepangia.

Punguza matumizi yako. Ikiwa unatumia pesa nyingi zaidi kuliko ulivyopanga na unaanza kuwa na madeni, punguza matumizi yako. Lipa madeni yako. Tumia pesa zako vizuri.

[Chati]

Kata na utumie jedwali hii!

Matumizi Yangu ya Kila Mwezi

Mapato Vitu ninavyopanga kununua Kiasi cha pesa nilichotumia

malipo chakula

kazi ya muda mavazi

mambo mengine simu

vitumbuizo

michango

akiba

mambo mengine

 

 

Jumla Jumla Jumla

 

[Picha]

Kumbuka kwamba ukitumia pesa vibaya unaharibu wakati uliotumia kuzichuma

[Picha katika ukurasa wa 11]

Waulize wazazi wako wakuonyeshe jinsi ya kupangia matumizi ya pesa