Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waliokoka kwa Kutii Maonyo

Waliokoka kwa Kutii Maonyo

Waliokoka kwa Kutii Maonyo

ILIKUWA Jumatano, Agosti 24, 2005, siku yenye joto jingi huko New Orleans, Louisiana, Marekani. Alan na familia yake waliondoka nyumbani kwa siku chache na kwenda Beaumont, Texas, zaidi ya kilometa 300 upande wa magharibi. Walibeba nguo ambazo wangetumia kwa siku tano. Alan anaeleza hivi: “Hatukujua kwamba Tufani inayoitwa Katrina, ilikuwa ikianza mashariki ya Florida. Hata hivyo, kufikia Ijumaa usiku ilikuwa wazi kwamba New Orleans ingekumbwa na tufani mbaya sana.”

Jumapili, Agosti 28, ilikuwa wazi kwamba tufani hiyo iliyoitwa Katrina ingekuwa kubwa sana. Meya wa New Orleans aliwaamuru watu wahame jiji hilo. Kufuatia amri hiyo, maelfu ya magari yalisonga polepole kuelekea kaskazini na magharibi, na hivyo kukawa na msongamano mkubwa wa magari. Maelfu ya watu ambao hawakuwa na magari walikimbilia makao ya kujikinga au kwenye ukumbi mkubwa wa michezo unaoitwa Superdome. Wengine waliamua kukaa nyumbani hadi tufani hiyo ipite.

‘Wakati Ujao, Nitakuwa wa Kwanza Kuondoka!’

Joe, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuwa miongoni mwa watu ambao hawakuhama. Aliamini kwamba angeweza kuokoka tufani hiyo akiwa nyumbani. Alijiambia kwamba madhara yaliyosababishwa na tufani zilizotokea awali hayakuwa mabaya kama wenye mamlaka walivyokuwa wametabiri. “Nilifikiri kwamba nitaokoka,” anasema. “Baada ya muda mfupi tu nilibadili maoni yangu! Upepo na mvua zilikuja kwa fujo. Kwa ghafula, paa la nyumba yangu liling’olewa. Kisha maji yakaanza kuongezeka kwa kiwango cha kutisha, meta 3 baada ya saa tatu! Maji yalikuwa yakiingia kwa kasi sana hivi kwamba ilinibidi kupanda kwenye orofa ya pili. Niliogopa sana kwa sababu upepo ulikuwa ukivuma, nazo kuta zilizokuwa zikiyumbayumba zilionekana kana kwamba zilikuwa karibu kuporomoka. Dari lilikuwa likianguka. Sasa nilikuwa nikifikiria jinsi ninavyoweza kutoroka.

“Nilidhani kwamba huenda ningeruka ndani ya maji yaliyokuwa yakienda kasi. Lakini kulikuwa na mawimbi hatari. Povu lilikuwa likipeperushwa kwenye barabara zilizokuwa karibu. Nilijua kwamba ikiwa ningeruka, ningekufa maji.”

Hatimaye, Joe aliokolewa na mashua iliyompeleka hadi kwenye daraja fulani. Maiti na kinyesi kilielea kila mahali. Usiku mmoja, Joe alilala ndani ya buti la gari. Kisha akasafiri kwa helikopta na basi hadi kwenye Kituo cha Jamii cha New Orleans. Anasema hivi: “Watu huko walinitendea kwa fadhili. Ilifika wakati ambapo nilianza kuzungumza kwa njia isiyoeleweka. Hangaiko langu kubwa lilikuwa, ‘Nitapata wapi maji ya kunywa?’”

Joe anapokumbuka mambo yaliyotukia, anatambua kwamba angeweza kuepuka mambo yaliyompata. “Nimejifunza jambo muhimu,” anasema. “Wakati ujao tutakapoambiwa ‘Hameni,’ nitakuwa wa kwanza kuondoka!”

Alipuuza Maonyo, Akakimbilia Mtini

Majiji ya Biloxi na Gulfport, yaliyo kwenye pwani ya Mississippi, yaliharibiwa vibaya sana na watu wengi wakafa. Kulingana na gazeti The New York Times la Agosti 31, 2005, Vincent Creel, meneja wa masuala ya umma wa Biloxi, alisema hivi: “Watu wengi walipuuza amri ya kuhama kwa sababu wao au nyumba zao ziliokoka Tufani iliyoitwa Camille [mnamo 1969].” Ilidhaniwa kwamba tufani hiyo ilikuwa na nguvu kuliko Katrina, lakini Creel alisema kwamba Katrina ‘ilisukuma maji mengi yanayoweza kulinganishwa na tsunami kwani yalikuwa kama ukuta usioweza kuzuiwa.’

Inell, aliyeishi Biloxi kwa muda mrefu alikuwa mmoja wa wakazi waliopuuza maonyo. Anasema: “Tulikuwa tumeokoka dhoruba nyingi zilizotokea miaka iliyopita. Kwa hiyo sikuwa na wasiwasi sana kuhusu Katrina.” Baada ya Inell kukusanya mama-mkwe wake mwenye umri wa miaka 88, mwana wake, binti yake, na mwana-mkwe wake, pamoja na mbwa wawili na paka watatu, waliamua kutohama nyumba yao iliyokuwa imejengwa vizuri. Kisha dhoruba ikapiga Biloxi karibu saa 4 asubuhi, Agosti 29. Inell anakumbuka: “Niliona maji yakivuja ndani ya chumba kimoja cha kulala kilichokuwa upande wa nyuma wa nyumba. Kisha yakaanza kuingia kupitia kila mahali. Tuliamua kuingia kwenye dari ili tuwe salama. Lakini maji yaliendelea kuingia. Tulilazimika kutoka kwenye dari ili tusikwame huko. Lakini tungeenda wapi?

“Ilimbidi mwana wangu atoboe shimo kwenye wavu wa waya ili tuweze kuogelea na kutoka nje. Tuliendelea kuelea kwa kujishikilia kwenye ncha ya paa. Watatu kati yetu tulielekea upande wa kulia wa nyumba naye binti yangu akaelekea upande wa kushoto. Niliona mti mkubwa karibu. Mimi, mwana wangu, na mama-mkwe, tuliogelea hadi kwenye mti huo na kuushikilia kwa nguvu. Kisha nikamsikia binti yangu akilia kwa sauti kubwa, “Mama! Mama!” Mwana-mkwe wangu, ambaye alikuwa wa mwisho kutoka kwenye dari, aliogelea ili kumwokoa. Walifaulu kuingia ndani ya mashua iliyokuwa imeegeshwa barabarani na ambayo ilikuwa ikielea karibu na nyumba. Walinihimiza niingie kwenye mashua hiyo. Sikutaka kujihatarisha kwa kuingia kwenye mashua hiyo kwa kuwa maji yalikuwa yakizunguka-zunguka upesi mahali hapo. Nilihisi nikiwa salama juu ya mti nami sikutaka kwenda popote.

“Nikiwa juu ya mti huo, niliona maji yakitiririka barabarani na kuzunguka nyumba. Nilianza kufikiria hali hiyo na kujiona kuwa mpumbavu kwa kutotii maonyo ya kuhama.

“Mwishowe, maji yalianza kupungua, na hatimaye sote tuliingia ndani ya mashua! Gari la zima-moto lilitokea na kutupeleka hospitali. Tulifurahi sana kuwa hai!”

Mpango wa Mashahidi wa Kuhamisha Watu

Katrina ilisababisha madhara kwenye pwani ya majimbo ya Marekani yanayopakana na Ghuba ya Mexico. Maelfu ya nyumba ziliharibiwa kutoka Louisiana kuelekea mashariki hadi Alabama. Lakini ni jambo la kawaida kwa tufani kutokea katika eneo hilo la Marekani. Kwa hiyo, kwa miaka kadhaa, Mashahidi wa Yehova wamekuwa tayari na mpango wa kuhamisha watu. Kila mwaka, hasa katika mwezi wa Juni, kabla ya msimu wa dhoruba kuanza, makutaniko 21 ya Mashahidi wa Yehova ya jimbo la New Orleans na maeneo yanayolizunguka hupitia mpango wa kuhamisha watu wakati wa dharura. Kwa hiyo, Mashahidi wengi walijua hatua walizopaswa kuchukua iwapo hali ya dharura ingetokea. Je, mpango huo ulifaulu Tufani Katrina ilipotokea?

Mara tu wasimamizi wa jiji walipowaamuru watu wahame, wazee katika kila kutaniko waliwasiliana na washiriki wa makutaniko yao na kuwatia moyo waondoke jiji hilo. Wengi walifaulu kuondoka pamoja na familia au rafiki zao. Mipango ya pekee ilifanywa ili kuwasafirisha na kuwasaidia wazee na wagonjwa. John, ambaye ni mshiriki wa halmashauri ya Mashahidi ya kutoa misaada, alisema, “Kwa kweli ninaamini kwamba kwa kufuata mpango huo tuliokoa watu wengi.” Hivyo, Mashahidi wengi wa Yehova waliweza kuhama jiji hilo kabla ya dhoruba hiyo kupiga. Ili kutoa msaada mara moja kwa maeneo yaliyoathiriwa, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Marekani ilianzisha halmashauri za kutoa misaada ya dharura.

Kuwatafuta Mashahidi Ndani ya Ukumbi wa Michezo

Wakimbizi wapatao 16,000, wengi wao kutoka Louisiana, walikuwa wakipewa chakula, maji, na makao katika ukumbi wa michezo wa Astrodome huko Houston, Texas. Halmashauri ya Mashahidi ya kutoa misaada huko Houston ilipata habari kwamba kulikuwa na Mashahidi kadhaa kati ya umati huo mkubwa. Lakini wangewatafutaje?

Mapema asubuhi ya Ijumaa, Septemba 2, kikundi cha wazee Wakristo walienda kuwatafuta akina ndugu kwenye ukumbi huo. Walishangaa kuwaona maelfu ya wanaume, wanawake, matineja, watoto na vitoto waliokuwa wamejaa katika ukumbi huo mkubwa. Uwanja huo wa mpira ulikuwa umejaa maelfu ya vitanda vidogo. Nao wakimbizi walikuwa wakisubiri kutatuliwa matatizo yao. Watu wengi walikuwa wamepanga mistari mirefu ili kupokea matibabu nao wafanyakazi wa kitiba walikuwa wakikimbia kuwapeleka wagonjwa kwenye ambulansi.

“Nilihisi kana kwamba nilikuwa katikati ya kambi ya wakimbizi,” akasema Samuel, mmoja wa wazee aliyekuwa akiwatafuta Mashahidi wenzake. Wangewapataje Mashahidi wachache kati ya umati huo mkubwa? Wazee hao walianza kuwatafuta kwa kutembea kwenye vijia wakiwa na mabango makubwa ya kuwaomba Mashahidi wajitambulishe. Baada ya kufanya hivyo kwa muda wa saa tatu bila mafanikio walitambua kwamba walihitaji kutumia mbinu nyingine inayofaa zaidi. Waliwaomba wafanyakazi wa shirika la Msalaba Mwekundu watangaze hivi kwa kutumia vikuza-sauti: “Mashahidi wote wa Yehova waliobatizwa, tafadhali nendeni kwenye jukwaa lililo upande wa chini wa mashariki mwa ukumbi.”

Hatimaye, Mashahidi walianza kumiminika mahali hapo huku wakitabasamu. Samuel anasema: “Walikuwa wakitokwa na machozi ya furaha. Walitukumbatia kwa nguvu na kutushika mikono. Hawakutaka kutuachilia kwa kuogopa wasipotee katikati ya umati.” Ijumaa na Jumamosi, Mashahidi 24 walipatikana na kupelekwa kwenye kituo cha kutoa misaada cha Mashahidi.

Wengi wao walikuwa wamepoteza kila kitu isipokuwa tu mavazi machafu waliyokuwa wamevaa. Shahidi mmoja alikuwa amebeba sanduku dogo lililotoshana na katoni ya viatu. Lilikuwa na hati muhimu ambazo ndizo tu aliweza kuokoa dhoruba hiyo kali ilipotokea.

Katika ukumbi huo, watu wengi walitambua kwamba wazee hao waliokuwa wamewatembelea ni Mashahidi wa Yehova nao waliwakaribia na kuwaomba Biblia na vichapo vya Biblia. Waliomba Biblia zaidi ya 220. Mashahidi hao pia waliwapa watu toleo la Amkeni! la Julai 22, 2005, lililokuwa na makala zilizofaa wakati huo zenye kichwa “Je, Misiba ya Asili Inaongezeka?”

Wengine Warudi Makwao

Mmoja wa watu waliookoka dhoruba hiyo ni ripota ambaye amefanya kazi hiyo kwa muda mrefu na pia ni meneja mkuu wa kituo cha televisheni cha New Orleans. Kwa sababu ya kazi yake, ameona uharibifu mwingi wakati uliopita. Alirudi nyumbani kwake huko Jefferson, Louisiana, ili kuchukua vitu fulani. Anasema hivi: “Nilipigwa na butwaa. Kila kitu kiliharibiwa kabisa. Kwenye televisheni, tulikuwa tumeona jinsi maji kutoka kwenye mifereji yalivyofurika yalipobomoa mabomba ya kuzuia maji. Lakini upepo wenye nguvu pia ulisababisha uharibifu mkubwa. Nyumba yangu ilikuwa imeharibiwa kabisa. Kuna kuvu, vitu vilivyooza, na uvundo. Kuna uvundo mbaya sana. Hali ni mbaya sana. Lakini angalau bado tuko hai.”

Mwishowe Alan, aliyetajwa mwanzoni, alirudi nyumbani kwake huko Metairie, kitongoji kilicho magharibi mwa New Orleans. Dhoruba hiyo ilikuwa imesababisha uharibifu mkubwa. “Lilikuwa jambo lenye kusikitisha, lenye kushangaza,” anasema. “Ni kana kwamba bomu la atomu lilikuwa limeangushwa kwenye jiji hilo. Kuna tofauti kati ya kusikia kuhusu mambo hayo kwenye redio au kuyatazama kwenye televisheni na kutembea au kuendesha gari katika eneo ulilokuwa ukiishi na kuona hasara na uharibifu huo mkubwa. Uharibifu huo hauelezeki.

“Kwa mfano, kulikuwa na uvundo, uvundo wa nyama iliyooza, harufu ya kifo. Majengo mengi ya biashara yaliharibiwa kabisa au kufurika maji. Kulikuwa na polisi na majeshi kila mahali. Lilikuwa kama eneo la vita.”

Jitihada Fulani za Kutoa Misaada

Wasimamizi wa jiji, wa jimbo, na wa serikali walifanya mipango ya kutoa misaada. Shirika kuu la serikali la kutoa misaada lilikuwa FEMA (Shirika la Serikali la Kushughulikia Hali ya Dharura la Marekani). Mashirika mengine yalishirikiana kuwasaidia maelfu ya wahasiriwa. Kiasi kikubwa cha chakula, nguo, na maji kilisafirishwa hadi kwenye maeneo yaliyoathiriwa vibaya na dhoruba. Punde si punde, shirika la FEMA lilianza kuwapa watu hundi na misaada mingine ya kifedha ili kuwasaidia kwa siku au majuma machache ya kwanza. Wakati huo Mashahidi wa Yehova walikuwa wakikabilianaje na hali?

Kukagua Uharibifu na Kufanya Marekebisho

Baada tu ya dhoruba hiyo kutokea, Mashahidi walipanga vikundi vya kukagua uharibifu na kuvituma kwenye maeneo yaliyoathiriwa ili kujua ni nyumba ngapi za Mashahidi na Majumba ya Ufalme yaliyokuwa yameharibiwa. Wangefanyaje kazi hiyo kubwa? Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, huko Brooklyn, New York, liliidhinisha halmashauri za kutoa misaada zianzishwe chini ya mwongozo wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani. Kisha, Halmashauri za Ujenzi za Mkoa kutoka sehemu nyingi za Marekani zikaalikwa zianze kujenga upya. * Zimetimiza nini?

Kufikia Februari 17, 2006, kikundi cha kutoa misaada cha Long Beach, Mississippi, kiliripoti kwamba katika eneo lao nyumba 632 za Mashahidi zilizokuwa zimeharibiwa, 531 zilikuwa zimerekebishwa kabisa, na 101 zilihitaji kurekebishwa. Pia Mashahidi waliwasaidia majirani ambao si Mashahidi. Majumba ya Ufalme 17 yalikuwa yameharibiwa paa kabisa, na kufikia katikati ya Februari, majumba 16 yalikuwa na mapaa mapya. Vipi halmashauri ya Baton Rouge, Louisiana?

Kikundi hicho hushughulikia eneo la Louisiana ambalo lilipigwa vibaya zaidi na Tufani Katrina. Kati ya nyumba 2,700 za Mashahidi ambazo zilihitaji kurekebishwa, nyumba 1,119 zilikuwa zimemalizwa kufikia katikati ya Februari, kwa hiyo bado halmashauri hiyo ya kutoa misaada ina kazi nyingi ya kufanya. Pia, majirani na familia zilizokuwa na uhitaji mkubwa zilisaidiwa. Majumba ya Ufalme 50 yaliharibiwa vibaya. Kufikia Februari, majumba 25 yalikuwa yamerekebishwa. Huko Texas, kikundi cha Houston kilihitaji kurekebisha nyumba 871 zilizokuwa zimeharibiwa na Tufani Rita iliyotukia Septemba. Kufikia Februari 20, nyumba 830 zilikuwa zimekamilishwa.

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Katrina

Maelfu ya watu walioathiriwa na Katrina wamejifunza kwamba ni muhimu kutii maonyo. Kwa kweli, wengi wanaweza kusema hivi kama alivyosema Joe aliyetajwa mapema: “Wakati ujao tutakapoambiwa ‘Hameni,’ nitakuwa wa kwanza kuondoka!”

Mashahidi wa Yehova wanaendelea kutoa msaada kwa watu walioathiriwa na tufani katika eneo la Ghuba ya Mexico. (Wagalatia 6:10) Hata hivyo, huduma yao si kutoa misaada ya kimwili tu. Tofauti na hilo, kazi kuu ya Mashahidi wa Yehova ambayo inafanywa katika nchi 235 ulimwenguni pote, ni kutoa onyo muhimu zaidi kuliko lile la dhoruba inayokaribia. Biblia inatabiri kwamba hivi karibuni Mungu atakomesha mfumo huu wa mambo usiomwogopa, asafishe dunia yetu na kuirudisha katika hali aliyokusudia. Ikiwa ungependa kujua yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu wakati huo wa hukumu, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lako au waandikie kwa kutumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoonyeshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili.—Marko 13:10; 2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 14:6, 7; 16:14-16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 32 Halmashauri za Ujenzi za Mkoa hufanyizwa na vikundi vya Mashahidi wa Yehova waliojitolea ambao wana uzoefu mwingi wa kujenga na kurekebisha Majumba ya Ufalme. Kuna vikundi 100 hivi kotekote Marekani na pia vingine vingi ulimwenguni pote.

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Picha ya setilaiti ya Tufani Katrina

[Hisani]

NOAA

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mafuriko huko New Orleans

[Hisani]

AP Photo/David J. Phillip

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tufani Katrina iliharibu majengo na kusababisha vifo vya watu wengi

[Hisani]

AP Photo/Ben Sklar

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Ukumbi wa Astrodome huko Houston, Texas, ulitumiwa na watu 16,000 hivi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wazee Wakristo waliwatafuta Mashahidi kati ya watu waliohamishwa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mashahidi walishukuru sana kurekebishiwa nyumba zao

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wajitoleaji warekebisha paa lililoharibiwa vibaya

[Picha katika ukurasa wa 18]

Pia wajitoleaji waliandaa chakula

[Picha katika ukurasa wa 19]

Alan